Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Mahakama ya Tanzania
imeendelea kutekeleza jukumu lake la kikatiba la utoaji haki kwa Wananchi kwa
ufanisi mkubwa kwa mwaka 2024, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof.
Elisante Ole Gabriel, amesema.
Akizungumza na Waandishi
wa Habari mkoani hapa leo tarehe 6 Februari, 2025 kuhusu utekelezaji wa bajeti
na majukumu ya Mahakama ya Tanzania kwa nusu mwaka wa fedha 2024/2025, Prof. Ole Gabriel amebainisha
kuwa Mahakama imepiga hatua katika viashiria vyote vikuu vya utendaji kazi
ikilinganishwa na mwaka 2023.
Ameeleza kuwa kiwango cha
umalizaji wa mashauri kimeongezeka kwa asilimia 101, huku kiwango cha
uondoshaji wa mashauri kikipanda kwa asilimia 84 na wastani wa muda wa kumaliza
shauri ukipungua hadi siku 78.
“Mahakama za Mwanzo
ambazo zimehudumia Wananchi wengi zaidi kwa asilimia 70 wanaotafuta haki kwenye
mfumo wa Mahakama zilitumia wastani wa siku 37 kumaliza shauri moja. Wastani wa
mashauri kwa kila Jopo umepungua toka mashauri 234 mwaka 2023 hadi 227 mwaka
2024,” amesema.
Akizungumzia Mahakama
Inayotembea, Mtendaji Mkuu amebainisha kuwa mashauri 39 yalivuka mwaka na mashauri
2,369 yalifunguliwa, ambapo jumla ya mashauri 2,374 yamesikilizwa na kumalizika,
sawa na asilimia 98.5 ya mashauri yote.
“Mahakama Inayotembea
imeendelea kutoa huduma kwa Mikoa ya Dar es Salaam na Mwanza. Wigo wa huduma
katika kipindi husika umeongezeka kwa Mikoa ya Mbeya na Dodoma. Hivi karibuni,
huduma zitaanza mkoani Tabora. Huduma hii kwa sasa imenufaisha watu 14,225,
wakiwapo wanawake 7,697 na wanaume 6,528,” amesema.
Prof. Juma ameeleza pia
kuwa kwa sasa Mahakama Inayotembea inatoa huduma katika ngazi ya Mahakama za
Mwanzo, hivyo kusogeza huduma karibu na Wananchi na imeonesha kuwa na ufanisi
kwa kusikiliza mashauri mengi kwa gharama nafuu na kwa muda mfupi.
Ameeleza kuwa siri ya
mafanikio hayo inatokana na utendaji na uwajibikaji nzuri wa Majaji, Mahakimu,
Watendaji na Watumishi wa Mahakama kwa ujumla, ushirikiano wa Wadau, matumizi
ya teknolojia na uwezeshaji wa Serikali katika maeneo mbalimbali, ikiwemo
rasilimali fedha na watu.
Katika kipindi husika,
Mtendaji Mkuu amebainisha kuwa jumla Majaji watano wa Mahakama ya Rufani na
Jaji mmoja wa Mahakama Kuu ya Tanzania wameteuliwa, hivyo kuongeza kasi ya
usikilizaji na umalizaji wa mashauri.
Aidha, Prof. Ole Gabriel amesema,
katika kipindi husika, Mahakama ya Tanzania imeajiri jumla ya watumishi 498,
kati yao wakiwa Mahakimu Wakazi 88, Watumishi 1,167 wamepandishwa vyeo na
wengine 107 wamebadilishwa kada, kati yao wakiwa Mahakimu Wakazi 43.
Mahakama ya Tanzania,
katika kutekeleza majukumu yake ya kikatiba, inatumia Mpango Mkakati wa Mwaka
2020/21- 2024/25 ambao umeweka vipaumbele katika maeneo mbalimbali.
Maeneo hayo ni
kuharakisha utatuzi wa mashauri na kutekeleza mkakati wa kumaliza mashauri ya
muda mrefu; kuimarisha uwezo katika ukaguzi na usimamizi wa shughuli za Mahakama
na kuendelea kutekeleza Mpango wa Ujenzi na Ukarabati wa Majengo ya Mahakama
katika ngazi mbalimbali.
Maeneo mengine ni kuboresha
Mifumo ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kama nyenzo muhimu ya
kuboresha utoaji wa huduma; kuongeza ushirikiano na Wadau ili kuharakisha
huduma ya utoaji haki na kuimarisha maendeleo ya rasilimaliwatu, ikiwa ni
pamoja na mafunzo na nidhamu kwa Watumishi.
Kwa mujibu wa Ibara ya 4(2) na 107A (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chombo chenye mamlaka na kauli ya mwisho katika kutekeleza utoaji haki ni Mahakama ya Tanzania. Mahakama ya Tanzania ipo katika ngazi za Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu (Kanda na divisheni), Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na Mahakama ya Mwanzo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni