Alhamisi, 6 Februari 2025

MAHAKAMA INAYOTEMBEA KUCHANJA MBUGA KATIKA MIKOA MINGINE SITA NCHINI

Na INNOCENT KANSHA – Mahakama, Morogoro

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel amesema Mahakama Inayotembea (Mobile Court) imeongeza kiwango kikubwa cha upatikanaji wa huduma za haki nchini na huduma hiyo muhimu imekuwa chachu na kuongeza ufanisi wa utoaji haki kwa wananchi. Mahakama inajivunia kutumia huduma hiyo kuwafikia wananchi badala ya wananchi kuifuata Mahakama mahali ilipo.

Akizungumza na Waandishi wa Habari na Umma kwa ujumla kupitia vyombo vya Habari mkoani Morogoro leo tarehe 6 Februari, 2025 kuhusu utekelezaji wa bajeti na majukumu ya Mahakama ya Tanzania kwa nusu mwaka wa fedha 2024/2025, Prof. Ole Gabriel amebainisha kuwa, huduma hiyo muhimu ya Mahakama mtaani kwako ama Mahakama Inayotembea ilianza kutumika kama programu ya majaribio (Pilot Program) kupitia Mikoa miwili ya Dar es salaam na Mwanza.

“Mahakama ya Tanzania imeongeza idadi ya Mahakama hizo kutokana na umuhimu wa mahitaji ya huduma hiyo kwa wananchi kutoka mbili za awali na kufikia nane kwa maana Mahakama zinazotembea sita tayari zimeagizwa mpaka sasa Mahakama hizo tatu zimekwisha pokelewa na kupelekwa maeneo yenye uhitaji. Lakini wigo wa huduma hiyo umetanuka na itapatikana katika mikoa ya Dodoma, Mbeya na Tabora ambao ni mkoa mkubwa sana katika nchi yetu,” ameongeza Prof. Ole Gabriel.

Prof. Ole Gabriel amesema, kwa kupitia huduma ya Mahakama Inayotembea kuendesha mashauri yaliyofunguliwa na wananchi. Mashauri 39 tu ndiyo yalivuka mwaka 2024 na mashauri 2369 yalifunguliwa na jumla ya mashauri 2374 yaliamuriwa sawa na asilimia 98.5 ya mashauri yote yaliyotolewa uamuzi mwaka 2024.

“Huduma ya utoaji haki kupitia Mahakama Inayotembea imewafikia wananchi wapatao 14,225 hii ni idada kubwa kwa kipindi kifupi sana, ikiwemo wanawake 7,697 na wanaume 6,528 hii inaonesha wanawake ni takribani asilimia 54 na wanaume ni asilimia 46 ya wale ambao wamefikiwa na kufungua mashauri yao katika  Mahakama hii,” amesema Mtendaji Mkuu huyo.

Huduma ya Mahakama Inayotembea imehakikisha inazingatia pia kutoa huduma bora kwa watu wenye mahitaji maalum imetengenezwa kumuwezesha mtu huyo kutumia ngazi maalum itakayoweza kumwezesha kuingia kwenye Mahakama hiyo ili kuhudumiwa kirafiki bila kujali hali ya muhusika. Kwa sababu Mahakama inaamini kwamba Mungu ndiye amemuumba kila mtu kwa namna ambavyo alivyo, ameongeza Prof. Ole Gabriel.

“Hivyo kwa maelekezo mahususi sana ya Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amesisitiza kwamba huduma zetu ziwe zinamlenga mwananchi (Citizen Centric) kwa hali yoyote ile na hii huduma sasa imekuwa ikisaidia sana kwa sababu huduma sasa imekuwa ikimfuata mwananchi badala ya wananchi kufuata huduma,” amesisitiza Mtendaji Mkuu.

Aidha, Mtendaji Mkuu huyo akataja maeneo takribani sita ya vipaumbele vya bajeti ya mwaka 2024/2025 pamoja na mambo mengine yamejikita katika kutekeleza majukumu ya vipaumbele, mosi ni kuharakisha utatuzi wa mashauri kwa kuondoa mashauri mlunikanao kwani kazi ya Mahakama ni kutoa maamuzi kwa njia ya kusikiliza mashauri yanayoletwa na wananchi mahakamani, kuimarisha uwezo katika usimamizi wa shughuli za kimahakama, kuendelea kutekeleza mpango wa ujenzi na ukarabati wa majengo katika maeneo mbalimbali nchini.

Vilevile, Prof. Ole Gabriel ameongeza kuwa vipaumbele vingine ni Uboreshaji wa mifumo ya tekinolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwa kutumia zaidi wataalum wa ndani, lakini pia kuongeza ushirikiano wa wadau mbalimbali mfano; Jeshi la Polisi, Magereza, Ofisi ya Mwendesha Mashtaka ya Taifa, Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Wakili Mkuu wa Serikali, Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Ustawi wa Jamii pamoja na wadau wengine katika mnyororo wa utoaji haki nchini na kuboresha maeneo ya rasilimali watu (Human Capita Development HCD).

Mahakama ina amini inapowekeza katika mafunzo kwa watumishi inapata watumishi wenye uwezo mkubwa na kupata matokeo chanya kwenye utendaji wa kutoa huduma kwa ufanisi mkubwa wa kuwahudumia wananchi.  

Mtendaji Mkuu huyo wa Mahakama akatoa rai na kuwasihi Waandishi wa Habari nchini kuendelea kuandika mambo kwa ufasaha, weledi na kuyaandika kwa fikira chanya ‘positive mind set’ ili kuuelimisha umma mambo yanayotekelewa na mhimili kwa manufaa ya umma kwa sababu mwandishi atakapo andika habari changanishi za kufanya yule mlaji wa habari achanganyikiwe itapunguza imani kwa mwananchi dhidi ya chombo chao ni matumaini ya Mahakama kwa waandishi wa hapa Morogoro lakini pia waandishi kote nchini watakuwa wamepokea rai hiyo na litakuwa ni jambo la maana katika kuwahudumia umma wa watanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifafanua jambo kwa Waandishi wa Habari wakati wa mkutano wake kupita vyombo vya Habari mkoani Morogoro leo tarehe 6 Februari, 2025 kuhusu utekelezaji wa bajeti na majukumu ya Mahakama ya Tanzania kwa nusu mwaka wa fedha 2024/2025.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifafanua jambo kwa Waandishi wa Habari wakati wa mkutano wake kupita vyombo vya Habari mkoani Morogoro leo tarehe 6 Februari, 2025 kuhusu utekelezaji wa bajeti na majukumu ya Mahakama ya Tanzania kwa nusu mwaka wa fedha 2024/2025.


Sehemu ya Mwandishi wa Habari kutoka vyombo mbalimbali walioshiriki mkutano huo.
Sehemu ya Mwandishi wa Habari kutoka vyombo mbalimbali walioshiriki mkutano huo.

 


Sehemu ya Viongozi mbalimbali Waandamizi kutoka Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro walioshiriki Mkutano huo, wa kwanza kushoto ni Katibu wa Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Bw. Majuto Mdenya.

Mwandishi wa Habari akimuuliza swali Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani) wakati wa mkutano huo. 

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akimsikiliza Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro Mhe. Stephen Magoiga walipokutana ofisini kwake Kituo Jumishi cha Utoaji Haki mjini Morogoro.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel akifafanua jambo wakati alipokutana na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro Mhe. Stephen Magoiga ofisini kwake Kituo Jumishi cha Utoaji Haki mjini Morogoro.
Mwandishi wa Habari akimuuliza swali Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo pichani) wakati wa mkutano huo. 

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni