Na KANDANA LUCAS- Mahakama, Musoma
Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania Kanda ya Musoma, Mhe. Fahamu Hamidu Mtulya, ametoa pongezi kwa watumishi wote wa Kanda ya Musoma walioshiriki kwenye bonanza la michezo lililofanyika mwanzoni mwa mwezi Februari, 2025 likihusisha Mahakama za Kanda tatu ambazo ni Mwanza, Musoma na Shinyanga.
Akizungumza na watumishi wa Kanda hiyo katika kikao maalumu cha kupokea makombe ya ushindi na kutambua wanamichezo walioiwakilisha vyema Mahakama Kuu Musoma, kilichofanyika katika ukumbi wa mikutano wa Mahakama hiyo hivi karibuni, Mhe. Mtulya alieleza namna alivyofurahishwa na ushindi huo kisha kuwahimiza watumishi kufanya mazoezi ya mara kwa mara ili kuimarisha afya zao na kuwa tayari kushindana pale inapohitajika.
“Ndugu watumishi, nimewaita kushiriki kikao hiki maalumu ili nitoe pongezi kwenu hasa kwa wanamichezo wote walioshiriki katika bonanza la michezo lililofanyika mwishoni mwa wiki iliyopita. Ushindi huo uwe chachu ya kuendelea kufanya mazoezi ya mara kwa mara ili kujiimarisha zaidi kiafya na kuwa na utayari wa kushindana muda wowote mashindano yanapojitokeza”. Mhe Mtulya alisema.
Katika Bonanza hilo lililofanyika jijini Mwanza, Kanda ya Musoma iliibuka mshindi wa jumla kwa kutwaa makombe matatu kati ya manne yaliyokuwa yameandaliwa pamoja na zawadi za mchezaji mmoja mmoja.
Michezo ambayo Musoma waliibuka washindi wa kwanza ni pamoja na mchezo wa kamba wanaume na wanawake, mpira wa pete, mchezo wa karata, kukimbiza kuku, kete/draft (wanaume),mchezo wa kukimbia na yai kwenye kijiko (wanaume na wanawake) na kukimbia kwenye magunia (wanaume na wanawake).
Viongozi wengine waliotoa pongezi za ushindi huo ni Jaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Musoma Mhe. Kamazima Kafanabo Idd, Naibu Wasajili (Mhe. Salome Mshasha, na Mhe. Monica Ndyekobora) na Mtendaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Musoma Bw. Leonard Maufi. Kwa nyakati tofauti, viongozi hao wamewapongeza watumishi wote walioshiriki katika mashindano hayo kwa kuonesha ushindani mkubwa hadi kutwaa tuzo mbalimbali.
Ushiriki katika michezo hiyo ni mwendelezo wa utekelezaji kwa vitendo mipango mbalimbali ya Kanda hiyo kuanzia usikilizwaji wa mashauri, ikizingatiwa mwaka 2024 Kanda nzima haikuvuka na mashauri mlundikano, ushiriki katika masuala ya kijamii kama vile watumishi kutembelea vivutio vya utalii na watumishi kutembelea vituo vya watu wenye mahitaji maalum (matendo ya huruma).
(Habari hii imehaririwa na MAGRETH KINABO-Mahakama, Dodoma)

Hakuna maoni:
Chapisha Maoni