Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Mahakama ya Mwanzo Wazo
Hill, ambayo ujenzi wake umekamilika hivi karibuni, itazinduliwa tarehe 31
Januari, 2025 kama sehemu ya shamrashamra za Maadhimisho ya Wiki ya Sheria kwa
mwaka 2025 katika Mkoa wa Dar es Salaam.
Hayo yamebainishwa na
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma
Maghimbi katika hafla ya uzinduzi wa maadhimisho hayo yaliyofanyika kimkoa kwenye
Viwanja vya Mnazi Mmoja jana tarehe 25 Januari, 2025.
“Mahakama hii ambayo ilianza kufanya kazi
tarehe 6 Januari, 2025 ipo Mtaa wa Nyakasangwe, Kata ya Wazo Hill, Tarafa ya
Kawe, Wilaya ya Kinondoni. Imelenga kuhudumia wakazi zaidi ya 312,394 kutoka Kata
ya Wazo Hill, Mabwepande, Bunju na Mbezi ambazo zina Mitaa 19,” alisema.
Jaji Mfawidhi alitumia
fursa hiyo kuwatangazia Wananchi wote wanaoishi katika Kata tajwa kiutumia
Mahakama hiyo ili kupata huduma za kimahakama karibu na wanakoishi.
Alieleza kuwa kabla ya
kujengwa kwa Mahakama hiyo, Wananchi walilazimika kusafiri umbali mrefu kupata
huduma za kimahakama katika Mahakama ya Mwanzo Kawe iliyopo katika maeneo ya
Kawe.
Mhe. Maghimbi alibainisha
kuwa ujenzi wa Mahakama hiyo ni utekelezaji wa Dira ya Mahakama na Mpango
Mkakati unaotekelezwa kupitia maboresho ya miundombinu ya Mahakama.
Akizungumzia utakelezaji
wa Nguzo ya Pili ya Mpango Mkakati wa Mahakama unaolenga kusogeza huduma za
kimahakama karibu zaidi na Wananchi, Jaji Mfawidhi alieleza kuwa Mahakama Kanda
ya Dar es Salaam imewezeshwa kwa kufunguliwa na kuanza kazi kwa Mahakama ya
Wilaya ya Ubungo iliyopo eneo la Kwembe na Mahakama ya Mwanzo Kwembe.
“Kabla ya uwepo wa
Mahakama hizi, Wananchi walilazimika kufuata huduma za kimahakama katika
Mahakama ya Wilaya Kinondoni na Mahakama ya Mwanzo Kimara,” alisema.
Aidha, Mhe. Maghimbi
alieleza kuwa ujenzi unaendelea wa
majengo ya Mahakama mpya ya Wilaya ya Kibiti, Mahakama za Mwanzo Bunju, Msata,
Kimanzichana, Mbagala na Gezaulole.
Uzinduzi wa maadhimisho
hayo ulifanywa na Mkuu wa Wilaya ya Temeke, Mhe. Sixtus Mapunda kwa niaba ya Mkuu
wa Mkoa wa Dar es Salaam, Mhe. Albert Chalamila. Mhe. Mapunda pia alipata
nafasi ya kutembelea mabanda ambayo yameandaliwa na Mahakama na Wadau
mbalimbali ambao wamejitokeza kutoa elimu ya sheria bure kwa Wananchi.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni