Ijumaa, 10 Mei 2024

WANANCHI WA KATA YA KWAKOA WATOA ENEO LA UJENZI WA MAHAKAMA

Na Paul Pascal –Mahakama Moshi.

Wanachi wa Kata ya Kwakoa Wilaya Mwanga Mkoani Kilimanjaro wamekabidhi eneo lenye ukubwa wa hekari Nne (4) kwa Uongozi wa Mahakama ya Wilaya Mwanga kwa ajili ya kuwezesha kujenga Mahakama ya Mwanzo itakayo wahudumia katika Kata hiyo yenye jumla ya vijiji 12 na idadi ya watu ipatayo 17,016 kwa mujibu wa Sensa ya watu na makazi ya mwaka 2022.

Akizungumza wakati wa mabidhiano ya eneo hilo jana tarehe 9 Mei 2024 Diwani wa Kata ya Kwakoa Bw. Kiende Athuman Mvungi alisema Kata hiyo ni miongoni mwa Kata Tano zinazounda Tarafa ya Jipendea ila katika Kata zote hakuna Mahakama ya Mwanzo hali inayopelekea wananchi kusafiri umbali mrefu. Mfano kutoka kata ya Toloha hadi ilipo Mahakama ya Mwanzo Lembini ni zaidi ya kilometa 50.

“Tumetoa eneo hili kuonyesha uhitaji na kiu ya kupata huduma hii muhimu ya haki katika Kata yetu ya Kwakoa kwa kuwa eneo hili lipo katikati ya Tarafa yetu, hivyo wananchi wa Kata zote watapata huduma kwa urahisi tukiwa na Mahakama yetu ya Mwanzo hapa. Niwaombe viongozi wa Mahakama kuona utayari na kiu yetu ya kutaka huduma ya Mahakama,” alisema Diwani huyo

Aidha, Mhe. Mvungi alisema, wananchi katika Tarafa hiyo wapo tayari kuanza ujenzi wa Mahakama hiyo kwa kutumia utaratibu wa msaragambo kama ambavyo tunafanya katika miradi mingime ya maendeleo katika tarafa hii, akawaomba viongozi wa Mahakama waliofika kupokea eneo hilo kufikisha kilio hichi kwa uongozi wa Kanda na Taifa ili kuona namna bora ya kushirikiana nao ili ujenzi huu ufanyike mapema.

Naye, Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Mwanga Mhe. Mariam Mfanga aliwashukuru Viongozi wa Kata hiyo kwa utayari wao na jitihada zao za kuonyesha nia ya dhati ya kutaka kusogezewa huduma za kimahakama karibu na jamii ili kila mwenye haki apate haki yake kwa wakati.

“Hii ni ishara njema ya uungwaji mkono wa Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania kwa kupitia ya nguzo ya Pili ya Mpango huo ambao ulianza kutekelezwa toka mwaka 2020/21-2024/25. Nawaahidi dhamira hii mliyoionesha hapa haitofifia nitawasilisha katika mamlaka zetu zote na kushirikiana nanyi tuweze kufanikisha yote tuliyojadili na kuafikiana,” alisema Mhe. Mfanga

Kwa upande wake, Afisa Utumishi Mahakama ya Wilaya mwanga Bw. Amedeusi Tarimo ambaye alimuwakilisha Mtendaji wa Mahakama Kanda ya Moshi aliwashukuru na kuwapongeza wananchi hao kwa kuonyesha imani yao kwa Mhimili wa Mahakama.

“Niwashukuru viongozi na wananchi wote wa Kata hii hakika mmetutia moyo katika kazi yetu ya kuhakikisha tunawahudumia watanzania wote kupata haki zao kwa wakati eneo hili mlilolitoa tumelipokea na niwahakikishie kwa kasi tuliyonayo Mahakama ya Tanzania italiendeleza kwa wakati na kwa shughuli mlizokusudia,” alisema Bw. Tarimo.

Shughuli hiyo ya mabidhiano iliudhuriwa na Hakimu Mkazi Mfawidhi Wilaya Mwanga, Afisa Utumishi Mahkama ya Wilaya ya Mwanga, Mhe. Diwani Kata ya Kwakoa, Mwenyekiti wa Kijiji cha Kwakoa, Mtendaji Kata ya Kwakoa, Mwenyekiti wa Kitongoji cha Kwakoa, pamoja na wananchi wa Kata hiyo kwa pamoja walisaini Muhtasari na barua za makabidhiano ya eneo hilo ikiwa ni ishara ya kuimilikisha Mahakama ya Wilaya ya Mwanga kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama na nyumba za watumishi watakaohudumu katika Mahakama hiyo itakapokamilika.

Afisa Utumishi wa Mahakama ya Wilaya Mwanga Bw. Amedeus Tarimo akizungumza na wananchi wa Kata ya Kwakoa baada ya makabidhiano ya eneo kwa ajili ya ujenzi wa Mahakama ya Mwanzo Kwakoa.

Diwani wa Kata ya Kwakoa Mhe. Kiende Athumani akizungumza wakati wa mkutano wa makabidhiano ya eneo kwa ajili ya kuomba upatikanaji  huduma ya  Mahakama ya Mwanzo Kwakoa

Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya ya Mwanga Mhe. Mariam Mfanga (wa pili kutoka kulia) akisikiliza mazungumzo ya washiriki wa mkutano katika zoezi la makabidhiano ya eneo kwa ajili ya kuleta huduma za Mahakama ya Mwanzo Kwakoa 

Viongozi wa Mahakama ya Wilaya ya Mwanga pamoja na Viongozi wa Vijiji na Vitongoji vya Kata ya Kwakoa wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya mkutano huo. 

Viongozi wa Mahakama ya Wilaya ya Mwanga pamoja na Viongozi wa Vijiji na Vitongoji vya Kata ya Kwakoa wakiwa katika picha ya pamoja mara baada ya mkutano huo.

(Habari Hii Imehaririwa na Innocent Kansha - Mahakama) 



 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni