·Baada ya kuwashindilia Maendeleo ya Jamii magori sita
Na
Faustine Kapama-Mahakama, Tanga
Timu ya Mahakama ya Tanzania (Mahakama Sports) Mpira wa
Miguu Wanaume leo tarehe 7 Octoba, 2022 imetinga kibabe katika hatua ya 16 bora
kwenye mashindano ya Shirikisho la Michezo ya Wizara na Idara za Serikali
(SHIMIWI) yanayofanyika jijini hapa baada ya kuwashindilia Maendeleo ya Jamii
kwa magori 6:1.
Mchezo huo uliochezwa katika Viwanja vya Shule ya
Sekondari Galanosi majira ya saa tano asubuhi ulianza kwa kasi huku Mahakama
Sports ikilisakama goli la wapinzani wao na kufanikiwa kupachika bao katika
dakika ya kwanza ya mchezo huo kupitia kwa mshambuliaji wake hatari Martin
Mapinduzi.
Mapinduzi alipokea pasi mpenyezo kutoka kwa
mshambuliaji na Nahodha wa timu hiyo, Selemani Magawa kabla ya kufunga bao hilo.
Dakika ya tatu baadaye katika kipindi hicho cha kwanza, mshambuliaji huyo huyo
aliwainua mashabiki wa Mahakama Sports kwenye viti vyao baada ya kuiandikia timu
yake bao la pili baada ya kupokea pasi safi kutoka kwa winga wa kulia, Frank Odadia.
Baada ya kupachikwa kwa magori hayo, timu zote
zilianza kushambuliana kwa zamu na katika dakika ya 15 Maendeleao ya Jamii wakafanikiwa
kupata bao la kufutia machozi. Timu hiyo ililazimika kufanya mabadiliko ya
haraka haraka katika dakika ya 20 baada ya kuzidiwa kimchezo na kufanikiwa kuwazuia
Mahakama Sports kuendelea kulishambulia lango lao.
Hadi timu zote mbili zinaenda mapunziko, matokeo
yalikuwa 2:1 kwa Mahakama na Maendeleo ya Jamii, mtawaliwa. Katika kipindi cha pili,
Mahakama Sports ilifanya mabadiliko kadhaa ya wachezaji kwa kumtoa mfungaji wa
mabao yote mawili ya mwanzo, Martin Mpanduzi na kumwingiza Timoth Mwakisambwe.
Mwalimu wa Timu hiyo Spear Mbwembwe pia alimbadilisha Shamte
Seif na kumwingiza Beatus Simwanza na baadaye akamwingiza David Mnubi badala ya
Gabriel Tabana. Mabadiliko hayo yalileta uhai kwenye timu ya Mahakama Sports
ambao walikuwa wanalishambulia lango la wapinzani wao kama nyuki.
Katika dakika ya 50 ya mchezo, winga hatari Frank
Obadia akafanikiwa kuweka mpira kwenye kamba kwa kichwa baada ya mlinda mlango
wa timu ya Maendeleo ya Jamii kuutema mpira kufuatia shuti kali liliomshimnda
ambalo lilichezwa na mshambuliaji, Beatus Simwanza. Bao hilo liliiwezesha
Mahakama Sports kuongoza kwa mabao 3:1.
Kana kwamba haitoshi, Mahakama Sports ilizidisha
mashambulizi ambapo mshambuliaji hatari, nahodha wa timu na mchezaji nyota wa
mchezo huo, Selemani Magawa akafanikiwa kupachika bao safi kwa kichwa katika
dakika ya 60, hivyo kuiandikia timu yake bao la nne.
Kufungwa kwa bao hilo kuliamsha ari ya wachezaji wa
Mahakama Sports na kulisakama lango la timu pinzani mara kwa mara. Wachezaji wa
Mahakama Sports walikosa magori mengi ya wazi kwa kushindwa kuwa watulivu, hasa
wanapoingia kwenye miguu 18 karibu na lango la wapinzani wao.
Ilibidi mwalimu wao awatulize na kuanza kucheza pasi
fupifupi, mbinu ambayo ikafanikisha Mahakama Sports kuingia tena kwenye kamba katika
dakika ya 65 ya mchezo baada ya mchezaji wake Timoth Mwakisambwe anayechezea winga
ya kushoto kuupachika mpira kwenye wavu na kuiandikia timu yake bao la tano
baada ya kupokea pasi maridadi kutoka kwa Selemani Magawa.
Katika dakika za lala salama, mshambuliaji Beatus
Simwanza aliunganisha pasi safi kutoka kwa Timoth Mwakisambwe na kuukwamisha mpira
katika nyavu na kuiandikia timu yake bao la sita. Hadi mpira unamalizika, Mahakama
Sports ilikuwa imevuna mabao sita, huku Maendeleo ya Jamii ikiambulia bao moja
la kufutia machozi.
Akiongea baada ya mchezo huo, Mwenyekiti wa Mahakama
Sports Wilson Dede aliwapongeza vijana wake kwa kupigana kufa na kupona na
baadaye kupata ushindi mnono wa kalamu ya magori, ambayo hata wapinzani wao
hawakutegemea kupata kipigo kikali kama hicho.
“Nimefurahishwa sana, na nadhani kila mmoja wetu
amefurahishwa na matokeo haya. Ninawapongeza sana wachezaji wetu kwa kujituma
na kucheza kitimu. Matokeo haya yanatuweka katika nafasi nzuri ya kuendelea
kwenye hatua inayofuata, hongereni sana,” alisema.
Mwalimu Mbwembwe amewapongeza vijana wake kwa ushindi
huo na kwa kazi nzuri waliyoifanya. “Nimefurahi, nimefurahi sana. Vijana wangu
wamefanyia kazi yale niliyowaelekeza. Hawa jamaa (Maendeleo ya Jamii)
wanabahati sana. Tulikuwa tunawapiga zaidi ya bao 10 hawa. Lakini tumshukuru Mungu
hata kwa hiki tulichokipata, nawapa salamu wale watakaokumbana na sisi, wataumia,”
alisema.
Wachezaji wa Mpira wa Miguu walioiwakilisha Mahakama katika mchezo huo walikuwa Fahamu Kibona; Iman Patson; Gisbert Chentro; Akida Mzee; Emmanuel Mwamole; Selemani Magawa; Frank Obadia; Gabriel Tabana; Martin Mpanduzi; Mwinjuma Bwanga, Shamte Seif, Hassan Aufi; Nassoro Mwampamba; Kelvin Rutalemwa; Shabiru Hood; David Mnubi; Beatus Simwanza na Timoth Mwakisambwe.
Viongozi ambao wameambatana na Timu ni Mwenyekiti
Wilson Dede, Makamu Mwenyekiti Fidelis Choka, Katibu Mkuu Robert Tende, Katibu
Mkuu Msaidizi Theodosia Mwangoka, Mweka Hazina Rajab Ally, Timu Meneja Antony
Mfaume, Afisa Michezo Nkrumah Katagile na Mjumbe Mwakilishi wa SHIMIWI Taifa
Shaibu Kanyochole.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni