Ijumaa, 24 Mei 2024

HISTORIA YAANDIKWA UPYA UJENZI WA KITUO JUMUISHI PEMBA

Na. Innocent Kansha – Mahakama, Pemba

Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla amesema mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Pemba unaenda kuandika histori mpya ya ushirikiano baina ya Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Zanzibar.

Akizungumza katika hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo hicho iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba jana tarehe 23 Mei, 2024, Mhe. Abdalla alisema kuwa kwa mara ya kwanza Mahakama ya Zanzibar imepata msaada mkubwa wa ujenzi wa kituo jumuishi Zanzibar.

Jaji Mkuu huyo aliihakikishia Mahakama ya Tanzania kuwa Mahakama ya Zanzibar kupitia Pemba ipo tayari kutoa ushirikiano wa hali ya juu kwa kipindi chote cha ujenzi wa kituo hicho hadi kukamilika kwake na kuanza kutumika. Akamtaka mkandarasi wakati wa ujenzi akikutana na changamoto zozote aujulishe uongozi wa Mahakama Zanzibar ili kwa pamoja wazitatue haraka na ujenzi ukamilike kwa wakati uliokusudiwa.

Aidha, Mhe. Abdalla alitoa rai kwa Mkandarasi wa ujenzi wa kituo hicho kusimamia ujenzi huo kwa makini kama mkataba unavyoelekeza na kwamba Mahakama haitarajii kusikia masuala ya wizi au udokozi wa vifaa vya ujenzi wa jengo hilo.

“Nitoe ahadi kwamba majengo haya tunayoyajenga sio tu kwa kujengwa na kukamilika pia tunakusudia kuboresha utendaji kazi wetu wa utoaji haki kwa wananchi kupitia majengo manne ya kisasa yanayendelea kujengwa katika maeneo mbalimbali Zanzibar, ikiwemo kituo hiki cha Pemba,” aliongeza Jaji Mkuu.

Mahakama ya Zanzibar inaendela na mchakato wa kujenga mifumo ya kisasa ya TEHAMA kwa ajili ya kusikilizia mashauri mahakamani itakayo simikwa katika majengo yote ya kisasa yanayojengwa Zanzibar ikiwemo kituo hicho.

Mhe. Abdalla alisema Mahakama ya Tanzania na Mahakama ya Zanzibar wapo kwenye mazungumzo ya kufufua utaratibu wa Majiji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Majiji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar kuwa wanapangiwa kusikiliza mashauri katika pende zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

 Jaji Mkuu wa Zanzibar alimshukuru Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwa kuendelea kutoa ushirikiano wa hali ya juu katika kudumisha na kuimarisha shughuli za utoaji haki baina ya pande zote mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mhe. Abdalla pia alimshukuru Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Mwinyi kwa kubariki mchakato mzima na kuridhia ujenzi wa Kituo hicho kujengwa kisiwani Pemba na kwa kuunga mkono Mahakama ya Zanzibar kwa kiwango kikubwa sana.

Naye, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel alisema Mahakama imetimiza ndoto iliyokuwa nayo muda mrefu ya kuanza safari ya ujenzi wa jengo la kituo jumuishi kisiwani Pemba na ujenzi huo umesabishwa na matokeo ya mahusiano mazuri ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Taasisi za kimataifa za kifedha. Alisema kuwa rasilimali fedha inayotumika kujenga kituo hicho inatokana na mkopo wa gharama nafuu kutoka Benki ya Dunia uliochukuliwa na Serikali ya Tanzania.

“Lengo la kujenga jengo hili lina mambo makubwa matatu, ikiwemo kutoa pia fursa kwa wenzetu wa Pemba wawaze kupata huduma hii ya kituo jumuishi kwa kuzingatia kwamba ngazi zote za kimahakama zinapatikana katika mwanvuli mmoja kwa maana ya Mahakama ya Mwanzo, Wilaya, Mahakama ya Hakimu Mkazi, Mahakama Kuu na Vikao vya Mahakama ya Rufani,” alisema Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabrel aliongeza sababu nyingine ya kujenga kituo hicho Pemba ni kushajihisha matumizi ya rasilimali katika muktadha wa Muungano ambao hadi sasa umetimiza miaka 60. "Kwa kuwa mkopo huo ni kwa ajili ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na hakuna Jamuhuri ya Muungano bila Zanzibar na kwa kuwa hata kodi za mrejesho wa mkopo unafanyika na kodi za watanzania, Mahakama ikaona ni jambo jema kuweka alama hiyo ya kumbukumbu ya kuhakikisha kwamba suala la Muungano linazidi kuendelea...

“Jambo la tatu ni kuhakikisha kwamba maboresho haya yanayotokea ya Mahakama kwa upande wa Bara kuwa ni vema pia yakaletwa upande wa pili wa Muungano. Kuwa na jengo kama hili la kituo jumuishi ni kichocheo kikubwa cha kuweza kuleta miundombinu ya mifumo ya TEHAMA kama vile Tafsiri na Unukuzi (TTS) na matumizi mengine ya ki-TEHAMA katika uendeshaji wa mashauri,” aliongeza Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabriel alisema mchakato wa ujenzi huo umewezekana kutokana na kuwa na timu nzuri na imara ya maboresho ya Mahakama ya Tanzania upande wa Bara inajulikana kama Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ‘Judiciary Delivery Unit’ (JDU) inayosimamiwa na Mkuu ya Kitengo cha Maboresho Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Dkt. Angelo Rumisha.

“Niishukuru Banki ya Dunia kwa kutuamini na kuendelea kutupa mikopo kama hii ili tueweze kuboresha miundombinu kwa hali ya juu. Pia nimpongeze Mkandarasi wetu kwa kupata nafasi hii ya ujenzi wa jengo hili kwani kinyanganyiro kilikuwa ni kikali na kigumu lakini alikidhi vigezo vyote vya kimataifa ambayo tulikuwa tunaviitaji,” alibainisha Mtendaji Mkuu

Prof. Ole Gabriel alitoa rai kwa Mkandarasi huyo wa M/s Deep Construction Limited kwa kumsisitiza kwamba mradi huo ni wa kipekee na wa kimkakati na akamtaka asifanye kosa la kushindwa kukidhi kigezo cha ukomo wa muda uliopangwa kukamilika kwa mradi huo ambao ni tarehe 23 Februari 2025.

“Niwaombe wakaazi wa Pemba watambue kwamba hii ni heshima ya pekee ambayo Mhe. Rais Dkt. Hussein Ally Mwinyi amewapa na kuonyesha kuwajali kwa kiasi kikubwa, kwani yeye ndiye aliyeamua kwamba jengo lijengwe Zanzibar lakini lijengwe Pemba,” aliongeza Mtendaji Mkuu.   

Kwa upande wake, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Zanzibar, Bw. Kai Mbaruk alisema, hafla ya utiaji saini ya ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki na kukabidhi eneo la ujenzi ni ishara ya kuandika historia mpya na kubwa kwa wananchi wa Tanzania.

“Mkataba huu uliosainiwa baina ya Mahakama ya Tanzania na Mkandarasi wa ujenzi wa kituo jumuishi hichi ni ishara tosha ya ushirikiano na utengamano wa wa taasisi hizi mbili za Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,” alisema Mtendaji Mbaruk.

Bw. Mbaruk akiongeza kuwa jambo kubwa litakalo fanyika kupitia ujenzi wa kituo hicho kitajumuisha Mahakama za ngazi mbalimbali lakini pia kitakuwa kinatoa fursa kwa ajili ya Mahakama ya Rufani ya Tanzania kwani Mahakama hiyo ya juu kabisa imekuwa ikifanya kazi zake katika kanda mbalimbali nchini Tanzania na kwa upande wa Zanzibar imekuwa ikifanya vikao vyeke pale kisiwa cha Unguja pekee. Wananchi wa Pemba wanalazimika kusafiri hadi Unguja kwa ajili ya kufuatilia mashauri yao.

“Sasa ujio wa mradi huu wa ujenzi wa kituo jumuishi cha utoaji haki unakwenda kuwapunguzi shida kwa kiasi kikubwa wananchi wa Pemba lakini pia utaoa nafasi kwa maana ya mazingira bora ya kufanyai kazi kwa Waheshimiwa Majaji, Mahakamu na watendaji wengine wa Mahakama Pemba,” alisema Mtendaji Mkuu huyo.

Bw. Mbaruk alisema jengo la kituo hicho likikamilika litatumia mifumo ya kisasa TEHAMA ya kuendeshea mashauri yote yatakayosajili mahakamani hii itasaidia kuharakisha usikilizaji wa mashauri lakini vilevile kuongeza uwazi katika uendeshaji wa mashauri hayo na kumrahisishia mwananchi ambaye atafika mahakamani kutafuta huduma ya haki.

“Sisi kama Zanzibar tunatoa shukrani nyingi kwa Mahakama ya Tanzania kwa kutuletea mradi huu na Viongozi wakuu wa nchi ambao mara zote wamekuwa wakisisitiza mashirikiano baina yetu na sasa juhudi hizo zimeonekana na kuzaa matunda,” alisisita Bw. Mbaruk

Akitoa maelezo mafupi ya Mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba, Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania na Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Dkt. Angelo Rumisha alisema Mahakama za pande zote mbili za Muungano na wananchi watashuhudia historia ikiandikwa tena kwa kusaini mkataba wa ujenzi wa kituo jumuishi cha utoaji haki Pemba

“Kupitia picha mjongeo zinazoonekana pale ukutani kwenye ‘Projector’ zinatoa tafsiri ya kwa nini leo sote tumekusanyika hapa ni historia inayoandikwa katika mstakabali mzima wa utoaji haki nchini,” alisema Jaji Dkt. Rumisha.

 Mhe. Dkt. Rumisha alisema kwa nini kinaitwa Kituo Jumuishi ni kwa sababu kimekusanya pamoja na kujumuisha Mahakama za ngazi zote kuanzia Mahakama ya chini mpaka Mahakama ya Rufani na wadau wote muhimu katika mnyororo wa utoaji haki ili kurahisisha upatikanaji wa haki na kwa kuwapunguzia gharama na kadha wananchi wanapotafuta haki.

Mhe. Dkt. Rumisha alisema kutokana na ripoti ya Tume ya haki jinai iliyowasilishwa kwa Rais wa Jamhuri ya Muungano Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan mnamo mwezi Januari 2023. Kwa upande wa Mahakama ya Tanzania baada ya kuichambua kwa kina ripoti ile Mahakama ilibainisha mambo 19 ya kufanyiwa kazi ili kuboresha utoaji haki nchini. Katika maoni hayo moja ilionekana kwamba wananchi wa Pemba walipohojiwa walisema wanapata kadha ya kusafiri ubali mrefu kufuata huduma za Mahakama ya Rufani.

Mhe. Dkt. Rumisha alibainisha kuwa wananchi walisema wangependa Mahakama ya Rufani iende Pemba na kwamba Mahakama ndiyo taasisi ya kwanza pekee kuanza mara moja kutekeleza mapendekezo ya ripoti hiyo ya Mhe. Rais.

“Kwa hiyo ujenzi wa kituo jumuishi Pemba kinakidhi na kutibu kiu ya wananchi wa Pemba waliosema wanataka kupata huduma za Mahakama ya Rufani. Lakini wakati kituo kinaendelea kujengwa Mahakama ikajiuliza kwa nini ijengwe Mahakama ya Rufani peke yake kwani hizo rufaa zinatoka wapi? Tukaona ni hekima kujenga Kituo Jumuishi kitakacho beba Mahakama zote ikiwemo ya Rufani kama wananchi wa Pemba walivyosema,” aliongeza Jaji Dkt. Rumisha.

Mhe. Dkt. Rumisha alisema Kituo Jumuishi hicho kitakuwa na ukubwa wa mita za mraba 3,782 na ghorofa nne pamoja na sakafu ya chini, ni pamoja na jengo kubwa, nyumba za walinzi, nyumba ya kangavuke ‘Generetor’, Mgahawa na Ofisi mbalimbali za wadau wa utoaji haki.

“Kituo Jumuishi cha Pemba kitakuwa cha pekee hapa Visiwani kwanza usanifu wake umezingatia kanuni za usanifu wa kisasa, pili kituo kitakuwa na Mahakama ngazi zote pamoja na kusogeza huduma karibu na wananchi pia kitapunguza gharama za upatikanaji wa haki na kuimarisha uwajibikaji kwa kutumia matumizi makubwa ya TEHAMA,” alisema Mhe. Dkt. Rumisha.

Mhe. Dkt. Rumisha alisema mradi huo utakamiliaka kwa kununuliwa samani pamoja na kuwekewa vifaa vya TEHAMA vya kisasa. Pia mradi huo unajengwa kwa unazingatia na kufuata taratibu zote za uasalama na mazingira ikiwa ni pamoja na kupata ridhaa kutoka Mamlaka ya Mazingira Zanzibar.

Mradi huo utakamiliki kwa gharama ya pesa za kitanzania Bilioni 9,882,759,789.96 gharama hiyo ni pamoja na ongezeko la thamani ‘VET’ pamoja na fedha za dharula. Hata hivyo Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeonesha nia ya dhati ya kusamehe kodi na tozo kwenye mradi huo. Iwapo hilo litakamilika huo mradi utakamilika kwa gharama ya Bilioni 7,976,400,153. 53

Kituo hicho kitajengwa ndani ya miezi tisa (9) bila nyongeza, muda wa ujenzi utaanza kuesabiwa kuanzia tarehe 23 Mei, 2024 Mkandarasi atakapokabidhiwa kiwanja na mnamo tarehe 23 Februari, 2025 Mkandarasi atakabidhi jengo.

Mradi huo unatekelezwa na Mkandarasi M/s Deep Construction Limited na utasimamiwa na Mkandarasi mshauri Arqes Africa ambaye atakuwa kiongozi wa washauri elekezi wa mradi.

Aidha, akitoa salamu fupi za Mahakama ya Tanzania, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya alitoa shukrani kwa wadau wote wa maendeleo wanaosaidia kuiwezesha Mahakama kufanya maendeleo ya maboresho ya ujenzi wa vituo jumuishi vinavyoendelea kujengwa ili kuboresha utoaji huduma za kimahakama kwani safari ya maboresho ya Mahakama ilianza 2016.

“Ujenzi wa Kituo Jumuishi hiki kinachojengwa hapa Pemba kitawasaidia wananchi kupunguza gharama za kufuata umbali mrefu huduma za kimahakama hasa ngazi ya Mahakama ya Rufani kwani sasa vikao vitafanyika hapa, kitu ambacho kitamsaidia mwananchi kutumia muda uliobakia kufanya shughuli nyingine za kimaendeleo za ujenzi wa Taifa letu,” alisema Mhe. Nkya.

 Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla akitoa hotuba wakati wa hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba  iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba jana tarehe 23 Mei, 2024.                                                                          

 Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akitia saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba, kulia ni Mkandarasi M/s Deep Construction Limited Bw. Rabinder Singh Jabbal hafla hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba.                                                                                                                               

Mkuu wa Kitengo cha Maboresho ya Mahakama ya Tanzania na Jaji wa Mahakama Kuu Mhe. Dkt. Angelo Rumisha Akitoa maelezo mafupi ya Mradi wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba.


Sehemu ya wageni mashauri waliohudhuria hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba 

Mkuu wa Kitengo cha usimamizi wa Majengo Mahakama ya Tanzania Mhandisi Moses Lwiva akimkabidhi michoro ya jengo la Kituo Jumuishi cha utoaji haki kitakacho jengwa kisiwani Pemba Mkandarasi wa M/s Deep Construction Limited Bw. Rabinder Singh Jabbal

Mkuu wa Kitengo cha usimamizi wa Majengo Mahakama ya Tanzania Mhandisi Moses Lwiva akifafanua jambo wakati wa kumkabidhi Mkandarasi eneo la ujenzi wa kituo hicho
Mkandarasi wa M/s Deep Construction Limited Bw. Rabinder Singh Jabbal akionyesha michoro ya jengo la kituo Jumuishi litakalo jengwa kisiwani Pemba.

 Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (aliyevalia reflector) akiwa ameshikilia michoro ya ujenzi wa Kituo Jumuishi kinachojengwa Pemba kama kama ishara ya kumkadhi Mkandarasi eneo la ujenzi huo.

Sehemu ya wageni mashauri waliohudhuria hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa neno wakati wa utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Zanzibar, Bw. Kai Mbaruk akitoa hotuba fupi katika hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba  iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba

Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akitoa salamu fupi za Mahakama ya Tanzania wakati wa hafla hiyo.

Mashahidi wakitia saini katika hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba kushoto ni Mwanasheria wa Mahakama ya Tanzania Mhe. Hassan Chuka

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (wa kwanza aliyesimama) akimuonyesha Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (wa kwanza kulia waliketi)  mara baada ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba, kulia waliosimama ni Mkandarasi M/s Deep Construction Limited Bw. Rabinder Singh Jabbal.                                                                                                                                

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akipongezana na Mkandarasi mara baada ya zoezi la uwekaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba, kulia ni Mkandarasi M/s Deep Construction Limited Bw. Rabinder Singh Jabbal hafla hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba.                    

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akibadilisha mikataba mara baada utiaji  saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba, kulia ni Mkandarasi M/s Deep Construction Limited Bw. Rabinder Singh Jabbal hafla hiyo iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba.  

                  

Meza Kuu walioketi ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba  iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba



Meza Kuu walioketi ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba  iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba.


Meza Kuu walioketi ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba  iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba.


Meza Kuu walioketi ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Zanzibar, Mhe. Khamis Ramadhan Abdalla (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na wadau mbalimbali wa Mahakama waliohudhuria hafla ya utiaji saini Mkataba wa ujenzi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki kisiwani Pemba  iliyofanyika kwenye ukumbi wa mikutano katika jengo la Mamlaka ya Mapato Chakechake Pemba.

(Picha na Innocent Kansha- Mahakama)


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni