Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi
wa Umma na Utawala Bora, Jenista Mhagama leo tarehe 5 Octoba, 2022 amefugua rasmi
mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI)
yanayofanyika jijini hapa na kutoa wito kwa uongozi wa shirikisho hilo kukutana
na Serikali ili kujadili njia bora, ikiwemo ongezeko la muda wa ushiriki katika
mashindano.
Akizungumza katika Uwanja wa Mkwakwani baada ya
kupokea maandamano ya wanamichezo kutoka taasisi mbalimbali wanaoshiriki katika
michezo hiyo, Waziri Mhagama alisema kuwa watumishi wa umma wakipata muda mrefu
wa kucheza wataweza kuonyesha umahiri na vipaji walivyonavyo, hivyo kuchangia
upatikanaji wa wachezaji wazuri katika ngazi ya vilabu na taifa kwa ujumla.
“Naomba kutoa wito kwa SHIMIWI, washiriki wa michezo
wanaongezeka, timu zinaongezeka, hebu tukae na Serikali tujadili, naona huko
mbele inatupasa kuongeza muda wa uwepo wa michezo hii, kwani muda uliopo
hautoshi. Tungependa kuona watumishi wa umma wanapata nafasi ya kucheza, lakini
siyo kucheza tu, wanaonyesha umahiri na vipaji vyao ili mwisho wa siku tuache
kuagiza (wachezaji nje), tunataka wawe watumishi wa umma hapa nchini,” alisema.
Waziri Mhagama alisema kuwa uwepo wa muda wa kutosha
katika kushiriki kwenye mashindano hayo kutayafanya yawe na tija na kusaidia nchi
kuwa na timu bora ambazo zinaweza kushindana kwenye medani za kitaifa kutoka
katika wafanyakazi au watumishi wa umma nchini.
“Napenda kuishukuru Wizara ya Utamaduni na Michezo kwa
kusimamia utekelezaji wa maelekezo ya Serikali kuhakikisha michezo inadumishwa
nchini na wananchi wote Tanzania, wakiwemo watumishi wote wa umma, wanapata
fursa ya kushiriki, hivyo kujikinga na maradhi yasiyoambukiza kupitia michezo,”
alisema.
Waziri huyo akatoa wito kwa SHIMIWI kuandaa programu maalumu
ya mashindano itakayoshirikisha Wizara mbalimbali kushindana kila mwezi jijini
Dodoma ili kuendeleza michezo, hatua itakayosaidia kuinua ari ya watumishi wa umma
kufanya mazoezi kila siku na kujiandaa na ratiba ya michezo ya kila mwezi.
Kadhalika, Waziri Mhagama aliishauri SHIMIWI kuwa
karibu na vyama vya michezo ambavyo vinautalaamu wa kutosha ili kusaidia kupata
ubobezi katika medani za michezo ya namna mbalimbali ambayo wamekuwa
wakishiriki.
Alitumia nafasi hiyo kuwaagiza waajiri wote kutoa
ruhusa kwa watumishi kwa ajili ya kujiandaa na mashindano hayo kwani kuja
kwenye mashindano ni jambo moja na maandalizi ni jambo jingine na wala
haipendezi kwa mwanamichezo kuja kwenye mashindano bila kujiandaa.
Aidha, aliwakumbusha watumishi hao kuongozwa na
maadaili ya utumishi wa umma kwani suala hilo siyo la mjadala wala hiari. Akawataka
kufuata taratibu za utumishi wa umma na kuhakikisha kila mmoja wao anazingatia
sheria na taratibu zilizowekwa na shirikisho.
Waziri huyo aliwapongeza wakuu wa taasisi za umma na
wakala wa serikali kwa kuwaruhusu wachezaji kufanya maandalizi na kuja
kushiriki kwenye michezo hiyo kwani ameshuhudia watumishi wakiwa wamewezeshwa
kusafiri, kupata stahili na stahiki za kujikimu kwa kipindi chote watakapokuwa Tanga.
“Tumeshuhudia taasisi zilizoweza kuwawezesha
wanamichezo kupata mavazi nadhifu ya michezo na leo uwanja umependeza sana.
Nitoe wito kwa taasisi ambazo hazijajiandaa vizuri mwakani zijitahidi kufanya
hivyo,” alisema.
Awali, akizungumza katika halfa hiyo, Naibu Waziri wa
Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo Pauline Gekul aliwapongeza wanamichezo wote
kwa kuonyesha utayari wa kushiriki kwenye michezo hiyo. Alitoa rai michezo hiyo
kuendeshwa kwa weledi na nidhamu ya hali ya juu ili kufikia malengo
yaliyokusudiwa.
“Michezo ni undugu, michezo ni afya na michezo ni
ajira. Ninaamini kwamba tutakapoondoka hapa Tanga tutakuwa tumeboresha haya
yote na ni azma ya Rais ambaye ameridhia tuendelee na michezo hii,” alisema.
Aliwakumbusha wanamichezo kuwa michezo ni taaluma
ambayo inahitaji nidhamu na weledi kama zilivyo taaluma zingine, hivyo ni imani
yake michezo hiyo itakuwa chachu ya upendo, mshikamano, amani na umoja kwa
watumishi wote na taifa kwa ujumla.
Kwa upande wake, Mwenyekiti wa SHIMIWI Daniel Mwalusamba
alimwambia Waziri Mhagama kuwa michezo ya mwaka huu (2022) imekuwa na mwitikio
mkubwa ukilinganisha na mwaka jana (2021). Alisema kuwa mwaka jana timu 47
zilishiriki kwenye michezo hiyo iliyofanyika mkoani Morogoro.
“Lakini mwaka huu timu zinazoshiriki ni 63, mwaka jana
ni mikoa 11 ilishiriki kwenye mashindano haya pale Morogoro, mwaka huu ni mikoa
18 inashiriki kwenye mashindano haya. Tunawashukuru viongozi wa mikoa kwa kuwa
na mwitikio na kuongeza ushiriki wa watumishi kutoka kwenye mikoa yao,”
alisema.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports)
inashiriki katika mashindano ya SHIMIWI kwenye michezo nane ambayo ni Kamba
Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe,
Riadha Wanaume na Wanawake pamoja na Baiskeli na tayari imeshaanza kutembeza
vipigo kwenye baadhi ya michezo hiyo kwenye hatua ya makundi.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa
Shaibu Kanyochole.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni