Jumapili, 26 Januari 2025

UZINDUZI WA WIKI YA SHERIA IRINGA WAFANYIKA

Na. LUSAKO MWANG’ONDA-Mahakama, Iringa

Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, imefungua Maadhimisho ya Wiki ya Sheria kwa kuanza na matembezi yaliyoongozwa na Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Peter Serukamba, akiambatana na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dustan Ndunguru.

Matembezi hayo yalianzia katika Viwanja vya Mahakama Kuu Kanda ya Iringa kupita mitaa ya Manispaa ya Iringa na kuishia katika Viwanja vya Garden (Posta) vilivyopo katikati ya Manispaa ya Iringa ambapo watumishi na Wadau walipata fursa ya kusikiliza hotuba kutoka kwa Viongozi hao.

Akizungumza wakati wa ufunguzi huo, Mhe. Serukamba aliwahimiza Wananchi wa Mkoa wa Iringa kuitumia vyema fursa hiyo ya uwepo wa Wiki ya Sheria ambapo watumishi wa Mahakama pamoja na Wadau mbalimbali watakuwa wanatoa elimu ya sheria bure kwenye maeneo mbalimbali.

Baadhi ya maeneo hayo ni kwenye mashuleni, vyuoni, maeneo yenye mkusanyiko wa watu na kutumia vipindi vya redio mbalimbali.

Naye Jaji Mfawidhi alieleza kuwa Mahakama kwa mwaka 2025 imejikita katika kuitafakari haki na ndiyo maana Kauli Mbiu ya maadhimisho imekuwa na mwelekeo wa kutafakari haki madai katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ifikapo mwaka 2050.

Mhe. Ndunguru alisisitiza kuwa msingi wa maendeleo na ustawi wa jamii ni amani na hakuna amani pasipo haki.

Jaji Mfawidhi aliwashukuru Wadau wa Mahakama ambao wanashiriki katika utoaji wa elimu kwenye maadhimisho hayo na pia amewakaribisha Wananchi kushiriki Siku ya Sheria nchini ambayo itafanyika Februari 3, 2025 katika Viwanja vya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa.

Katika ufunguzi huo, Viongozi mbalimbali wa Mahakama na Serikali ya Mkoa wa Iringa walipata nafasi ya kutembelea mabanda yaliyoandaliwa na kujionea namna Mahakama na Wadau walivyojipanga vyema katika zoezi la utoaji elimu kwa wiki nzima.

Mkuu wa Mkoa wa Iringa, Mhe. Peter Serukamba akizungumza wakati wa ufunguzi wa Wiki ya Sheria.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Iringa, Mhe. Dustan Ndunguru akizungumza wakati wa uzinduzi huo.

Sehemu ya watumishi wa Mahakama waliojitokeza katika uzinduzi wa Wiki ya Sheria.

Sehemu ya wanafunzi wa shule ya Sekondari ya Lugalo waliojumuika katika hafla ya uzinduzi huo.


 Mavazi mbalimbali ya kimahakama kama yalivyowekwa kwenye banda ya Mahakama ikiwa ni sehemu ya maonyesho katika Wiki ya Sheria.
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam)

 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni