Na INNOCENT KANSHA – Mahakama, Dodoma
Maadhimisho
ya Wiki ya Sheria nchini yamezidi kushika kasi wakati zoezi la kutoa elimu ya
sheria kwa wananchi katika viunga vya jiji la Dodoma likipata mwitikio mkubwa,
huku elimu iliyoonekana kuwavutia wanananchi wengi wa viunga hivyo ikiwa ni ya
Mirathi, Ndoa, Talaka, Madai, Utekelezaji wa hukumu, Utatuzi wa migogoro ya Ardhi,
Usalama wa Raia na Mali zake na Elimu ya Usalama Barabarani, dhahiri ikionesha kuwa
ni mwarobaini wa matatizo ya kisheria kwa wananchi.
Akizungumza
na wananchi kwa nyakati tofauti katika Soko la Maisha Plus (Bonanza) Chamwino
na Stendi ya mabasi ya Chamwino Makore jijini Dodoma leo tarehe 31 Januari,
2025 Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hawa Mguruta akitoa darasa
la Ndoa na Talaka amesema, kuna aina kuu tatu za ndoa mosi ndoa ya mke mmoja,
ndoa ya wake wengi na ndoa inayothaniwa kuwa ya wake wengi.
“Kuna
imani zimejengeka miongoni mwa jamii zetu zinazosema eti kwamba, ukikaa na
binti wa mtu kwa muda wa miezi sita tu, eti huyo anaaminika kuwa mke wako
halali kisheria si kweli. Ukweli ni kwamba, kisheria ili mke na mume watambulike
kama mke na mume kuna kitu kinaitwa dhana ya ndoa. Dhana hii kisheria
inasema ni lazima wawili hao waishi pamoja kwa muda wa zaidi ya miaka miwili
wakishudiwa na majirani na jamii inayowazunguka wakiishi paa moja, wakiishi
hivyo, kisheria watatambulika na itahesabika kama mke na mume ama ndoa halali
kwa jicho la kisheria,” amesisitiza Mhe. Mguruta.
Aidha,
Mhe. Mguruta amebainisha kwamba, kuna aina tatu ya ndoa ila kuna aina tatu ya
namna ndoa zinavyofungwa na kusherehekewa katika jamii, moja ni kwa njia ya
Kimila, kwa njia ya Kikristo na kwa njia ya Kiislamu. Aidha ndugu wananchi hizi
siyo aina za ndoa bali ninamna ndoa zinavyofungu kulingana na imani na tamaduni
za jamii husika.
Akitoa
elimu kuhusu ufunguaji wa mashauri ya ndoa mahakamani, Naibu Msajili hiyo
amesema, ili ufungue shauri la ndoa kuna vitu viwili vya muhimu unapaswa
kuzingatia cha kwanza lazima ndoa inayotakiwa kuivunja iwe na umri wa zaidi ya
miaka miwili. Hivyo mtu yeyote ambaye ndoa yake haijafikisha miaka miwili
hawezi kufungua shauri la ndoa mahakamani.
“Ispokuwa
kama kutakuwa na sababu za msingi za kupewa ruhusa na Mahakama kwa maana ya
kwamba ukitaka kufungua shauri la ndoa kabla ya kutimiza miaka miwili ni sharti
uende mahakamani na uiombe Mahakama ikupe ruhusa ya kufungua shauri hilo, na
sababu pekee ni kwamba, kuna mazingira fulani fulani magumu yasiyoweza kuvumilika
katika hali ya kawaida. Endapo Mahakama ikiridhika sababu za mleta maombi
itatoa ruhusa ya kufungua shauri hilo la ndoa,” ameongeza Mhe. Mguruta.
Jambo
la pili la msingi ili mtu aweze kufungua shauri la talaka ni lazima ndoa hiyo
iwe imesuluhishwa na Baraza la Usuhishi la Kata au Uongozi wa Kanisa au Baraza
la Kiislam Bakwata kulingana na imani ya mtu anayetaka kufungua shauri la
talaka kwa ajili ya usuluhishi. Na endapo vyombo hivyo vitashindwa kuwapatanisha
watatoa fomu namba tatu (3) ambayo muhusika ataitumia kwenda mahakamani
kufungua shauri la ndoa. “Sasa ukipata fomu namba tatu utaiambatanisha fomu
hiyo kwenda nayo mahakamani na utaomba kufungua shauri lako,” ameongeza Naibu
Msajili huyo.
Mhe.
Mguruta amesema, shauri hilo la ndoa unaweza kulifungua Mahakama ya Mwanzo,
Mahakama ya Wilaya, Mahakama ya Hakimu Mkazi ama Mahakama Kuu. Mahakama zote
hizo zina mamalaka zinazofanana.
“Endapo
unataka kufungua shauri hilo, ila hujui udai vitu gani, kwenye shauri la ndoa
unaweza kuomba nafuu zifuatazo kwanza kabisa unaweza kuomba talaka, kwamba ndoa
yako ivunjwe na upewe talaka kuonyesha usitisho wa ndoa yako, lakini pia
unaweza kuomba uangalizi wa watoto, kwa maana ya nani anastahili kuishi na
watoto kati ya wanadoa waliotalakiana. Lakini pia unaweza kuomba matunzo ya
watoto na upande uliotalakiwa ambao Mahakama itatoa matunzo hayo kwa kuzingatia
maslahi mapana ya watoto. Vilevile anaweza kuomba amri ya watoto wasisumbuliwe
na wenza uliyetalakiana,” amesisitiza Mhe. Mguruta.
Vilevile,
akifafanua hatua za rufaa kwenye mashauri ya ndoa ama talaka, Mhe. Naibu
Msajili amesema, ikiwa hujaridhika na amri ama hukumu iliyotolewa unapaswa
ufanye nini? Sheria inakuruhusu ukate rufaa. Kama shauri la talaka
lilisikilizwa Mahakama ya Mwanzo utakata rufaa kwenda Mahakama ya Wilaya na
kama lilikuwa linasikilizwa Mahakama ya Wilaya au Mahakama ya Hakimu Mkazi utakata
rufaa kwenda Mahakama ya Kuu na pia kama shauri lilisikilizwa na Mahakama Kuu
utakata rufaa kwenda Mahakama ya Rufani ya Tanzania.
“Na
rufaa hizi kutoka Mahakama yoyote niliyoitaja hapo juu inatakiwa maombi hayo ya
rufaa yaombwe ndani ya siku arobaini na tano (45) na mtu akizidisha siku hizi
bila kukata rufaa ni lazima kwanza kabla ya kukata rufaa yake apeleke kwanza
maombi ya nyongeza ya muda wa kukata rufaa akieleza sababu za kumsababisha kutokufanya
hivyo ndani ya muda uliotajwa kisheria,” amefafanua.
Kwa
upande wake, mdau wa Mahakama ya Tanzania kutoka Ofisi ya Taifa ya Mashtaka
nchini, Mwendesha Mashtaka Mwandamizi Bw. Hebel Kihaka akitoa elimu kwa
wananchi amesema, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka ilianzishwa kama Ofisi huru ya
umma kupitia Tangazo la Serikali namba 49 la Mwaka 2018 la tarehe 13
Februari,2018 la kuanzishwa kwa Mamlaka hiyo kwa ajili ya kutekeleza mamlaka ya
kikatiba aliyopewa Mkurugenzi wa Mashtaka ya kusimamia haki jinai kwa mujibu wa
Ibara ya 59B ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya mwaka 1977.
“Wajibu
wa Msingi ni kushirikiana na wadau ikiwepo Mahakama kuendesha kesi za jinai
bila woga, upendeleo au ubaguzi ili kuhakikisha haki, amani na usalama
vinatamalaki katika jamii,” amesema Mwendesha Mashtaka huyo.
Majukumu
ya Msingi ya Ofisi ya Taifa ya Mashtaka ni kusimamia uendeshaji wa mashauri ya
jinai kote nchini, kusimamia na kuratibu shughuli za upelelezi, uchnguzi wa
mashauri yote ya jinai, kutoa ushauri wa kisheria kwa mamlaka mbalimbali katika
masuala ya kijinai, kuendesha na kusimamia mashauri ya utaifishwaji wa mali
zinazohusianav na uhalifu.
Vilevile,
kuratibu mashauri yanayohusiana na uhamishwaji wa wahalifu kutoka ndani na nje
ya nchi katika masuala ya jinai.
Wakati zoezi la kutoa elimu ya sheria kwa wananchi katika viunga vya jiji la Dodoma likipata mwitikio mkubwa, mtaani kwetu kulikuwa na kazi, shwangwe na nderemo.
Wakati zoezi la kutoa elimu ya sheria kwa wananchi katika viunga vya jiji la Dodoma, Dogo Janja hakubaki nyuma akitokomea na machapisho ya mashauri ya watoto kusambaza upendo
Kaka Mkubwa umakini mkubwa akichuja elimu ya sheria kupitia kipeperushi maadhimisho wiki ya sheria mtaani jiini Dodoma.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni