- Mamia wajitokeza uzinduzi Maadhimisho Wiki ya Sheria
- Majaji wa Rufani, Mahakama Kuu watembea kilometa tano bila kuchoka
- Mkuu wa Wilaya atoa ujumbe mzito
Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Wakazi wa jiji la Dar es
Salaam leo tarehe 25 Januari, 2025 wamejitokeza kwa wingi katika uzinduzi wa Maadhimisho
ya Wiki ya Sheria yanayofanyika kimkoa katika Viwanja vya Mnazi Mmoja Wilaya ya
Ilala.
Uzinduzi huo umetanguliwa
na matembezi ya kilometa tano yaliyoanzia kwenye Viwanja vya Mahakama ya Hakimu
Mkazi Kisutu na kupita katika Barabara mbalimbali jijini Dar es Salaam na
kuishia kwenye Viwanja vya Mnazi Mmoja.
Katika matembezi hayo, Majaji
wa Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu, Naibu Wasajili, Mahakimu, Watendaji, Watumishi wa Mahakama
na Wananchi kutoka Taasisi mbalimbali waliungana na Mkuu wa Wilaya ya Temeke,
Mhe. Sixtus Mapunda kwenye matembezi hayo yaliyochukua zaidi ya masaa matatu.
Baada ya kushiriki kwenye
matembezi hayo, Wananchi walifanya mazoezi mepesi na baadaye kupata burudani kutoka
Kwaya ya Mahakama ya Tanzania, maarufu kama Ng’aring’ari kabla ya Mhe. Mapunda,
aliyemwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila, kuzindua
maadhimisho hayo kimkoa.
Akizungumza katika hafla
hiyo, Mkuu wa Wilaya ameipongeza Mahakama ya Tanzania kwa kusimamia sheria na
kutekeleza jukumu la utoaji haki kwa weledi na uadilifu mkubwa.
“Mnayoyafanya
yanaonekana, bahati nzuri mifumo hii ya utoaji haki, ukifanya vizuri hakuna
atakayekusifia, ukifanya vibaya ndiyo utasikia kelele. Nichukue fursa hii
kuwaambia, katika kipindi cha mwaka uliopita, hatujapata kelele zinazotokana na
utendaji wenu, zaidi ya kusifiwa na kuonewa huruma kwa jinsi umlivyo na mzigo
wa mafaili ya kuhudumia watu…
“Shughuli yenu inahitaji
umakini, uzalendo na moyo wa kujituma. Hatuna shaka yoyote katika Mihimili
mitatu ya Serikali, Mhimili wa Mahakama ni kimbilio la wote. Mahakama kwa kiasi
kikubwa inatenda haki. Kuna changamoto za hapa na pale, lakini ukizitizama
hazitokani na utendaji wa Mahakama, ila zinatokana na maandalizi ya vyombo
vingine kabla ya taarifa sahihi kufika mahakamani,” amesema.
Amewaomba watumishi wa
Mahakama kutumia Wiki ya Sheria kufanya tathmini ya shughuli walizofanya mwaka
jana wa 2024, kubeba changamoto zote zinazowakabili na kuchukua maoni
mbalimbali ya Wadau ili watakapoanza mwaka mpya wa kimahakama wawe na nguvu za
kutosha kulitumikia Taifa.
Akizungumza katika
uzinduzi huo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es
Salaam, Mhe. Salma Maghimbi ameeleza kuwa jumla ya mabanda 39, yakiwemo 12 ya Mahakama
na 27 ya Wadau yameandaliwa kwa ajili ya kuonesha shughuli mbalimbali za
kimahakama na Wadau kwa kipindi chote cha Wiki ya Sheria.
Amesema kuwa maadhimisho
ya Wiki ya Sheria mwaka 2025 yanahusisha kazi mbalimbali zinazotekelezwa na Mahakama
na Wadau, ikiwemo kufanya tathmini ya utendaji kazi na usimamizi wa mashauri kwa
mwaka 2024 na kushiriki katika utoaji elimu kwa Wananchi kuhusu shughuli zinazotolewa
na Mahakama na Wadau.
“Jumla ya Vyuo vya kati
viwili, Shule tano za Sekondari na Shule tano za Msingi zitapata fursa ya
kukutana na watoa elimu kutoka Mahakama na Wadau mbalimbali tunaoshirikiana nao.
Jumla ya Magereza manne yaliyopo Mkoa wa Dar es Salaam ya Ukonga, Keko, Segerea
na Wazo Hill na Mahabusu ya Watoto moja Upanga yatatembelewa kwa lengo la kutoa
elimu ya jumla ya haki za Wananchi na huduma za Mahakama,” amesema.
Amebainisha pia kuwa maeneo
ya mikusanyiko ya watu, ikiwemo Stendi ya Magufuri, Kituo cha Mwendokasi
Kivukoni na Soko la Mbagala yatatembelewa na kutumika kutoa elimu sambamba na
ugawaji wa vipeperushi.
Kadhalika, Mhe. Maghimbi
amewaeleza Wananchi kuwa elimu kwa njia ya Vyombo vya Habari pia itatumika na
tayari wamefanya matangazo yanayorushwa katika mitandao ya kijamii na katika
vipindi vya matangazo vya radio na televisheni.
Jaji Mfawidhi amesema pia
kuwa katika kipindi cha Wiki ya Sheria kutakuwa na maonesho kwenye mabanda mbalimbali
ya Mahakama na Wadau, onesho la picha mjongeo kuhusu hatua za ushughulikiaji
mashauri kwa mtandao, bonanza la michezo na uzinduzi wa Mahakama ya Mwanzo Wazo
Hill.
Amewaalika Wananchi
kufika kwa wingi katika Viwanja hivyo kuja kupata elimu na huduma nyingine na
kuwakaribisha kwenye maadhimisho ya Siku ya Sheria itakayofanyika katika
Viwanja vya Mahakama Kuu Dar es Salaam tarehe 3 Februari, 2025.
Maadhimisho ya Wiki na
Siku ya Sheria kwa mwaka 2025 yanabeba Kauli Mbiu inayosema, “Tanzania ya
2050:Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki Madai katika Kufikia Malengo Makuu ya
Dira ya Taifa ya Maendeleo.”
Bendi ya Jeshi la Polisi ikiongoza matembezi kuelekea uzinduzi wa Maadhimisho ya Wiki ya Sheria katika Mkoa wa Dar es Salaam. Picha chini ni umati mkubwa wa Wananchi waliojitokeza kwenye matembezi hayo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni