Jumanne, 28 Mei 2024

LINDENI UTU, HAKI ZA MASHAHIDI WA MASHAURI YA UNYANYASAJI WA KINJINSIA; JAJI KILEKAMAJENGA

Na Stephen Kapiga-Mahakama, Mwanza.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga mewataka Maafisa Mahakama kulinda utu na haki za mashahidi wa mashauri ya unyanyasaji wa kinjinsia wanaposikiliza mashauri hayo bila kutonesha majeraha ya unyanyasaji wa kinjinsia.

Akifungua mafunzo ya namna bora ya kuepuka kutonesha majera ya kisaikolojia kwa waathirika wa ukatili wa kingono na kijinsia jana tarehe 27 mei, 2024 kwa Mahakimu 14 na Maafisa ustawi wa Jamii, yanayofanyika katika ukumbi wa mikutano wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza, Mhe. Dkt. Kilekamajenga aliwasihi Mahakimu hao wakiwa kama Maafisa wa Mahakama wana jukumu la kuhakikisha kuwa haki inatendeka bila kuathiri watu waliopata madhara yaliyotokana na unyanyasaji.

“Mnapotoa haki hakikisheni mnatimiza wajibu wenu, huku mkilinda utu na haki za watu wote wanaohusika katika mnyororo wa haki. Ni marajio ya Mahakama kwamba  mwisho wa mafunzo haya yatawajengea ujuzi na maarifa mtambuka katika kushughulikia mashauri hayo kwa uangalifu na uwelewa bila kusababisha mathara ya kisaikolojia kwa  wote ambao wamepatwa na madhara ya unyanyasaji wa kijinsia…

Kwa kuzingatia itifaki za kisheria pamoja na viwango vya maadili ambavyo ni muhimu katika fani yetu, mafunzo haya yatutujengea uelewa wa sheria na miongozo ambayo imeweka kwa ajili ya kumlinda shahidi ambaye ni muathirika kwa ujumla kwenye mashauri yanayohusu unyanyasaji wa kingono. Kupitia msingi huo tutakuwa tunaimarisha kanuni ya haki ambayo ndiyo msingi mkuu wa mfumo haya,” alisema Mhe. Dkt. Kilekamajenga.

Mafunzo hayo yaliyoratibiwa na Chuo cha Uongozi wa Mahakama Lushoto (IJA) pamoja na Irish Rule of Law International (IRLI) yanafanyika kwa muda wa siku tatu (3) yakiwa na lengo la kuwajengea Mahakimu uelewa wa kutonesha juu ya majeraha ya kisaikolojia na kuimarisha umuhimu wa kushughulikia mashauri hayo.

Lengo lingine la mafunzo hayo ni kuimarisha ujuzi wa kuchukua ushahidi unaokubalika na kuhakikisha kuwa itifaki za kisheria na viwango vya maadili vinafuatwa ili kulinda utu na uadilifu wa mashahidi na pia kuchangia kufikia maamuzi ya haki na sawa. Vilevile kuhakikisha kuwa mtuhumiwa anashughulikiwa kwa kuzingatia misingi ya haki.

Mafunzo hayo yanaendeshwa na wawezeshaji ambao ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma, pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tabora Mhe. Pamela Mazengo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akifungua mafunzo ya namna bora ya kuepuka kutonesha majera ya kisaikolojia kwa waathirika wa ukatili wa kingono na kijinsia jana tarehe 27 mei, 2024 kwa Mahakimu 14 na Maafisa ustawi wa Jamii, yanayofanyika katika ukumbi wa mikutano wa jengo la Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki Mwanza. Kushoto ni Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma na kulia ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya mwanza Mhe. crecensia kisongo.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya mwanza Mhe. crecensia kisongo (aliyesimama) akitoa neno wakati wa hafla ya kufungua mafunzo hayo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga (aliyesimama) akiteta jambo na washiriki wa mafunzo hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga (katikati walioketi) wakiwa kwenye picha ya pamoja na washiriki wa mafunzo hayo.

Mkufunzi wa Mafunzo hayo Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza Mhe. Wilbert Chuma akitoa darasa kwa washiriki wa mafunzo hayo (hawapo pichani).

Mkufunzi wa mafunzo hayo Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Tabora Mhe. Pamela Mazengo (aliyesimama) akitoa mada kwa washiriki hao.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha-Mahakama)

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni