- Majaji wajadili maandalizi usikilizaji mashauri 139
- Mfumo wa kuratibu mashauri kuanza kutumika
Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama,
Dar es Salaam
Amidi wa Majaji wa
Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Augustine Mwarija leo tarehe 7 Februari, 2025
ameongoza kikao kazi maalum kuangalia maandalizi yaliyofanyika ili kuhakikisha
mashauri yaliyopangwa kwa muda wa wiki tatu zijazo yanasikilizwa bila vikwazo
vyovyote.
Kwa mara ya kwanza, kikao
hicho kimeendeshwa kwa njia ya mtandao kikiwaunganisha Majaji wa Mahakama ya
Rufani, Jaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu katika Kanda na Divisheni, Naibu
Wasajili, Wasaidizi wa Sheria wa Majaji na Makarani ambao walikuwa kwenye
maeneo mbalimbali nchini.
Kadhalika, kikao hicho
kimewahusisha Wadau kama Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Ofisi ya Wakili
Mkuu wa Serikali, Magereza, Jeshi la Polisi, Chama cha Mawakili Tanganyika na
wengine wengi.
Kikao hicho kimejadili
mashauri 139 ambayo yatasikilizwa na majopo matano, yaani matatu yatakayoketi
Dar-es-Salaam na mengine mawili ambayo yapo Makao Dodoma. Kesi nyingi za Dodoma
zinahusu masuala ya kodi na biashara, huku za Dar es Salaam zikihusu ardhi na
madai mengine.
Akizungumza katika kikao
hicho, Mhe. Mwarija amewaelekeza Mawakili wote watakaohusika kwenye usikilizaji
wa mashauri hayo kufika mahakamani kwa tarehe walizopangiwa ili kusiwepo na
sababu zozote zitakazokwamisha usikilizaji wa mashauri ambayo yamepangwa kwenye
vikao hivyo.
Kadhalika, Jaji Mwarija
amewataka wataalam wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) wa Mahakama
ya Tanzania kujiandaa vizuri kwani, kwa mara ya kwanza, Majaji wa Mahakama ya Rufani
wamejipanga kuanza kutumia kikamilifu Mfumo wa Kuratibu Mashauri kusikiliza
mashauri hayo.
Akiwasilisha taarifa ya
Msajili wa Mahakama ya Rufani kuhusu mashauri hayo, Naibu Msajili, Mhe. Dyness
Lyimo amewaeleza wajumbe wa kikao hicho kuwa maandalizi yote yameshakamilika na
sehemu kubwa ya wadaawa wameshajulishwa kuhusu vikao vitakavyoanza tarehe 10
hadi 28 Februari, 2025.
“Tupo tayari kwa usikilizaji wa mashauri yote ambayo yamepangwa baada ya maandalizi kukamilika,” Mhe. Lyimo amesema.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni