Jumatano, 29 Januari 2025

MAHAKAMA KUU KANDA YA MTWARA YAZINDUA WIKI YA SHERIA

Na HUBERT MAANGA-Mahakama, Mtwara

Maadhimisho ya Wiki ya Sheria katika Mkoa wa Mtwara yalizinduliwa tarehe 27 January 2025 katika Viwanja vya Mashujaa, Manispaa ya Mtwara, huku Mgeni Rasmi akiwa Mkuu wa Mkoa, Kanali Patrick Sawala.

Uzinduzi huo ulifanyika tarehe 27 Januari, 2025 badala ya tarehe 25 Januari, 2025 kufuatia kibali maalumu kilichotolewa na uongozi wa Mahakama.

Maadhimisho hayo yalianza kwa maandamano ya Wananchi na Wadau wa Mahakama kuanzia Viwanja vya Mahakama Kuu Mtwara hadi Viwanja vya Mashujaa ambapo shughuli ya uzinduzi ilifanyika.

Akizungumza kwenye uzinduzi huo, Mkuu wa Mkoa alisisitiza umuhimu wa sheria katika kukuza maendeleo ya jamii na kuhakikisha kuwa haki inatendeka kwa wote. Aliwahimiza Wananchi kuitumia fursa hiyo ya Wiki ya Sheria kujifunza zaidi kuhusu haki zao na wajibu wao.

Aidha, aliwasihi watumishi wa Mahakama kuwa mstari wa mbele kuhakikisha wanafanya kazi kwa uadilifu katika kutekeleza majukumu yao.

 Kwa upande wake, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim, kabla ya kumkaribisha mgeni rasmi, alizungumzia juu ya jukumu la Mahakama katika kulinda haki za Wananchi kulingana na kauli mbiu ya mwaka 2025.

Kauli Mbiu hiyo inasema, “Tanzania ya 2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki Madai katika Kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo.” Mhe. Ebrahim aliahidi kuwa Mahakama itaendelea kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha kila mtu anapata haki yake kwa wakati.

Baada ya hotuba fupi, mgeni rasmi pamoja na Viongozi wengine walitembelea mabanda ya maonyesho yaliyoandaliwa na Taasisi mbalimbali, ikiwemo Mahakama, Magereza, Ustawi wa Jamii, Tume ya Haki za Binadamu na Jeshi la Polisi ambapo kila mmoja alikuwa na jambo la kipekee la msaada wa kisheria kwa jamii.

Maadhimisho ya Wiki ya Sheria Mtwara yamekuwa na mafanikio makubwa katika kuwajengea uwezo Wananchi kuhusu masuala ya kisheria na kuimarisha uhusiano kati ya vyombo vya sheria na jamii.

Jaji Mfawidhi Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim akihutubia Wadau mbalimbali wa sheria na Wananchi katika maadhimisho ya uzinduzi wa Wiki ya Sheria, Viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara.

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Patrick Sawala akifungua maadhimisho hayo katika Viwanja vya Mashujaa mkoani Mtwara.

Mkuu wa Mkoa wa Mtwara, Kanali Patrick Sawala (katikati), Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Rose Ebrahim (wa pili kushoto), Jaji wa Mahakama Kuu, Mhe. Martha Mpaze (kushoto), wakiwa wameketi meza kuu pamoja na Katibu Tawala Mkoa Bahati Geuzye (wa pili kulia) na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara, Mhe. Abdallah Mwaipaya (kulia) katika maadhimisho hayo.

Sehemu ya Watumishi wa Mahakama na Wadau wakiwa katika Maadhimisho ya Wiki ya Sheria wakitembea kutoka Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara kuelekea Viwanja ya Mashujaa.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni