Alhamisi, 16 Mei 2024

EPUKENI KASORO KATIKA MNYORORO WA KESI DHIDI YA UJANGILI-JAJI MTULYA

Na Mwandishi wetu.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya amewahimiza wadau wa haki wanaoshiriki mafunzo ya namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu kuzingatia vema sheria, kanuni na taratibu ili kuondoa changamoto zinazojitokeza katika hatua mbalimbali za uendeshaji wa mashauri hayo.

Mhe. Jaji Mtulya ametoa kauli hiyo tarehe 13/05/2024 wakati akifungua mafunzo hayo ya awamu ya tano ya wadau wa haki jinai zaidi ya 179 katika ukumbi wa Blue Sky Hotel mjini Tarime mkoani Mara ambayo yanaendeshwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) kwa ufadhili wa Taasisi isiyo ya Kiserikali ya PAMS Foundation inayojihusisha na uhifadhi wa mazingira na usalama wa Wanyamapori.

Mafunzo hayo yatakayodumu kwa wiki moja hadi tarehe 17/05/2024 yanawajumuisha washiriki ambao ni Majaji wa Mahakama Kuu, Mahakimu, Waendesha Mashtaka   na Wapelelezi wa ngazi mbalimbali kutoka mikoa ya Mwanza, Kagera, Shinyanga, Simiyu na Mara.

Katika hotuba yake, Mhe. Jaji Mtulya amesema: “Mashauri haya ya wanyamapori yana sheria zake, kuna taratibu nyingi kuanzia mtu anapokamatwa mpaka mtu kuhukumiwa, ila taratibu hizo mara nyingi huwa zinakosewa na wadau, hivyo tunakutana hapa ili kupeana ufahamu wa pamoja katika kutatua changamoto hizo ili tuweze kulinda rasilimali  hizo na kulinda uchumi wa nchi.”

Nae Mkurugenzi wa mafunzo ya Kimahakama kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Dkt. Patricia Kisinda amesema kuwa mafunzo hayo yameandaliwa baada ya utafiti uliyofanywa na IJA kubaini uwepo wa kasoro katika kuendesha mashauri hayo ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu.

Kuhusu matarajio baada ya mafunzo hayo, Mhe. Dkt Kisinda amebainisha: “Matarajio yetu ni kwamba washiriki hawa watakaporudi katika vituo vyao vya kazi ni kuweza kuyaweka katika vitendo yale waliyofundishwa darasani, kwa sababu katika mafunzo haya wanafundishwa kwa vitendo ikiwemo kupelekwa mbugani kuona kwa vitendo yale waliyofundishwa darasani ambayo yanahusiana na rasilimali hizo za wanyamapori na misitu.”

Kwa upande wake Mkurugenzi wa Mafunzo na Operesheni wa PAMS Foundation, Bw. Samson Kassala amewaambia washiriki hao kuwa wana jukumu kubwa katika mapambano dhidi ya majangili na kulinda rasilimali hizo muhimu kwa taifa.

“Ni muhimu mkatambua kuwa mna jukumu zito katika mapambano ya kitaifa dhidi ya majangili. Kujitoa kwenu na ustahimilivu wenu ndio msingi wa matumaini ya Tanzania katika kulinda mali hizo,” amesema Bw. Kassala.

Nae mmoja wa washiriki wa mafunzo hayo akiwemo Afisa muhifadhi kutoka Mamlaka ya usimamizi wa wanyamapori Tanzania (TAWA), Gift Sanga amesema kuwa mafunzo hayo yatawasaidia ufahamu wa kutatua changamoto zinazojitokeza katika hatua mbalimbali hususani za ukamataji na uchukuaji wa vielelezo vya ushahidi.

“Kumekuwepo na changamoto katika hatua za mwanzo za ukamataji, kwani kuna baadhi ya ukamataji unakuwa haujafuata sheria pamoja na uchukuaji wa kielelezo pamoja na kukihifadhi. Hivyo kukosewa kwa hatua hizo kunasababisha changamoto katika kuendesha mashauri,” amesema Bw. Sanga.

Mafunzo hayo ni sehemu ya utekelezaji wa makubaliano kati ya IJA na PAMS Foundation na yameshafanyika katika mikoa zaidi ya 20 huku washiriki 785 wakinufaika na mafunzo hayo ambayo yanafanyika kwa awamu ya mwisho hapa Tarime.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya akihutubia wakati wa ufunguzi wa mafunzo yahusuyo namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu wilayani Tarime mkoani Mara  tarehe 13/05/2024.

                          

Mkurugenzi wa mafunzo ya Kimahakama kutoka Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA), Mhe. Dkt. Patricia Kisinda akitoa neno la utangulizi wakati wa ufunguzi wa mafunzo yahusuyo namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu wilayani Tarime mkoani Mara.

Baadhi ya Washiriki wa mafunzo yahusuyo namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu wakimsikiliza mgeni rasmi ambaye ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya(hayupo pichani) wakati wa ufunguzi wa mafunzo yahusuyo namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu wilayani Tarime mkoani Mara.

Mkurugenzi wa Mafunzo na Operesheni wa PAMS Foundation Bw. Samson Kassala akihojiwa na vyombo vya habari wakati wa ufunguzi wa mafunzo yahusuyo namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu wilayani Tarime mkoani Mara.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo yahusuyo namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu wilayani Tarime mkoani Mara.

Meza kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Mtulya (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo yahusuyo namna bora ya uendeshaji wa mashauri ya uhalifu dhidi ya wanyamapori na makosa ya misitu wilayani Tarime mkoani Mara.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni