Jumapili, 17 Machi 2024

TANZANIA NCHI YA KWANZA BARANI AFRIKA KUTUMIA TTS; PROF. ELISANTE

Na Mary Gwera, Mahakama-Dodoma

Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amesema Tanzania ndio nchi ya kwanza barani Afrika kutumia Mfumo wa Unukuzi na Tafsiri (TTS) mahakamani.

Prof. Ole Gabriel ameyasema hayo leo tarehe 17 Machi, 2024 wakati Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria ilipotembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma kwa lengo la kukagua Mfumo huo.

“Kwa kifupi napenda niseme tu kwamba Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Utawala, Katiba na Sheria imeguswa na kuridhishwa na matumizi ya teknolojia hii na kwa Afrika, Tanzania ndio itakuwa Nchi ya kwanza kutumia Mfumo huu,” amesema Mtendaji Mkuu.

Amesema, Mahakama inazidi kuongeza kasi kwenda kidijiti na hakuna namna juhudi hizo zitarudi nyuma (no reverse gear) na kwamba kwa sasa Mhimili huo una mifumo ya Kitehama ipatayo 11.

Ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa ushirikiano ambao inaendelea kuipa Mahakama ya Tanzania katika kuboresha huduma zake.

Kadhalika, Prof. Ole Gabriel amesema kwamba, Mfumo wa TTS unasimamiwa na Idara ya TEHAMA kwa kushirikiana kwa karibu na Mamlaka ya Serikali Mtandao ‘e-GA’

“Napenda kuipongeza na kuishukuru Idara yetu ya TEHAMA ya Mahakama kwa kazi kubwa ya kusimika na kuboresha Mfumo wa TTS inayofanywa na Wataalam wetu wa ndani,” ameeleza Mtendaji Mkuu.

Ametoa rai kwa wananchi kutumia namba ya Huduma kwa Mteja 0752 500 400 ili kupata taarifa mbalimbali za Mhimili huo ikiwemo maboresho ya kidijitali.

Kwa upande wake, Mjumbe Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Alice Kaijage ameipongeza Mahakama kwa hatua iliyopiga.

"Mfumo huu ni mzuri na sisi kama Bunge tunafikiria kwa baadaye kama inawezekana tuweze kuutumia kwakuwa utapunguza kazi ya kuandaa 'hansard' za Bunge," amesema Mhe. Dkt. Alice.

 
Mtendaji Mkuu Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwaonesha Wajumbe wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria jinsi Mfumo wa Unukuzi na Tafsiri unavyofanya kazi leo tarehe 17 Machi, 2024 wakati Kamati hiyo ilipofanya ziara ya kuukagua Mfumo huo.
Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Joseph Muhagama (katikati), Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Pindi Chana (kushoto) pamoja na Wajumbe wengine wa Kamati hiyo wakimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) wakati akielezea Mfumo wa TTS leo tarehe 17 Machi, 2024.
Mjumbe Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Utawala, Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Alice Kaijage akiuzungumzia Mfumo wa TTS mara baada ya yeye pamoja na Wajumbe wenzake kuukagua Mfumo huo leo tarehe 17 Machi, 2024.



Hakuna maoni:

Chapisha Maoni