Jumatatu, 20 Mei 2024

BENKI YA DUNIA YAKOSHWA NA KASI YA MABORESHO YA MAHAKAMA

Na. Innocent Kansha- Mahakama

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete ameishukuru Mahakama ya Tanzania kwa niaba ya Banki ya Dunia kwa uamuzi wa busara wa kufanya kazi na Benki hiyo.

Akizungumza leo tarehe 20 Mei, 2024 alipotembelea Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha masuala ya familia Temeke jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake ya kukangua na kujifunza mambo mbalimbali ya maboresho yanayoendelea kustawisha utoaji haki nchini yanayofanywa na Mahakama kupitia mradi wa Banki ya dunia Bw. Belete amesema Mahakama ya Tanzania imefanya kazi kubwa ya kustawisha utoaji haki kwa wananchi wake.

“Mekuwa mara nyingi mkitushuru sisi lakini napenda kusema sisi ndiyo tunapaswa kuwashuru ninyi kwa kutupatia nafasi ya kufanya kazi nasi Benki ya Dunia na imani kubwa mnayoendelea kuonyesha kwetu. Tunawapongeza sana kwa kazi kubwa mnayoifanya ya kuboresha mazingira ya utoaji haki kwa wananchi,” amesema Mkurugenzi Mkazi Bw. Belete.

Bw. Belete amesema kuwa, kitu ambacho viongozi wengi wa nchi za Afrika wanapaswa kufanya ni kuhakikisha wanaboresha mifumo ya utoaji haki kwa wananchi wao ili kuhakikisha haki za wananchi zinalidwa kupitia mfumo wa utoaji haki ulio huru na wa uwazi.

“Kilicho nivutia katika ziara yangu leo ni pale nilipoambiwa kwamba watu wengi wa hali za kawaida wanakosa huduma nzuri za kimahakama. Uwepo wa Kituo cha kisasa kama hiki ni dhahili shairi kwamba Mahakama ya Tanzania imetoa dirisha la uhakika la kuwahudumia wananchi wake,” amesema Bw. Belete.

Bw. Belete amesema msingi wa maboresho ya miundombinu kama hiyo ni kusaidia kurahisisha utoaji haki, kupunguza gharama na kuondoa ucheleweshaji wa mashauri kwa wananchi wakati wa kutafuta haki.

Aidha, Mkurungezi hiyo ameongeza kuwa, kupitia vituo hivyo Mahakama ina nafasi ya kujifunga ili kuboresha miradi mingine inayoendelea kujengwa kwa kuboresha zaidi mazingira ya utoaji haki kwa kusanifu na kuongeza mambo mazuri zaidi ili kuimarisha utoaji haki kwa wananchi.

“Kitu kizuri kingine nilichojifunza kutoka Mahakama ni namna ambayo Mahakama inafanya kazi kwa kushirikiana na wadau wake katika mnyororo mzima wa utoaji haki. Nimeona wataalum mbalimbali kama vile kutoka ustawi wa jamii, dawati la njinsia, vyama vya kutoa msaada wa kisheria na wadau wengine. Hii inaonyesha kwamba Mahakama haijioni kama ndiyo kila kitu katika kutoa haki bali ushirikishwaji wa wadau ndiyo msingi wa maboresho,” ameongeza Mkurungenzi huyo.

Kwa upande wake Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amemshukuru Mkurugenzi huyo na ujumbe wa Benki ya Dunia kwa kuendelea kutoa ushirikiano kwa Mahakama katika safari ya maboresho na mageuzi makubwa ya kuboresha utoaji haki.

Mtendaji Mkuu amemuhakikishia Mkurugenzi Mkazi huyo kwamba, mikopo inayotolewa na inayoendelea kutolewa kwa masharti nafuu itaendelea kusimamiwa vizuri ili kuhakikisha inakidhi mahitaji halisi ya uboreshaji wa utoaji haki kwa ustawi wa wananchi.

Prof. Ole Gabriel amesema Mahakama ya Tanzania inatarajia kuanza ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba ikiwa ni sehemu ya kuendelea kuboresha miundombinu ya utoaji haki nchini.

“Maboresho makubwa yanayofanyika na yanayoendelea kufanyika mahakamani na kwa mafanikio makubwa siri yake ni ushirikiano uliopo anaotupa Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma. Jaji Mkuu ni mtu wa vitendo ni ni mtu wa matokeo, mtu asiye taka mzaha kwenye mambo ya muhimu kama uboreshaji wa huduma za kimahakama,” amesisitiza Prof. Ole Gabriel.

Aidha, Mtendaji Mkuu ameongeza kuwa pamoja na mambo mengine maboresho yamekuwepo pia katika upande wa mashauri Mwaka 2015 mashauri ya mlundikano yalikuwa asilimia 10 hadi 12 na kufika Mwaka 2023 Desemba mashauri ya mlundikano yamefikia asilimia tatu (3). Hakika kazi hiyo siyo ndogo hivyo akaushukuru ujembe wa Benki ya Dunia kwa ushirikiano waoutoa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Mahakama.

Prof. Ole Gabriel amesema lengo la Mahakama ni kuendelea kuboresha utoaji wa haki na huduma za kimahakama, hasa kuanzia Mahakama za Mwanzo aidha takribani asilimia 70 ya mashauri yanayosajiliwa mahakamani yanatoka Mahakama za Mwanzo. Hivyo mwelekeo wa Mahakama ni kuhakikisha miundombinu ya Mahakama hizo inaimarika ili kupunguza mashauri katika Mahakama za juu. 


Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete akifafanua jambo alipofika kumsalimu Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (hayupo pichani) akiwa kwenye ziara ya kukagua na kujifunza mambo mbalimbali ya maboresho yanatekelezwa na Mahakama ya Tanzania leo tarehe 20 Mei, 2024 jijini Dar es salaam.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa neno la utangulizi mbele ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma wakati Mkurugenzi huyo alipowasili Ofisini hapo.

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete akisalimiana na Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alipowasili Ofisini kwake kumsalimu.


Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete (wa tatu kushoto) pamoja Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania na wa Benki ya Dunia.


Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete akiteta jambo Ofisini kwa Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kulia) akimkaribisha na kusalimiana na Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete aliwasili Mahakama ya Rufani Jijini Dar es salaam.

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete akiteta jambo alipokuwa akikagua shughuli mbalimbali zinazoendelea ndani ya Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki cha Masuala ya Familia Temeke jijini Dar es salaam.

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete (wa kwanza kulia) akieleza jambo wakati wa kikao kifupi cha majumuisho ya ziara yake ya ukaguzi, katikati ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akimsikiliza na kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Angelo Rumisha 


Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete (wa kwanza kulia) akimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel  wakati wa kikao kifupi cha majumuisho ya ziara yake ya ukaguzi wa shughuli mbalimbali za maboresho ya Mahakama, kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania Mhe. Dkt. Angelo Rumisha.

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete (wa pili kushoto) akiwa kwenye picha ya pamoja na Viongozi waandamiazi wa Mahakama ya Tanzania na Benki hiyo.

Mkurugenzi Mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania, Malawi, Zambia na Zimbabwe Bw. Nathan Belete (wa pili kulia) akimsikiliza Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel  wakati anakagua Mahakama Inayotembea.








                                             (Picha na Innocent Kansha-Mahakama).

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni