Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Matumizi ya Teknolojia ya
Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kwenye shughuli za kimahakama yameleta mafanikio
makubwa kwa Wananchi, ikiwemo kupunguza gharama na muda kwenye mchakato mzima
wa utoaji haki.
Akizungumza na Waandishi
wa Habari mkoani hapa leo tarehe 6 Februari, 2025, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya
Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amesema kuwa TEHAMA inamwezesha Mwananchi
kufungua shauri popote alipo na kusikilizwa kwa njia ya kielektroniki bila ya
kulazimika kwenda mahakamani.
Ametaja baadhi ya mifumo
mbalimbali inayomilikiwa na Mahakama ya Tanzania ambayo inamwezesha Mwananchi
kupata huduma mbalimbali za kimahakama kwa urahisi kama Mfumo wa kielektoniki
wa Kuratibu Mashauri (e-CMS), Mfumo wa Kunukuu na Kutafsiri Mwenendo wa
Mashauri (TTS), Mfumo wa Takwimu (Data Hub) na Mfumo wa Taarifa za Hukumu na
Sheria Tanzania (TanzLII).
“Mfumo wa TanzLII
umeondoa kabisa malalamiko ya Wananchi ya kupata hukumu baada ya shauri
kumalizika kwa upande wa Mahakama Kuu na Mahakama ya Rufani. Kwa sasa hukumu
zinapandishwa kwenye Mfumo huo siku hiyo hiyo baada ya kusomwa. Hadi sasa jumla
ya uamuzi 60,319 umechapishwa katika mfumo wa TanzLII,” Mtendaji Mkuu amesema.
Prof. Ole Gabriel
ameeleza baadhi ya mafanikio ambayo yamepatikana kufuatia matumizi ya TEHAMA
mahakamani, ikiwemo kufanikisha upatikanaji wa takwimu za Mahakama za Mwanzo
kupitia Mobile App na kufanikisha upatikanaji wa nakala za hukumu kwa wateja
kupitia mfumo.
Mafanikio mengine ni upatikanaji
wa taarifa mbalimbali za mwenendo wa mashauri kupitia ujumbe mfupi (SMS), utoaji wa namba za
mashauri kupitia mfumo wa kielektroniki na kuwezesha usajili wa mashauri kwa
njia ya kielektroniki, hivyo kupunguza muda na gharama na mwingiliano kati ya
Watumishi wa Mahakama na Wananchi.
“Maboresho katika nyanja
ya TEHAMA ni endelevu hususan katika kuhakikisha huduma ya utoaji haki inafanyika kwa haki na kwa wakati,” Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania
amesema na kuongeza kuwa mifumo
ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ni nyenzo muhimu katika
kuboresha utoaji wa huduma mahakamani.
Prof. Ole Gabriel amewaeleza Waandishi wa Habari
kuwa Mahakama ya Tanzania itaendeleza matumizi ya TEHAMA katika shughuli
mbalimbali za Mahakama kwa ngazi zote na kuongeza wigo wa huduma za TEHAMA kwa
kujumuisha mifumo inayotumia akili mnemba kupitia simu za mkononi.
Kadhalika, Mtendaji Mkuu ameeleza kuwa Mahakama ya
Tanzania itaendelea kutoa mafunzo kwa Majaji, Mahakimu, Makarani na maafisa
TEHAMA; kuimarisha ushirikiano na Wadau katika kubadilishana taarifa ili
kuongeza ufanisi na kuendeleza ubunifu na kuzingatia mahitaji ya watumiaji wa
mifumo ya TEHAMA katika kutumia teknolojia ya hali ya juu.
Kwa mujibu wa Ibara ya 4(2) na 107A (1) ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, chombo chenye mamlaka na kauli ya mwisho katika kutekeleza utoaji haki ni Mahakama ya Tanzania. Mahakama ya Tanzania ipo katika ngazi za Mahakama ya Rufani, Mahakama Kuu (Kanda na divisheni), Mahakama za Hakimu Mkazi, Mahakama za Wilaya na Mahakama ya Mwanzo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni