Na Christopher Msagati- Mahakama, Manyara
Mkuu
wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Cuthbert Sendiga jana tarehe 25 Januari, 2025
amewaongoza Wananchi na Watumishi wa Mahakama Kanda ya Manyara kwenye hafla ya
ufunguzi wa Maadhinmisho ya Wiki ya Sheria kimkoa iliyotanguliwa na matembezi
maalum.
Akizungumza
wakati wa kufungua maadhimisho hayo yaliyofanyika Standi ya zamani ya mabasi
mjini Babati, Mhe. Sendiga aliwasisitiza wananchi wa Mkoa wa Manyara kutumia
vyombo rasmi vilivyowekwa kwa ajili ya utatuzi wa migogoro na utoaji wa haki na
siyo kutumia watu wanaojifanya kuwa wajuzi wa masuala ya kisheria ambao
wanapotosha na kuwaingiza wananchi katika matumizi makubwa ya fedha yasiyo ya
lazima.
“Mkoa
wa Manyara una watu wengi wanaojifanya kuwa wajuzi wa sheria na wengi wamekuwa
wakiwalaghai wananchi na kuwapotosha, ifike wakati wananchi wa Manyara
mbadilike na kutambua kuwa Mahakama ipo kwa ajili yenu hivyo itumieni bila woga na siyo kuwatumia watu wasiostahili,”
alisema Mhe. Sendiga.
Aidha,
Mhe. Sendiga alibainisha kuwa, Mahakama imekuwa ikitoa kauli mbiu mbalimbali
kila mwaka kwa ajili ya maadhimisho ya Wiki na Siku ya Sheria ambayo kwa mwaka
huu 2025 inasema, ‘Tanzania 2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki Madai katika
Kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo’.
“Hatuwezi kuwa na malengo ya kimaendeleo ya muda mrefu ikiwa tuna Mahakama ambayo ina malengo yanayokinzana na dira yetu kama Taifa, lakini ninaipongeza sana Mahakama ya Tanzania kwa kuwa malengo yake yamewekwa wazi na yamejikita katika mabadiliko chanya ya utoaji haki kwa wakati na kwa kuweka msisitizo mkubwa wa matumizi ya TEHAMA jambo ambalo tunaona kuwa linaenda sambamba na Dira yetu ya Taifa ya Maendeleo,” alisisitiza Mhe. Sendiga.
Naye,
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza
amewahakikishia wananchi kuwa Mahakama na wadau wake wako tayari kuwahudumia
wakati wote wa maadhimisho hayo na hata baada ya hapo, kwani bado wanayo nafasi
ya kufikisha kero, malalamiko na maoni yao kwenye madawati maalum ambayo yapo
katika kila Mahakama.
“Tunawasisitiza
sana wananchi muweze kuhudhuria maeneo mbalimbali ambayo tutakuwa kwa hii wiki
yote, kwa sababu hiki ni kipindi ambacho wananchi wataweza kupata elimu
mbalimbali kutoka kwa watumishi wa Mahakama na pia mtapata huduma mbalimbali
kutoka kwa wadau wa Mahakama ambao tutakuwa tumeambatana nao katika kipindi
hiki chote” alisema Mhe. Kahyoza.
Wiki
ya Sheria kwa Mahakama Kanda ya Manyara imeanza kutekelezwa kuanzia tarehe 25
Januari, 2025 kwa kutoa elimu sehemu za Mkoa wa Manyara, kwenye mabanda
yaliyopo kwenye Viwanja vya Kituo cha zamani cha mabasi Babati, mashule,
vyuoni, kwenye masoko na minada pamoja na vyombo vya habari kwa lengo la
kufikisha elimu ya masuala mbalimbali ya kisheria kwa wananchi.
Mkuu wa Mkoa wa Manyara Mhe. Queen Cuthbert Sendiga akihutubia wananchi na watumishi wa Mahakama (hawapo pichani) wakati wa uzinduzi wa maadhimisho ya wiki ya sheria mjini Babati jana tarehe 25 Januari, 2025.
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara, Mhe. John Kahyoza akiwahakikishia wananchi uwepo wa huduma za kisheria zitakazo tolewa wiki ya sheria kwa mkoa wa Manyara na Wilaya zake.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni