Na Innocent Kansha – Mahakama, Dodoma
Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesema maboresho makubwa yaliyotekelezwa na yanayoendelea kutekelezwa na Mahakama ya Tanzania ni sehemu ya Uongozi wa Rais Mstaafu wa Awamu ya Nne wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete kwani anafahamu Mahakama ilipotoka na inapokwenda katika kuhakikisha inatoa huduma bora ya haki kwa wananchi.
Akizungumza
wakati wa hotuba ya kufungua Wiki ya Sheria nchini inayoadhimishwa kitaifa
jijini Dodoma leo tarehe 25 Janiari, 2025 Mhe. Prof. Juma amesema, Mhe. Dkt.
Kikwete ana historia ndefu ya chimbuko la Programu ya Maboresho ya Mahakama na
ushawishi wake kwa Benki ya Dunia.
“Maboresho
ya Mahakama yanayoendelea unafahamu chimbuko lake. Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed
Chande Othman katika hotuba yake ya kukukaribisha kama mgeni Rasmi Siku ya Sheria
nchini ya tarehe 4 Februari, 2015 anatukumbusha historia hiyo,” amesema Mhe.
Prof. Juma.
Mhe.
Prof. Juma akimnukuu Jaji Mkuu Mstaafu Mohamed Chande Othman amesema, “Tunakushuru
sana pamoja na kuwa ulikuwa kwenye matibabu kwa kututambulisha kwa Viongozi wa
Juu wa Benki ya Dunia, Novemba, 2014. Tumeanza mazungumzo nao kwa kushirikiana
na Hazina. Kwa upande wetu napenda kukuhakikishia kuwa viwanja, michoro, mifano
(models) na maandalizi mengine yako tayari. Tegemeo letu liliobaki kwenye
miradi ya maendeleo ya Mahakama ni wewe, Mhe. Rais, tuwiye radhi kwa kukusumbua
tena.”
Aidha,
akifafanua Kauli Mbiu ya maadhimisho ya Siku ya Sheria nchini 2025 isemayo “Tanzania
2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki Katika Kufikia Malengo Makuu ya Dira
ya Taifa ya Maendeleo.” Jaji Mkuu Prof. Juma
amesema, Inalenga kuikumbusha Mahakama kujipanga ili itekele DIRA 2050. Vilevile,
Kauli mbiu inazihamasisha Taasisi za Haki Madai ili kujiweka katika utayari wa
kufanikisha malengo makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.
“Tunakumbushana
kuwa Mahakama, na pia Taasisi za Haki Madai, zina wajibu wa kuhakikisha kwamba,
mfumo wa sheria na utawala bora unaohitajika utaakisi Malengo ya Dira ya Taifa
ya Maendeleo 2050 yanafikiwa kikamilifu,” ameongeza Mhe. Prof. Juma.
Mhe.
Prof. Juma ameongeza kuwa, kila mwaka Mahakama huadhimisha Siku ya Sheria ikiwa
ni kuashiria mwanzo wa shughuli za Mahakama kwa mwaka husika baada ya
kumalizika kwa likizo ya Mahakama inayoanza tarehe 15 Desemba, 2024 na
kumalizika tarehe 31 Januari, 2025.
Siku
ya sheria nchini hutanguliwa na wiki ya sheria ambayo hutumika kutoa elimu ya
sheria kwa wananchi kwa lengo la kuwawezesha wananchi kuelewa masuala
mbalimbali ya kisheria na hivyo kupambanua stahiki zilizo ndani ya sheria na
kutafuta njia za kuzipata, amesema Jaji Mkuu.
Mhe.
Prof. Juma amesisitiza kwamba, kupitia utoaji wa elimu katika ya Wiki ya
Sheria, wananchi watapata fursa ya kufahamu Katiba, Sheria, Kanuni, na taratibu
zinazohusu haki na wajibu wao. Wananchi watapata pia nafasi ya kushuhudia
shughuli mbalimbali zinazofanywa na Mahakama na wadau wake ili kuboresha
mazingira ya utoaji haki.
“Hii
inasaidia zaidi wananchi watapata fursa ya kutoa mrejesho wa huduma wanazopokea
kupitia maoni yao. Maoni yatakayotolewa yatatumika kama mtaji wa kuboresha
utoaji haki nchini,” ametanabaisha Jaji Mkuu.
Wiki ya Sheria ya mwaka huu naanza leo, tarehe 25 Januari, 2025 na kuendelea hadi tarehe Mosi Februari, 2025. Siku ya Sheria na kilele cha wiki ya sheria kitakuwa tarehe 3 Februari, 2025 jijini Dodoma katika viwanja vya Chinangali Pack, na mgeni rasmi atakuwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan.
Jaji
Mkuu Mhe. Prof. Juma akachukua fursa hiyo, kutoa rai kwa wananchi na wadau wote
wa Sheria kutembelea sehemu zote zitakazoandaliwa kwa ajili maadhimisho ya Wiki
ya Sheria nchi nzima.

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni