Jumamosi, 1 Oktoba 2022

MAHAKAMA SPORTS GUMZO MASHINDANO SHIMIWI TANGA

·Kutoa dozi kutwa mara tatu kwa kila timu.

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) imewasili jijini Tanga leo tarehe 1 Octoba,2022 kushiriki mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI).

Kuwasili kwa Timu hiyo inayoshiriki katika michezo nane mwaka huu ya Kamba Wanaume na Wanawake, Mpira wa Miguu Wanaume, Netiboli, Bao, Karata, Tufe, Riadha Wanaume na Wanawake pamoja na Baiskeli kumezua gumzo kwenye viunga mbalimbali jijini hapa na kufanya baadhi ya wapinzani kuanza kuweweseka.

Hatua hiyo inaonekana kuwakatisha tamaa wapinzani wa Mahakama Sports baada ya kusikia minong'ono  ya chini chini kuwa timu hiyo ya Mahakama mwaka huu haipo vizuri na haitashiriki mashindano.

"Jamaa wameshafika, sijui itakuwaje mwaka huu. Tusipojipanga vizuri tutabaki kuwa wasindikizaji tu katika mashindano haya. Hawa jamaa ni hatari, hasa kwenye mchezo wa Kamba, aisee wapo vizuri sana. Hatuwawezi hawa," alisikika mwanamichezo mmoja ambaye hakufahamika anatoka taasisi gani.

Akizungumza muda mchache baada ya kufika Tanga, Katibu wa Mahakama Sports Donald Tende amesema wanamichezo wote wamefika salama na wapo tayari kwa mashindano.

"Wachezaji wote wapo vizuri na tupo tayari kwa michezo ambayo ipo mbele yetu. Kama kawaida yetu, Mahakama inatoa haki, tutatoa haki sawa kwa wakati na kwa wote bila upendeleo wowote, tunaomba wapinzani wetu walijue hilo,” alisema.

Tende ameonya kuwa haki watakayotoa kwa kila mpinzani itaenda sanjari na dozi ya ‘kutwa mara tatu’ kwa kila mpinzani atakayejitutumua na kutunisha misuri. "Safari hii hatubakishi kitu kwenye mashindano haya, tuna wachezaji wazuri sana mwaka huu kwenye kila mchezo tunaoshiriki," alisema.

Mwalimu wa Timu Spear Mbwembwe amesema mara baada ya kuwasili wachezaji wote wataenda moja kwa moja kambini kujiwinda na mechi kesho tarehe 2 Octroba, 2022 kwenye michezo yote. "Hatuna muda wa kupoteza, Mahakama Sports haipoi. Tunataka dozi tutakazotoa ziwe takatifu, nadhani wapinzani wetu wanalijua hili," alisema.

Kwa mujibu wa ratiba ya mashindano, Mahakama Sports Kamba Wanaume imepangwa kwenye kundi A pamoja na Ikulu, Dodoma RAS na Haki na itaanza kupeperusha bendera ya Mahakama ya Tanzania kwa kutunishiana misuri na Haki kesho tarehe 2 Octoba, 2022 na baadaye itakutana na RAS Dodoma tarehe 4 Octoba, 2022 kabla ya kumaliza mzunguko wa makundi na Ikulu tarehe 6 Octoba, 2022.

Ratiba hiyo inaonyesha Kamba Wanawake imepangwa kundi A na timu za Maji, RAS Kilimanjaro na Viwanda na katika mechi ya kwanza itakutana na Maji kesho tarehe 2 Octoba, 2022 na baadaye kupepetana na RAS Kilimanjaro tarehe 4 Octoba, 2022 na kumaliza kwenye kundi hilo na Viwanda tarehe 6 Octoba, 2022.

Mahakama Sports Mpira wa Miguu Wanaume imepangwa kundi D na timu za Tume ya Utumishi wa Umma, Ukaguzi na Hazina na itatupa karata yake ya kwanza kwa kumenyana na Ukaguzi kesho tarehe 2 Octoba, 2022 na baadaye kukutana na Hazina tarehe 4 Octoba, 2022 kabla ya kumaliza mechi za makundi tarehe 6 Octoba, 2022 kwa kukutana na Utumishi.

Katika Mpira wa Netiboli, Mahakama Sports imepangwa katika kundi H na timu za Ujenzi, Kilimo, Waziri Mkuu Kazi na RAS Mtwara na itaanza kupambana na RAS Mtwara kesho tarehe 2 Octoba, 2022 na baadaye kukutana na Ujenzi tarehe 4 Octoba, 2022. Tarehe 6 Octoba, 2022 Timu hiyo itakutana uso kwa uso na Waziri Mkuu Kazi, kabla ya kumaliza mechi za makundi kwa kukutana na Kilimo tarehe 7 Octoba, 2022.

Mashindano ya SHIMIWI ambayo yameanza leo tarehe 1 Octoba, 2022 yanatarajiwa kufunguliwa rasmi na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Kassimu Majaliwa tarehe 5 Octoba, 2022. Kauli mbiu ya mashindano ya SHIMIWI 2022 ni “Michezo hupunguza magonjwa yasiyo ambukiza na kuongeza tija mahala pa kazi.”

Mashindano hayo ambayo yanashirikisha michezo mbalimbali yatafanyika katika viwanja tofauti tofauti nane ambavyo ni Viwanja vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana.

Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira Wanaume wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya viongozi kabla ya kuanza safari kuelekea Tanga kwenye mashindano ya SHIMIWI.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa Netiboli wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya viongozi kabla ya kuanza safari kuelekea Tanga kwenye mashindano ya SHIMIWI.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanaume wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya viongozi kabla ya kuanza safari kuelekea Tanga kwenye mashindano ya SHIMIWI.
Wachezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake wakiwa katika picha ya pamoja na sehemu ya viongozi kabla ya kuanza safari kuelekea Tanga kwenye mashindano ya SHIMIWI.
Safari kuelekea Tanga imeiva.
Sehemu ya wachezaji (juu na chini) wakiwa ndani ya gari kuelekea Tanga.

Sehemu nyingine ya wachezaji (juu na chini) wakiwa ndani ya gari kuelekea Tanga.

Hodi Tanga, Majabali yanaingia.
Sehemu ya wachezaji (juu na chini) wakishuka kwenye gari baada ya kuwasili Tanga.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni