Jumapili, 26 Januari 2025

MBEYA YAZINDUZI RASMI MAADHIMISHO YA WIKI YA SHERIA

Na Daniel Sichula – Mahakama, Mbeya

Watumishi wa Mahakama, Wananchi wa jiji la Mbeya na Viunga vyake, Taasisi za Serikali na zisizo za Serikali jana tarehe 25 Januari, 2025 wajitokeza kwa wingi katika uzinduzi wa maadhimisho ya Wiki ya Sheria yanayofanyika katika viwanja vya Kabwe stendi ya mabasi mkoani Mbeya.

Uzinduzi huo ulitangaliawa na matembezi ya kilometa nne yaliyoanzia kwenye Viwanja vya Mahakama Kuu Tanzania Kanda ya Mbeya na kupita katika barabara mbalimbali za mitaa ya jiji la Mbeya.

Akizungumza wakati wa uzinduzi wa maadhimisho hayo, Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga aliielezea kauli mbiu ya maadhimisho hayo kuwa ni, “Tanzania ya 2025: Nafasi ya taasisi zinazosimamia haki katika katika kufikia malengo makuu ya dira ya taifa ya maendeleo.”

“Maadhimisho haya ya wiki sheria yanabebwa na Mahakama ikiwa ndiyo chombo mama katika kusimamia sheria bila kuwasahau wadau ambao wanaisaidia Mahakama katika kutimiza wajibu wake kisheria,” alisema Jaji Mfawidhi.

Vilevile, Mhe. Tiganga alieleza kuwa, maadhimisho ya wiki ya sheria yanaenda sambamba na utoaji wa elimu wa kisheria kutoka kwa Maafisa Mahakama na Wadau mbalimbali wa sheria.

Maeneo mbalimbali yatatembelewa kutoa elimu ya masuala ya kisheria yakiwemo mashule, Vyuo Vikuu, Taasisi za umma na binafsi alikadhalika maeneo ya stendi ya mabasi ya Mbalizi na Uyole jijini Mbeya kutakuwa na watoa elimu mbalimbali waliobobea kwenye masuala ya kisheria na kutoa vipeperushi kwa wananchi kwa hiyo wananchi msisite kufika kupata elimu hiyo, alisisitiza Mhe. Tiganga.

Kwa upande wake, Mgeni rasmi wa uzinduzi wa maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Juma Homera akitoa hotuba yake ya ufunguzi aliipongeza Mahakama Kuu, Kanda ya Mbeya kwa kuendelea kutoa haki kwa wananchi na kuipongeza Mahakama Tanzania kwa hatua waliyochukua ya kuendesha shughuli za kimahakama kwa mtandao, ambayo inaenda sambamba na kauli mbiu ya taifa iliyozinduliwa mwaka 2024.

“Kauli mbiu ya mwaka huu inaikumbusha Mahakama na wadau wa kusimamia sheria kutenda haki kwa nafasi waliyonayo katika kufikia lengo la dira ya taifa 2050, suala la haki na madai ni mtambuka haihusu Mahakama tu bali hata Taasisi za Serikali na pia Taasisi binafsi na wadau wote,” alisema Mhe. Homera.

Naye, Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa akihitimisha kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu pamoja na  mgeni rasmi kwa kufika kwake katika siku ya uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya sheria na kumwongoza kupita katika mabanda mbalimbali ya Taasisi zilizojitokeza katika uzinduzi huo, wakiwemo TAWJA, Kitengo cha TEHAMA Mahakama Kuu, Mbeya, Kitengo cha Masjala, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS), Jeshi la Magereza, Jeshi la Polisi, Ofisi ya Mwendesha Mashtaka wa Serikali, Ofisi ya Mawakili wa Kujitengemea, NMB bank, Yas Tanzania, Vodacom, Madalali wa Mahakama na Wasambaza Nyaraka za Mahakama, Ofisi ya Taifa ya Mashtaka, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), Ofisi ya Wakili Mkuu wa Serikali na Mtandao wa Waleta Mabadiliko Chanya Ulipo (LeMaChu).

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga akifafanua jambo wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya sheria jijini Mbeya

Mgeni rasmi wa uzinduzi wa maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Juma Homera akitoa hotuba yake ya ufunguzi wa maadhimisho ya wiki ya sheria nchini jijini Mbeya.

Mgeni rasmi wa uzinduzi wa maadhimisho hayo Mkuu wa Mkoa wa Mbeya, Mhe. Juma Homera (wa pili kushoto) akikagua sehemu ya mabanda ya utoaji elimu kwa wananchi, na wa kwanza kushoto ni Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Joachim Tiganga 

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mbeya Mhe. Victoria Nongwa akitoa shukurani kwa washiriki wa maadhimisho hayo.

Matembezi ya kilometa nne yakiendelea kueleke viwanja vya kabwa jijini Mbeya

Viongozi wakipasha misuli kujiweka tayari kwa Matembezi ya kilometa nne yakiendelea kueleke viwanja vya kabwa jijini Mbeya.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Mbeya Mhe. Aziza Temu akifafanua jambo kuelekea uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya sheria.



Burudani nayo ilikuwa sehemu ya uzinduzi wa maadhimisho ya Wiki ya Sheria.




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni