- Diwani awaita Wananchi kuitumia badala ya kwenda Kawe
- Jaji Mfawidhi asema jitihada za Mahakama kusogeza huduma karibu na Wananchi dhahiri
Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama,
Dar es Salaam
Jaji Mfawidhi wa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi leo tarehe 31
Januari, 2025 amezindua Mahakama ya Mwanzo Wazo Hill, hatua inayolenga kusogeza
huduma za utoaji haki karibu na Wananchi.
Akizungumza katika hafla
hiyo, Mhe. Maghimbi amewaambia Wananchi kuwa kuzinduliwa kwa Mahakama hiyo kumeongeza idadi ya
Mahakama za Mwanzo katika Mkoa wa Dar es Salaam kutoka 14 na kufikia 15.
”Hii ni historia kwa kuwa katika Wilaya ya Kinondoni yenye Tarafa mbili na
Kata 20 Mahakama za Mwanzo zimeongezeka kutoka Mahakama tatu hadi nne na
ni historia kwa kuwa katika Tarafa ya Kawe yenye Kata 10 zimeongezeka Mahakama
za Mwanzo kutoka moja hadi mbili,” amesema.
Jaji Mfawidhi ameeleza kuwa kujengwa kwa jengo hilo na kuanzishwa kwa huduma
za Mahakama ya Mwanzo Wazo Hill siyo kwa bahati mbaya, bali ni utekelezaji wa
programu ya maboresho unaofanywa na
Mahakama ya Tanzania.
Utekelezaji huo ni kupitia Mpango Mkakati wa Mahakama ulioanza Awamu ya Kwanza
Mwaka 2015/2016 hadi 2019/2020 na kwa sasa ukimalizia utekelezaji wa Awamu
ya Pili ya Mpango Mkakati huo kwa mwaka 2020/2021 hadi 2024/2025.
Amebainisha kuwa katika maboresho
hayo, yapo mambo mengi yalibainishwa na kuwekewa mikakati ya utekelezaji, ikiwemo
ujenzi wa majengo mapya na ukarabati wa majengo chakavu . Mhe. Maghimbi amesema
kuwa tafiti zilifanyika na matokeo
kuonesha kuwepo kwa majengo chakavu
mengi na maeneo mengi kutokuwa na majengo ya Mahakama.
”Kupitia tathmini hiyo, Mahakama iliandaa Mpango wa Miaka Mitano wa Maendeleo ya Miundombinu ambao umeainisha
malengo ya ujenzi na ukarabati. Mpango huo ndio dira ya ujenzi unaoendelea
katika maeneo mbalimbali ngazi ya Mahakama Kuu kila Mkoa, Mahakama za Hakimu
Mkazi kila Mkoa, Mahakama za Wilaya kila Wilaya na Mahakama za Mwanzo angalau
kila Kata...
”Kwa hiyo, jengo hili la Mahakama ya Mwanzo ni ushahidi wa kivitendo wa
jitihada za Mahakama ya Tanzania kwa kushirikiana na Serikali kusogeza huduma
za kimahakama karibu na Wananchi kama tulivyojiwekea katika Nguzo ya Pili ya
Mpango Mkakati; lakini pia jengo hili ni
matokeo ya uboreshaji wa mazingira ya kufanyia kazi kwa watumishi na
wadau,” amesema.
Jaji Mfawidhi ameupongeza Uongozi wa Mahakama ya Tanzania chini ya Jaji
Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na wale wanaomsaidia kwa
kukubali na kuridhia Kanda ya Dar es Salaam kupewa mradi huo ambao sasa ni
Mahakama kamili.
Kadhalika, ameishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania chini ya
Uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu
Hassani kwa kutoa fedha zote asilimia mia moja zilizowezesha kujengwa na
kukamilika kwa jengo hilo.
Mhe. Maghimbi ametumia fursa hiyo kuwajulisha Wananchi kwamba maboresho ya huduma za Mahakama hayajalenga tu
majengo bali pia kubadili mitazamo ya watumishi kutoka kutoa huduma za haki kwa
mtazamo wa zamani wa Mahakama inayotisha na sasa kutoa huduma za kimahakama
zinazomlenga Mwananchi.
Amesema kuwa programu ya maboresho ya Mahakama imeleta utamaduni mpya wa
utoaji huduma, wenye mitazamo ya utoaji haki kwa haraka, weledi, uwazi na
ufanisi na unaomjali mwananchi ili Mwananchi atumie muda wake mwingi kwenye
uzalishaji mali badala ya kupoteza muda katika kutatua migogoro mahakamani.
Awali, akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa mradi huo, Mtendaji wa
Mahakama ya Hakimu Mkazi Kivukoni, Bw. Beatus Benedictus alieleza kuwa jengo
lilianza kujengwa na Mkandarasi Works Construction Ltd Agosti, 2022
na kutarajiwa kukamilika Februari, 2023 kwa gharama ya zaidi ya millioni za
Kitanzania 600.
Alibainisha kuwa fedha za mradi huo zimetolewa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano
wa Tanzania na kwamba jengo limekamilika
mwaka 2024.
Kwaupande wake, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Mwanzo Wazo Hill, Mhe.
Niccodemus Maroa alisema walianza kutoa huduma za kimahakama tarehe 6 Januari,
2025 na tayari mashauri 65 ya jinai yamesajiliwa na 33 kati ya hayo
yameshatolewa uamuzi.
Alisema kuwa Mahakama hiyo inatarajiwa kuhudumia wakazi 392,587 wa kata nne
ya Bunju, Mbezi juu, Wazo Hill na Mabwepande ambao awali walikuwa wakipata
huduma katika Mahakama ya Mwanzo Kawe iliyopo umbali wa kilometa 20.
Mhe. Maroa alibainisha changamoto zinazowakabili kama yidadi ndogo ya
watumishi pamoja na umbali kutokana na barabara ya kufika mahakamani hapo kuwa
mbovu.
Akizungumza katika hafla hiyo, Diwani wa Kata ya Wazo Hill, Mhe. Leonard
Manyama aliwataka wananchi wa kata hiyo kutokwenda kufungua mashauri katika
Mahakama ya Mwanzo Kawe na badala yake watumie Mahakama hiyo.
"Wenyeviti wa mitaa na Kata nne nawaelekeza mkaitishe mikutano katika
mitaa yenu kuwaeleza Wananchi uwepo wa Mahakama hii waweze kuitumia,"
alisema.
Kuhusu changamoto ya umbali na ubovu wa barabara kufika katika jengo la Mahakama
hiyo, Diwani huyo alisema tayari imeshapitishwa bajeti ya ujenzi wa barabara
hiyo kutoka eneo la Tegeta Bwawani hadi Madare kwa kiwango cha rami.
Alibainisha kuwa kabla ya ujenzi huo, barabara hiyo itakarabatiwa kwa kiwango cha changalawe. Alisema pia kuwa wataanza mazungumzo ya kuweka ruti ya daladala kutoka Tegeta Kibaoni hadi Kata ya Nyakasangwe ili wananchi waweze kufika kirahisi na kupunguza gharama za kukodi bajaji na pikipiki.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni