Alhamisi, 30 Januari 2025

RUSHWA NI ADUI WA HAKI USITOE WALA KUPOKEA NDUGU MWANANCHI

Na INNOCENT KANSHA – Mahakama, Dodoma.

Wananchi wataadhalishwa kuepuka kutoa rushwa ama kwa kushawishi au kushawishiwa wanapokuwa wakihitaji huduma katika ofisi za umma kwani kwa kufanya hivyo wanatenda kosa kisheria kwa mtoa rushwa na mpokea rushwa, ifahamike kuwa ni kosa la jinai linaloambana na adhabu ya kifungo au fani ama adhabu zote mbili kwa wakati mmoja.

Rai hiyo imetolewa leo tarehe 30 Januari, 2025 Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hawa Mguruta kwa nyakati tofauti wakati wa utoaji Elimu ya sheria kwa wananchi wa jijini Dodoma katika Viunga vya Makulu na Kikuyu kufuatia mwendelezo wa utoaji wa elimu ya sheria katika Maadhimisho ya wiki ya sheria inayoadhimishwa kote nchini.

“Vitendo vya rushwa ni adui namba moja wa haki kwani havitakiwi kufumbiwa macho na jamii ya watu wasitarabu, rushwa hupofusha macho na kusababisha mwenye haki asiipate haki hiyo anayoitafuta. Ni rai yangu, ndugu wananchi tunapoona viashiria vya rushwa mahali popote unapotafuta huduma vilipotiwe mara moja kwenye mamlaka husika ili hatua stahiki zichukuliwe dhidi ya watumishi wasiyokuwa waadilifu,” amesisitiza Mhe. Mguruta.

Aidha, Mhe. Mguruta amewambia wananchi hao kuwa, Mahakama ya Tanzania imeanzisha Kituo cha Huduma kwa Mteja, Kituo hicho kinafanya kazi masaa 24 kupokea malalamiko, pongezi, ushauri, maoni na hata taarifa zenye viashiria vya kudai na kupokea rushwa kwa watumishi wasiyo waadilifu kwa lengo la kuboresha huduma za utoaji haki kwa wananchi. Kituo kinatumia namba ya bure: 0800 750 247 ambayo mwananchi akiitumia atasikilizwa kwa weledi mkubwa na shida yake kutatuliwa kutokana na msingi wa huduma aliyopewa mahakamani.

“Kituo hicho cha huduma kwa mteja cha Mahakama ya Tanzania kinachotumia namba hiyo ya bure kimeanzishwa maalum kwa ajili ya kuongeza uwazi, ufanisi na uwajibikaji miongoni mwa watumishi wa Mahakama na kusaidia kuongeza ufanisi wa utoaji huduma kwa wananchi ni vema tukaitumia namba hiyo muda wote tunapoona viashiria vya kutopata huduma stahiki ili kutatua changamoto tunazokutana nazo wakati tunapata huduma za kimahakama,” ameongeza Naibu Msajili huyo.

Vilevile, Mhe. Mguruta amesema, hivi sasa Mahakama ya Tanzania imejiimarisha katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kupunguza mwingiliano na mawasiliano yasiyo ya lazima na ya moja kwa moja baina ya wateja wa Mahakama na watumishi. Kwani mteja anaweza kusajili shauri lake akiwa nyumbani, kusikiliza shauri lake akiwa nyumbani, kutoa ushahidi wake hata akiwa nje ya nchi, kupokea nakala ya hukumu kwa njia ya mtandao bila kufika mahakamani kwani nakala za hukumu zinatolewa bure pasipo na malipo yoyote na hata kufanya malipo ya ada zitozwazo na Mahakama kwa njia ya kimtandao bila kufika mahakamani.

“Matumizi ya TEHAMA yanapunguza mianya ya rushwa na kupunguza malalamiko kwa kiasi kikubwa, kuongeza uwazi, ufanisi na uwajibakaji katika kutoa huduma kwa wananchi wanaohudumiwa na Mahakama ya Tanzania. Ni vema ndugu wananchi tukajielisha namna ya kutumia TEHAMA kupata huduma za kimahakama kwa njia rahisi inayookoa muda, usumbufu usio wa lazima na kuokoa gharama ili mwananchi huyu awaze kupata muda wa kutosha kushushiliki shughuli za kiuchumi na uzalishaji mali ili kukuza pato lake na la Taifa,” ametanabaisha Mhe. Mguruta.

Kwa upande wake, Mdau wa Mahakama ya Tanzania kutoka Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), ambaye ni Msuluhishi Mwandamizi Bw. Thomas Malekela akitoa elimu kuhusu migogoro ya kazi amewambia wananchi kuwa, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ni Taasisi ya Serikali ambayo imewekwa mahususi kwa ajili ya utatuzi wa mashauri yanayotokana na ajira ama kesi zinazotokana na ajira.

“Wewe mwajiriwa ama ndugu yako ameajiriwa au wewe umeajiri, haki zako zinazotokana na uhusiano huo na zinasimamiwa na Tume ya Usuluhishi na Uamuzi. Watu wenye tafsiri ambayo pengine ni potofu tungeweza kusema wanafikiri kwamba sisi kazi yetu ni kutetea wafanyakazi la hasha. Sisi kazi yetu ni kusimamia haki kati ya Mwajiri na Mfanyakazi katika umoja wao au mtu mmoja mmoja,” amesema Bw. Malekela.

Bw. Malekela amesema, Tume ya Usuluhishi na Uamuzi inatatua migogoro kwa namna mbili, njia ya kwanza ni kusuluhisha na kurejesha mahusiano mahali pa kazi na njia ya pili ni kutoa hukumu kwa pande zilizoshindwa kabisa kurejesha mahusiano mahala pa kazi, kwa kutambua hilo ni Tume ni Taasisi maalum kwa ajili ya utatuzi wa migogoro inayotokana na ajira.

“Baadhi yetu tumekuwa tukienda kwa Viongozi wengine kama vile wa Mtaa, wa Kata, kwa Diwani, kwa Katibu Tarafa, kwa Katibu Tawala Wilaya hata kwa Mkuu wa Wilaya kueleza migogoro yetu na waajiri. Kule kwa kufanya hivyo wanakuwa wamepoteza muda wao kwa sababu siyo mamlaka sahihi kwa utatuzi wa migogoro ya kiajira,” amesisitiza Msuluhishi huyo.

Bw. Malekela amebainisha kwamba, Sheria imeweka utaratibu bayana kwamba, mwajiriwa akiwa na tatizo la aina Fulani mfano, kuachishwa kazi unatakiwa kufungua kesi kwenye Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ndani ya siku 30 bila kuchelewa ili asipoteze haki zako za kiajira.

“Sasa wewe ukiamua kwenda kwa Afisa Mtendaji unapoteza muda wako kwa sababu siyo mamlaka sahihi kwa kesi uliyonayo ama mgogoro ulionao vivyo hivyo ukienda kwa Katibu Trafa na kwa Mkuu wa Wilaya na hata wengine wasiyo kuwa na mamlaka ya sheria ya kitume,” amesisitiza Msuluhishi huyo.

Tume ya Usuluhishi na Uamuzi ni chombo cha kimahakama kwa sababu kinatoa hukumu, kinatoa tuzo (Decree) ambayo ina nguvu sawa na Mahakama ya Wilaya na Mahakama ya Mkoa, na kama mtu anakuwa hajaridhika na maamuzi yaliyotolewa na Tume anapaswa kukata rufaa kwenda Mahakama Kuu, Kitengo cha ajira ama Kazi kwa muda ulibainishwa kisheria, ameongeza Bw. Malekela.

Vilevile, Msuluhishi huyo amewasisitiza wananchi kwamba, migogoro ya ajira inautaratibu wake wa kushughulikiwa na siyo kila mtu anamamlaka ama uwezo wa kusuluhisha migogoro ya ajira. Bali Tume tu ndiyo inauwezo na mamlaka kisheria kushughulikia migogoro ya mahusiano kazini. 

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hawa Mguruta (mwnye tsherti nyeupe) akitoa Elimu ya sheria kwa wananchi wa jijini Dodoma katika Viunga vya Makulu na Kikuyu katika zoezi la utoaji elimu kwenye mkusanyiko wa wananchi leo tarehe 30 Januari, 2025 Viunga vya Makulu.


Mtaalum akitoa elimu ya Mirathi, Wasia, Ndao na masuala ya Talaka. Hakimu Mkazi Mhe. Sifa Jacob (mwenye Tisheti ya Mahakama).
 
Mdau wa Mahakama ya Tanzania kutoka Tume ya Usuluhishi na Uamuzi (CMA), ambaye ni Msuluhishi Mwandamizi Bw. Thomas Malekela akitoa elimu ya usuluhishi wa migogoro ya ajira.



Mtaalum akitoa elimu ya Mirathi, Wasia, Ndao na masuala ya Talaka. Hakimu Mkazi Mhe. Sifa Jacob (mwenye Tisheti ya Mahakama).
 





Mwakilishi kutoka Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Coplo Ester Makali akipangua hoja za wananchi wakati wa utoaji Elimu ya sheria kwa wananchi wa jijini Dodoma katika Viunga vya Makulu na Kikuyu.


Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hawa Mguruta (mwnye tsherti nyeupe) akimsikiliza mwananchi wakati wa kutoa Elimu ya sheria kwa wananchi wa jijini Dodoma katika Viunga vya Makulu na Kikuyu katika zoezi la utoaji elimu kwenye mkusanyiko wa wanananchi.

Naibu Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hawa Mguruta (mwnye tsherti nyeupe) akimsikiliza mwananchi wakati wa kutoa Elimu ya sheria kwa wananchi wa jijini Dodoma katika Viunga vya Makulu na Kikuyu katika zoezi la utoaji elimu kwenye mkusanyiko wa wanananchi.

Mwakilishi kutoka Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Coplo Ester Makali akipangua hoja za wananchi wakati wa utoaji Elimu ya sheria kwa wananchi wa jijini Dodoma katika Viunga vya Makulu na Kikuyu.

Mtaalum akitoa elimu ya Mirathi, Wasia, Ndao na masuala ya Talaka. Hakimu Mkazi Mhe. Sifa Jacob (mwenye Tisheti ya Mahakama).

Mwakilishi kutoka Jeshi la Polisi Kikosi cha Usalama Barabarani Coplo Ester Makali akipangua hoja za wananchi wakati wa utoaji Elimu ya sheria kwa wananchi wa jijini Dodoma katika Viunga vya Makulu na Kikuyu.








Mtaalum akitoa elimu ya kwenye Basi la abiria kuhusu Mirathi, Wasia, Ndao na masuala ya Talaka. Hakimu Mkazi Mhe. Sifa Jacob (mwenye Tisheti ya Mahakama).









     (Picha na Innocent Kansha- Mahakama, kutoka  Viunga vya Makulu na Kikuyu)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni