Ijumaa, 7 Oktoba 2022

MAHAKAMA SPORTS KAMBA WANAWAKE YAISAMBARATISHA VIWANDA

Na Faustine Kapama-Mahakama, Tanga

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake leo tarehe 7 Octoba, 2022 imekamilisha mechi yake ya mwisho ya makundi katika mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa baada ya kuisambaratisha Timu ya Viwanda.

Mchezo huo uliochezwa majira ya saa moja asubuhi katika Viwanja vya Shule ya Sekondari Usagala ulianza kwa kasi ambapo Viwanda walionekana kukamia, lakini wachezaji wa Mahakama walibaki kuwa watulivu muda wote, huku wakiwasoma wapinzani wao.

Mchezo ulipoanza katika mzunguko wa kwanza, Mahakama Sports hawakuwa na jambo jingine zaidi ya kutembeza kichapo kikali kwa mvuto moja na kuwaacha wapinzani wao wakipoteana huku wakiugulia maumivu waliyoyapata.

Nusura timu ya Viwanda igomee kurudi uwanjani katika mzunguko wa pili kufuatia kugalagazwa vibaya na mabingwa hao wa mchezo wa Kamba Wanawake katika mashindano hayo ya SHIMIWI.

Kama ilivyodhaniwa hapo awali, mzunguko wa pili ulipoanza timu ya Mahakama Sports haikuwa na huruma na mtu baada ya kuwasambaratisha wapinzani wao kwa mara nyingine kwa mvuto mmoja pekee, hivyo kujizolea pointi zote muhimu.

Akizungumza baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa Mahakama Sports Wilson Dede amewapongeza vijana wake kwa kuonyesha mchezo mzuri na wa kiungwana baada ya kuwavuta wapinzani wao kistaarabu.

"Nimeuangalia mchezo huo vizuri. Ni huruma tu ambayo imetumika kumaliza mchezo huu. Nina wasiwasi kwenye mechi zijazo atavunjwa mbavu mtu hapa. Mahakama Sports Kamba Wanawake siyo timu ya kuchezea, kaa nayo mbali, vinginevyo utaumia," alisema.

Mahakama Sports Kamba Wanawake imemaliza mechi zake za makundi kwa kushinda zote na kufanya iongoze kwenye kundi hilo. Ilicheza mechi yake ya kwanza ya makundi na RAS Singida ambapo ilitoa kichapo kikali.

Mechi yake ya pili ilikutana na Maji ambayo yalikamuliwa kisawasawa kwa mizungo miwili na katika mechi ya tatu ilipangiwa RAS Manyara ambao waliingia mitini baada ya kuogopa kupokea dozi iliyokuwa imeandaliwa kwa ajili yao.

Wachezaji wa Kamba Wanawake ni Zahara Abdallah, Beatrice Dibogo, Judith Mwakyalagwe, Melina Mwinuka, Dotto Mlandula, Rebecca Mwakabuba, Salma Mwamende, Sarafina Mkumbo, Mariam Mayala, Zawadi Amir, Namweta Mcharo, Valeria Ntyangili, Anna Hebron, Lucy Mbwaga, Rose Mwalongo na Tumaini Kizito.

Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa Shaibu Kanyochole.

Mashindano ya SHIMIWI ambayo yalianza tarehe 1 Octoba, 2022 na kufunguliwa rasmi tarehe 5 Octoba, 2022 yanafanyika katika viwanja tofauti tofauti ikiwemo Viwanja vya Mkwakwani, Shule ya Sekondari Popatlal, Galanos Sekondari, Bandari, Shule ya Tanga, Polisi Chumbageni na Viwanja vya Gymkhana. 

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake ikiwa katika picha ya pamoja kabla ya mvutano.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake ikiwa tayari kuwakabili Viwanda.
Timu ya Viwanda ikijiandaa kwa mtifuano.
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake (juu) ikiwakamua kisawasawa Viwanda (chini) ambao walipoteana baada ya kusambaratishwa vibaya.

Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Kamba Wanawake ikishangilia ushindi baada ya kuwasambaratisha Viwanda. Picha chini mashabiki wa Mahakama Sports wakiungana pamoja kusherekea ushindi.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni