Jumapili, 26 Januari 2025

SUMBAWANGA NAKO MAMBO NI MOTO WIKI YA SHERIA

Na Mayanga SomekeMahakama, Sumbawanga

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Abubakar A. Mrisha, ametoa rai kwa wananchi kutumia fursa ya wiki ya sheria nchini kujipatia elimu ya sheria itakayotolewa.

Wiki ya sheria imezinduliwa jana tarehe 25 Januari, 2025 kwa matembezi yaliyoongozwa na Mhe. Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Rukwa Mhe. Peter Lijualikali. Aidha, kilele cha maadhimisho hayo ya siku ya sheria nchini itafanyika tarehe 03 Februari, 2025.

Akifafanua Kauli Mbiu ya Maadhimisho hayo Jaji Mrisha alisema, kauli mbiu ya mwaka 2025 kwa ajili ya maadhimisho ya Wiki na Siku ya Sheria inasema, ‘Tanzania 2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki Madai katika Kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo’.

Kauli mbiu hii inabeba ujumbe mkubwa juu ya wajibu wa Mahakama na asasi mbalimbali zinazoshughulikia haki madai katika kuhakisha wanafikia malengo ya Dira ya mpango wa maendeleo ya Tanzania ya Mwaka 2050’’alisema Mhe. Mrisha.

Aidha, Mhe. Mrisha aliongeza kuwa, Haki madai ni mfumo ambao unahusika na usimamizi wa haki katika masuala ya madai. Lengo kuu la haki madai ni kuhakikisha utolewaji haki kwa mujibu wa Ibara ya 107 A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Katika wiki hii ya sheria, Mahakama pamoja na wadau wa sheria watahusika kutoa elimu kwa Wananchi juu ya shughuli za utoaji haki kwa Wananchi. Pia ni nafasi kwetu Mahakama kupata mrejesho wa kazi zetu kutokea kwa Wananchi kupitia maonesho ambayo yatadumu hapa kwa muda wa wiki nzima. Nawasihi wananchi kutumia fursa hii kujipatia elimu ya sheria itakayotolewa katika eneo hili,” alisema Kaimu Jaji Mfawidhi.

Naye, Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe.  Peter Lijualikali ameipongeza na kuishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa hatua mbalimbali inayochukua kuboresha huduma za utoaji haki nchini.

“Kwa dhati kabisa, tunapongeza jitihada zinazofanyika katika kuboresha miundombinu ya majengo ambayo inaziwezesha Mahakama katika Mkoa wetu kutoa haki katika mazingira bora kabisa,” alisema Kaimu Mkuu wa Mkoa huyo.

Vilevile, Mhe. Lijualikali aliipongeza Mahakama kwa hatua ya hivi karibuni iliyochukuliwa na serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Tume ya Utumishi wa Mahakama kwa kuajiri Mahakimu Wakazi wapya themanini na wanane (88) ambao naamini kuwa wataongeza nguvu katika eneo la utoaji haki nchini.

Mhe. Lijualikali aliongeza kuwa, anatambua ya kuwa katika kuadhimisha ya wiki na siku ya Sheria nchini kwa mwaka 2025 inaongozwa na kauli mbiu isemayo; ‘Tanzania 2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki Madai katika Kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo’.

Aidha, Kaimu wa Mkoa huyo aliongeza kwamba, Kauli Mbiu hiyo ndiyo itakuwa muongozo wa Mahakama na Taasisi nyingine zitakazoshiriki maadhimisho ya wiki ya sheria yatakayo endelea kwa wiki nzima na hatimaye siku ya kilele.

Kwa uzoefu nilionao, natambua ya kwamba, uzinduzi huu utaambatana na utoaji wa Elimu  ya sheria katika sehemu mbalimbali kama vile taasisi za elimu, vituo vya redio, stendi za mabasi, bajaji, bodaboda na dalala na katika utoaji wa elimu hiyo naamini ya kwamba wananchi wote wakubwa kwa wadogo, wanaume kwa wanawake watapata fursa ya kuelimishwa kinagaubaga juu ya kauli mbiu ya mwaka huu lakini pia, wataweza kuuliza na kujibiwa maswali na dukuduku walizokuwa nazo juu ya masuala ya kisheria,” alisisitiza Mhe Lijualikali.

Akielezea umuhimu wa Kauli Mbiu hiyo Mhe. Lijualikali alisema, kwa kutambua umuhimu wa wadau wa haki madai katika kutoa haki kwa wakati, nipongeze Uongozi wa Mahakama ya Tanzania kwa kutambua ya kuwa Serikali inajukumu moja tu la kuendelea kufanya kazi katika nyanja zote ili kuendelea kukuza Uchumi wa nchi.

Maadhimisho haya yanatoa fursa kwa wananchi kutambua nafasi ya taasisi zinazosimamia haki madai nchini katika kufikia malengo ya Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050. Pia, wananchi watatambua kuwa utoaji haki kwa wakati unawawezesha kutumia muda wake vizuri katika kujiletea maendeleo yao na taifa kwa ujumla,” aliongeza Kaimu Mkuu wa Mkoa huyo.

Wito wangu kwa wananchi ni kuwa tutumie vizuri Mahakama pamoja na wadau wengine wa haki madai katika kutatua migogoro mbalimbali ili haki iweze kutolewa kwa wakati na wananchi waweze kutumia muda mwingi katika uzalishaji mali ili kujiinua kimaisha.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Abubakar A. Mrisha akiwahutubia wananchi, watumishi na wadau mbalimbali walioshiriki maadhimisho ya wiki ya sheria mjini Sumbawanga jana tarehe 25 Februari, 2025

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe.  Peter Lijualikali akiwahutubia wananchi, watumishi na wadau mbalimbali walioshiriki maadhimisho ya wiki ya sheria mjini Sumbawanga jana tarehe 25 Februari, 2025

Kaimu Mkuu wa Mkoa wa Rukwa, Mhe.  Peter Lijualikali (wa pili kushoto) na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Sumbawanga, Mhe. Abubakar A. Mrisha (wa kwanza kushoto) wakipata maelezo kutoka banda la Polisi wanaoshiriki kutoa elimu.


Sehemu ya washiriki wa maadhimisho ya wiki ya sheria wakiwa kwenye matembezi.


Sehemu ya washiriki wa maadhimisho ya wiki ya sheria wakiwa kwenye matembezi




Hakuna maoni:

Chapisha Maoni