Watembelea pia Mahabusu ya Watoto Upanga
Na FAUSTINE
KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Watumishi wa Mahakama
Kanda ya Dar es Salaam leo tarehe 30 Januari, 2025 wametembelea Makazi ya Wazee
wenye Mahitaji Maalum Nunge, Wilaya ya Kigamboni na kutoa msaada wa vitu
mbalimbali kama sehemu ya Maadhimisho ya Wiki ya Sheria kwa mwaka 2025.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa
Mahakama ya Wilaya Ilala, Mhe. Heriet Mwailolo, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati
ya Huduma za Jamii, aliwaongoza watumishi hao kwenye tukio hilo la matendo ya
huruma.
Mhe. Mwailolo alishirikiana
na Katibu Tawala wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Sokoine, Bi. Lightness Kiula,
ambaye pia ni Katibu wa Kamati hiyo.
Watumishi hao waliwasili
katika Makazi hayo majira ya saa 4.30 asubuhi na kupokelewa na Afisa Ustawi wa
Jamii, Bi. Jacqueline Kanyamwenge, ambaye alionesha kufurahishwa na ujio wa wageni
wake hao.
Baadaye alieleza historia
fupi ya Makazi hayo na kuishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kuwafikiria,
kuwakumbuka na kuwajali Wazee hao kwa mahitaji mbalimbali muhimu.
“Hili mlilolifanya ni jambo
jema sana. Wazee wetu wanafurahi sana mnapowatembelea na kuwasaidia mahitaji muhimu
kama haya. Tutamfikishia Katibu Mkuu wa Wizara taarifa ya ujio wenu ili naye
apate kufahamu, asanteni sana,” amesema.
Naye Mwenyekiti wa Kamati
ameeleza kuwa Viongozi wa Mahakama wameona vema katika kipindi hiki cha Maadhimisho
ya Wiki ya Sheria kutuma wawakilishi kuja kuwaona kama Wadau na kuwasalimia.
“Viongozi wetu wameona
tusiishie kwenye zoezi la utoaji elimu pekee, bali pia tupate fursa ya
kuwatembelea Wadau wetu na kuonesha jinsi Mahakama inavyowathamini,” Mhe.
Mwailolo, amesema.
Awali, Katibu wa Kamati aliwasilisha
kwa Uongozi wa Makazi hayo orodha ya vitu mbalimbali walivyokuja navyo kwa
ajili ya kutoa kama msaada kwa wazee hao.
Sehemu ya vitu hivyo ni
kilo 100 za mchele, kilo 50 za sukari, kilo 100 za unga wa sembe, kanga za urafiki
doti sita, mafuta ya kupikia lita 20, fulana za ndani dazani tisa, mafuta ya
nazi dazani mbili, sabuni za unga mifuko mitano, juice boksi kubwa dazani 10 na
sabuni za kuogea dazani 14.
Watumishi hao wamewasilisha
pia mikeka mikubwa 15, maziwa ya unga dazani moja, sawa na kopo 24, nyanya sado
mbili, vitunguu maji kilo tano, karoti kilo tano, pilipili hoho kilo tano,
matikiti matatu, mananasi matatu pamoja na viungo vingine.
Wawakilishi wa Wazee hao,
Bw. Mussa Muna na Bw. George Joseph wameelezea kufurahishwa na kitendo
kilichofanywa na Mahakama kwa kuwakumbuka na kuja kuwatembelea.
Jana tarehe 29 Januari,
2025, watumishi hao, wakiongozwa na Mlezi wa Kamati hiyo, ambaye pia ni Jaji wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Hussein Mtembwa walitembelea Mahabusu ya Watoto
Upanga na kutoa zawadi za aina mbalimbali kwa wahitaji.
Miongoni mwa zawadi hizo
ni vyandarua 46, sukari kilo 25, mchele kilo 50, sabuni za kuogea, sabuni za
chooni, vikombe mfupa wa Samaki dazani nne na nyingine nyingi.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Wilaya Ilala, Mhe. Heriet Mwailolo, ambaye ni Mwenyekiti wa Kamati ya Huduma za Jamii, akizungumza kabla ya makabidhiano ya zawadi mbalimbali zilizotolewa na Watumishi wa Mahakama kwa Wazee hao.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni