Jumatano, 29 Januari 2025

UTOAJI ELIMU YA SHERIA MTAANI MAMBO NI MOTO

Na INNOCENT KANSHA – Mahakama, Dodoma.

Utoaji Elimu ya Sheria mtaani na maeneo mbalimbali yenye mikusanyiko wa wananchi imezidi kuwavutia wengi na kuacha gumzo kwa wananchi wakiwa wenye furaha na kusaidia kuongeza uelewa wa masuala mbalimbali ya kisheria ikiwa ni jitihada ya Mahakama ya Tanzania kujaribu kuwafikia wananchi wengi zaidi na kuwaelimisha.

Katika hatua hiyo Mahakama ya Tanzania na wadau wake wa utoaji haki leo tarehe 29 Januari, 2025 wametoa elimu hiyo katika maeneo ya Nane Nane standi ya Mabasi yaendayo mikoani na Kituo kilichofuata ilikuwa ni Soko la SabaSaba jijini Dodoma, shauku ya wananchi kutaka kujua taratibu za kisheria ilileta shangwe kwa wananchi, hamasa na maswali mengi kuulizwa kwa maafisa mbalimbali walioshiriki kutoa elimu hiyo.

Akizungumza na wananchi kwa nyakati tofauti katika maeneo hayo akitoa elimu ya Mirathi, Wasia, Ndao na masuala ya Talaka. Hakimu Mkazi Mhe. Sifa Jacob kwa ubobevu mkubwa amesema, mashauri ya mirathi yamekuwa yakishuhudiwa kuwa na changamoto kubwa katika jamii nyingi hapa nchini kutokana na uelewa mdogo wa wanajamii, kutawaliwa na ubinafsi na kutotambua taratibu za kutatua changamoto za masahuri hiyo.

Akifafanua taratibu za ufunguaji wa mashauri ya mirathi na uendeshaji wake mahakamani, Mhe. Sifa Jacob amesema, ili mtu afungue mirathi sharti azingatie mambo kadhaa ikiwemo kuwa na cheti cha kifo cha marehemu ili kuthibitisha kwamba, mali anayotaka kuisimamia mmiliki wa mali hizo zinazodaiwa ni zake amefariki.

Aidha, mfungua mirathi anatakiwa awe na muhutasari wa kikao cha ukoo uliokubaliana kwa pamoja uteuzi wa mpeleka maombi mahakamani ya kuomba kuteuliwa kwake kuwa msimamizi wa mirathi hiyo. Vilevile mtu hiyo atachukua nyaraka hizo ikiwa ni pamoja na wosia kama marehemu atakuwa ameacha wosia wa maandishi au wa mdomo utakao takiwa kuthibitisha mahakamani na mashahidi waliyoshudia maneno hayo ya wosia yakitamkwa na marehemu.

Mhe. Jacob akatanabaisha kuwa, jambo la msingi ni mwombaji kutambua kuwa ni Mahakama gani angepende kwenda kuomba ateuliwe kuwa msimamizi wa mirathi ya marehemu. Kwani, kwa kuzingatia mashauri hayo Mahakama za Mwanzo zote nchini zina mamlaka kisheria kusikiliza mashauri hayo, lakini pia Mahakama za Wilaya au Mahakama Kuu.

Mahakama ya Mwanzo ina mamlaka pale ambapo sheria inayotumika kusimamia mirathi hiyo ni sheria ya Kiislam au sheria ya kimila. Hivyo kama marehemu alikuwa inaonekana kuwa, mirathi yake itasimamiwa kwa sheria ya kiisilam ama ya kimila mpeleka maombi ya kuteuliwa kuwa msimamizi wa mirathi ya maehemu atakwenda Mahakama ya mwanzo. Lakini kama sivyo hivyo, basi mpeleka maombi ya kuteuliwa kuwa msimamizi wa mirathi ataenda Mahakama ya Wilaya au Mahakama Kuu akiwa na nyaraka husika za kumsaidia kufungua mirathi hiyo.

Mhe. Jacob ameongeza kuwa, jambo lingine la msingi ni utaratibu wa mpeleka maombi atakapo fika mahakamani. Mahakama itamuamuru atoe tangazo akiutaarifu umma kwamba, mpeleka maombi ya kuteuliwa kuwa msimamizi wa mirathi husika ameomba usimamizi wa mirathi ya marehemu bini Fulani, kama kutakuwa na mtu mwenye pigamizi juu ya mleta maombi basi pingamizi lake litasikilizwa na Mahakama na kulitolea uamuzi.

Lakini Mahakama ikilizika kwamba mleta maombi amekidhi vigezo vya kuteuliwa kuwa msimamizi wa mirathi basi Mahakama itamteua mleta maombi na kumpatia barua na nyaraka muhimu za kusimamia mirathi hiyo.

“Na kama msimamizi huyo aliomba hati ya kutekeleza wosia basi Mahakama itatoa hati ya kutekeleza wosia wa mali za marehemu ili kazi ya utekelezaji wa majukumu hayo uanze,” amesema Hakimu Mkazi huyo.

Mhe. Jacob ameongeza kuwa, baada ya kuteuliwa na Mahakama msimamizi wa mirathi ana kazi zipatazo tatu hadi nne, mosi Msimamizi wa mirathi ndiyo mwakilishi wa marehemu kwenye masuala yote ya kisheria na mali zake. Kwa hiyo ana wajibu wa kukusanya mali zote za marehemu kokote ziliko, anamamlaka ya kushitaki na pia mtu anayemdai marehemu anamamlaka ya kumshitaki msimamizi huyo wa mirathi.

Aidha, Msimamizi wa mirathi anawajibu wa kukusanya mali zote za marehemu na kulipa madeni yote yaliyothibitishwa aliyokuwa anadaiwa marehemu na kisha kugawa mali za marehemu kwenda kwa warithi halali waliothibitishwa na vikao vya ukoo kwa mujibu wa mali zilizoachwa na marehemu.

“Jambo moja la msingi la kuzingatia ndugu wananchi ni kwamba msimamizi wa mirathi siyo mmiliki wa mali za marehemu lakini pia msimamizi wa mirathi anateuliwa na Mahakama na mchakato wote wa usimamizi wa mirathi unafanyika mahakamani hayo ni mambo ya msingi ya kuzingatia na si vinginevyo,” ameongeza Mhe. Jacob.

Mhe. Jacob amesema, kuteuliwa kwa msimamizi siyo kwamba mchakato unakuwa umekamilika ni lazima msimamizi huyo akusanye mali alipe madeni na agawe mali hizo kwenda kwa warithi halali na mwisho awahamishie mali hizo kwenda kwanye majina ya warithi kwa maana ya majina yao mfano; kama marehemu ameacha nyumba inatakiwa umiliki uhame na isomeke ni nyumba ya mrithi Fulani ama kama ni gari itafanyika vivyo hiyo. Baada ya mchakato huo kukamilika Mahakama itafunga jarada hilo na haita pokea malalamiko mengine kuhusiana na mirathi hiyo.    

Kwa upande wake,  akitoa elimu kwa wananchi ya `Zimamoto na Uokoaji, Askari wa Jeshi la Zimamoto na Uokoaji Tanzania, Konstebo Jegu Dosela amesema, Jeshi hilo lina majukumu makuu mawili muhimu la kwanza ni kuzima moto pale unapotokea lakini jukumu la pili ni kufanya Uokoaji.

“Lakini ili mambo haya makuu mawili yafanyike kwa ukamilifu wake aidha, la kuzima moto uliotokea kuna vitu vinavyofanywa ili kuhakikisha moto huo hauleti madhara makubwa au hasara kubwa kwa wananchi. Kitu cha kwanza ni ukaguzi wa kinga na tahadhali dhidi ya majanga ya moto na ukaguzi huo unapokuwa umefanyika basi mwananchi atashauriwa kuweka vifaa ambavyo vitamsaidia mwananchi kukabiliana na tukio hilo endapo litatokea,” amesema Konstebo huyo.

Konstabo Dosela amesema, jukumu la tatu ni kutoa elimu ya majanga ya moto kwa wananchi matahalani kutoa namba ya kupiga wakati wa dharura ya Jeshi la zimamoto na uokoaji ambayo inapatikana muda wote pasipo changamoto na jeshi likipigiwa litafika eneo husika kwa ajili ya kazi ya uokoaji ama kutoa huduma hiyo.

“Changamoto inatokea mara nyingi mwananchi anapoona tukio la moto unatokea anaanza kuzima mwenyewe na anapoona moto unamzidia ndipo anakumbuka kupiga namba 114 ya Jeshi la zimamoto na uokoaji.  Mwananchi unashauriwa unapogundua kuna moto wakati jitihada za kuzima zikiendelea basi taarifa itolewe kwa wakati na Jeshi litafika kwa wakati. Vinginevyo itabaki kuwa lawama kama ambavyo zipo nyingi kwamba Jeshi linachelewa kila siku, lakini ukitoa taarifa kwa wakati Jeshi litafika kwa wakati,” amesisitiza Konstebo Dosela.

Majukumu ya uokoaji yamegawanyika katika maeneo mengi mfano, ajali barabrani, kuokoa watu waliozama kwenye maji, watu kudumbukia kwenye makalo ya vyoo mathalani watoto kutupwa huko Jeshi linahusika moja kwa moja. Hayo majumu yote yanatekelezwa na Jeshi la zimamoto na Uokoaji chini ya sheria ya sheria ya Jeshi la zimamoto na uokoaji ya mwaka 2007.

Afande Dosela akaelezea suala la usalama wa moto jikoni, hususani matumizi ya gesi inapokuwa inatumika kwa matumizi ya nishati ya kupikia wananchi wanashauriwa kuongeza umakini katika matumizi yake. Ili ikitokea mlipo wa gesi isiwadhuru watumiaji na kupoteza mali na maisha.

“Gesi inapokuwa imevuja ndani hakikisha mtungi unatoka nje ya nyumba na hakikisha unafungua madirisha na milango ili ile gesi iweze kuisha ndani ya nyumba na nyumba itakuwa salama, vinginevyo itakuwa kama mlipuko mkubwa ambao unaweza kukusababishia ulemavu ama kifo ni tahadhali za kuzingatia,” amesema Aande Dosela.

Hakimu Mkazi Mhe. Sifa Jacob (mwenye tisherti nyekundu) akitoa elimu ya Mirathi, Wasia, Ndao na masuala ya Talaka kwa wananchi.











Hakimu Mkazi Mhe. Sifa Jacob (mwenye tisherti nyekundu) akitoa elimu ya Mirathi, Wasia, Ndao na masuala ya Talaka kwa wananchi.

































Hakuna maoni:

Chapisha Maoni