·Yamchanachana mtu mbele ya Waziri Mhagama
Na
Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports)
Netiboli leo tarehe 5 Octoba, 2022 imeichanachana Timu ya Kilimo na baadaye kuishindilia
vikapu 28:26 katika ufunguzi rasmi wa mashindano ya Shirikisho la Michezo ya
Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.
Mchezo huo ambao umechezwa katika Viwanja vya Bandari baada
ya Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala
Bora, Jenista Mhagama kufungua mashindano hayo ulianza majira ya mchana kwa
kasi huku timu zote zikishambuliana kwa zamu.
Timu ya Kilimo ilikuwa ya kwanza kubahatisha kutupia
vikapu kwenye lango la Mahakama. Muda mchache baadaye, Mahakama Sports walijibu
mapigo na kuanza kulishambulia lango la wapinzani wao kama nyuki na kuwafanya
wapoteane, hivyo kufanikiwa kutupia vikapu kadhaa.
Mchezo huo ambao ulichezwa kwa dakika 40 ulivutia
mashabiki wengi katika mashindano hayo ambapo baadhi ya timu pinzani ambazo
tayari zimeshagalagazwa na Mahakama Sports kwenye michezo mbalimbali
zilijitahidi kuishangilia timu ya Kilimo ili kuweza kuipa nguvu.
Hata hivyo, pamoja na janja janja hizo, wachezaji wa
Mahakama Sports waliunyamazisha umati wa washangiliaji wa timu pinzani baada ya
kuendeleza kichapo cha hapa na pale na kufanikiwa kujizolea kapu la magori
katika mpambano huo.
Wachezaji wa Mahakama Sports wanaoshiriki kwenye mashindano
ya SHIMIWI katika michezo mingine walitunishiana misuri na mashabiki wa timu
pinzani katika kushangilia timu zao na kufanikiwa kuwanyamazisha licha ya uchache
wao, hasa baada ya Mahakama kucheza kwa kujiamini na kwa ubora wa hali ya juu.
Hadi timu zinaenda mapumziko, Kilimo walikuwa
wanaoongoza kwa idadi ndogo ya vikapu. Kipindi cha pili kilipoanza, Mahakama
Sports ikazidisha mashambulizi na kulisakama lango la wapinzani wao mara kwa
mara huku wakitupia tupia vikapu kadri wanapofika kwenye eneo la timu hiyo.
Juhudi za wachezaji wa Mahakama za kuongeza
mashambulizi na umakini katika mchezo zililipa na hadi mechi hiyo inamalizika
ikafanikiwa kuondoka na ushindi wa vikapu hivyo 28 kwa 26 walizoambulia Kilimo,
ambao hawakuamini kabisa kile kilichotokea, licha ya kupata kuungwa mkono na
taasisi zingine marafiki kwenye ushangiliaji.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Mwalimu wa Timu
Mtumwa Sululu amewapongeza wachezaji wa timu yake kwa kuendeleza vichapo kwenye
mashindano hayo na ameahidi timu itakayokumbana nayo huko mbele ya safari
itakumbana na kichapo kikali zaidi.
"Nawapongeza sana vijana wangu kwa ushindi huu,
kwa kweli wamecheza vizuri ingawa mechi ilikuwa ngumu kiasi chake maana
inaonekana wapinzani wetu walikuwa wametukamia sana. Lakini wachezaji wangu
wamesimama imara kabisa katika kuitetea timu yao na hatimaye wameibuka na
ushindi," alisema.
Kabla ya kuanza kwa mchezo huo, Waziri Mhakama
alizikagua timu zilioshiriki kwenye ufunguzi huo na kuzitakia heri katika
mashindano hayo.
Wachezaji wanaoiwakilisha Mahakama Sports kwenye
mchezo huo wa Netiboli ni Filomena Haule, Upendo Mapunda, Nyangi Saimora,
Veronica Kajobi, Dianes Akanganyila, Shani Ally, Tarita Kayuni, Marikia Nondo,
Margaret Kanyaga, Agnes Kilian, Jackline Paul, Adeudata Mkonkosha, Sharifa Selemani,
Sophia Songoro, Taus Mwambujale, Agness Mwanyika na Kuruthum Mkundawatu.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa
Shaibu Kanyochole.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni