·Baada ya kubanwa mbavu na Mahakama Sports Netiboli
Na
Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports)
Netiboli leo tarehe 6 Octoba, 2022 imeibamiza Timu ya Waziri Mkuu Kazi kwa vikapu
25:23 katika mechi ya mwisho ya makundi katika mashindano ya Shirikisho la
Michezo ya Wizara na Idara za Serikali (SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa.
Mchezo huo ambao umechezwa majira ya saa tano asubuhi katika
Viwanja vya Polisi Chumbageni ulitawaliwa na kosa kosa za kutupia vikapu vya hapa
na pale huku timu zote mbili zikishambuliana kwa zamu.
Ilikuwa Timu ya Mahakama Sports iliyofungua msululu wa
kutupia vikapu ambapo wachezaji wake walilisakama lango la wapinzani wao kila
mara. Hata hivyo, Timu ya Waziri Mkuu Kazi ilijitahidi kusawazisha mambo baada
ya kupata vikapu kadhaa kwa kutumia makosa yaliyofanywa na Mahakama Sports.
Hadi timu zinaenda kwenye mapumziko, Mahakama Sports
ilikuwa inaongoza kwa vikapu kadhaa. Kipindi cha pili kilipoanza, Timu ya Waziri
Mkuu ililisakama lango la Mahakama Sports, hasa katika dakika za mwazo na
kufanikiwa kutupia vikapu kadhaa, hatua iliyowafanya kuongoza kwenye mchezo huo.
Baada ya hapo, Mahakama Sports ilichachamaa na kuanza
kumkimbiza mwizi kimya kimya na kufanikiwa kusawazisha vikapu ambavyo timu
pinzani ilikuwa imetangulia kutupia na baadaye kupindua meza kwa kuwajaza
wapinzani hao vikapu vya haraka haraka.
Kitendo hicho kiliwanyamazisha mashabiki wa Timu ya Waziri
Mkuu Kazi waliokuwa wanashangilia kwa nguvu kila timu yao inapotupia kikapu.
Shangwe hizo zilihamia upande wa pili wa shilingi,
yaani Mahakama Sports baada ya wachezaji wake kukonga nyoyo zao, hasa baada ya
kutulia na kurudi kwenye mchezo na kulishambulia lango la Waziri Mkuu Kazi kama
nyuki.
Hadi mechi inamalizika, ubao wa matokeo ulikuwa
unasoma vikapu 25 kwa Mahakama Sports huku Timu ya Waziri Mkuu Kazi ikiambulia
vikapu 23 ilivyovitupia kufuatia makosa ya wachezaji wa Mahakama Sports.
Akizungumza baada ya mechi hiyo, Mwalimu wa Timu
Mtumwa Sululu aliwasifia wachezaji wa timu yake kwa kusahihisha makosa katika
kipindi cha pili, kitendo kilichoichanganya timu pinzani na kuifanya ipoteane.
"Tunashukuru tumepata matokeo mazuri na kumaliza
mechi zetu za makundi tukiwa katika nafasi nzuri. Kati ya mechi nne tumeshinda tatu
na kutoka sululu mechi moja. Nawapongeza sana vijana wangu kwa kufanya vizuri,”
alisema.
Katika mechi za makundi, Mahakama Sports ilianza kwa
kuiadhibu RAS Mtwara kwa vikapu 40:4 na baadaye kutoana jasho na Ujenzi kwa
kila timu kutupia vikapu 20. Baada ya hapo, Mahakama Sports ilikuta na Kilimo
na kuichanachana kwa vikapu 28:26.
Wachezaji wanaoiwakilisha Mahakama Sports kwenye
mchezo huo wa Netiboli ni Filomena Haule, Upendo Mapunda, Nyangi Saimora,
Veronica Kajobi, Dianes Akanganyila, Shani Ally, Tarita Kayuni, Marikia Nondo,
Margaret Kanyaga, Agnes Kilian, Jackline Paul, Adeudata Mkonkosha, Sharifa
Selemani, Sophia Songoro, Taus Mwambujale, Agness Mwanyika na Kuruthum
Mkundawatu.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa
Shaibu Kanyochole.
Mpira uliorushwa na mchezaji wa Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Netiboli ukitumbukia kwenye kikapu.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni