Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam
Mahakama ya Tanzania
inaendelea kutekeleza Mpango wa Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Mahakama
kwa kujenga majengo ya kisasa katika maeneo mbalimbali nchini ili kusogeza huduma
za kimahakama karibu zaidi na Wananchi na kuimarisha mifumo ya utendaji kazi.
Hayo yamebainishwa na
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel mkoani hapa
leo tarehe 6 Februari, 2025 alipokuwa anaongea na Waandishi wa Habari kuhusu
utekelezaji wa bajeti na majukumu ya Mahakama ya Tanzania kwa nusu mwaka wa fedha 2024/2025.
“Hadi kufikia Disemba,
2024, Mradi wa Maboresho kupitia fedha za Benki ya Dunia umeendelea kutekelezwa
katika miradi ya ujenzi wa majengo ya Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki tisa katika
Mikoa ya Katavi, Simiyu, Songwe, Ruvuma, Geita, Lindi, Njombe, Singida na Pemba
na Mahakama za Mwanzo 60 katika Mikoa mbalimbali hapa nchini,” amesema.
Prof. Ole Gabriel
amebainisha kuwa ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania jijini
Dodoma umefikia asilimia 97.5 huku ujenzi wa nyumba za Majaji jijini Dodoma ukiwa
umefika asilimia 98.5.
“Jengo hili litakapozinduliwa
litakuwa la sita kwa ukubwa duniani na la kwanza katika Bara la Afrika.
Tunaishukuru sana Serikali inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania,
Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa kutoa fedha za ujenzi wa jengo hili la
kihistoria katika nchi yetu,” amesema.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama
ametaja miradi mingine inayoendelea kama ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya
Korogwe ambao umefikia asilimia 80 na ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya ya
Ubungo ambao upo asilimia 97.
“Ujenzi wa majengo ya
Mahakama za Mwanzo saba za Ilangala (Ukerewe) ambao umefika asilimia 20,
Mbalizi (Mbeya) asilimia 64, Ketumbeine (Arusha) asilimia 80, Machame
(Kilimanjaro) asilimia 10, Kinusi (Mpwapwa) asilimia 25, Rugwa (Manyoni) asilimia
0.05 na Haubi asilimia 28,” amesema.
Prof. Ole Gabriel ameeleza
pia kuwa ujenzi wa majengo ya Mahakama za Wilaya nane nao unaendelea kwa
viwango tofauti huku Mahakama ya Wilaya Kibiti (Pwani) ikifikia asilimia 3.5,
Nachingwea (Lindi) asilimia 2, Simanjiro (Manyara) asilimia 2, Hanang (Manyara)
asilimia 4.1, Mbulu (Manyara) asilimia 5, Chamwino (Dodoma) asilimia 15.3,
Mkalama (Singida) asilimia 5 na Tunduru (Ruvuma) asilimia 1.5.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama
amesema pia kuwa miradi ambayo ipo katika hatua za awali na manunuzi na Wakandarasi
wamekabidhiwa maeneo ya ujenzi hivi karibuni kwa miradi ya ujenzi wa jengo la
Mahakama ya Wilaya Kilosa; Uyui na ujenzi wa jengo la Mahakama za Mwanzo Magubike
(Kilosa) na Kipili (Sikonge).
Ametaja miradi iliyo
katika hatua mbalimbali za manunuzi kama ujenzi wa jengo la Mahakama ya Wilaya Masasi,
Handeni; Kishapu; Tarime; Kiteto; Kalambo; Mlele; Momba; Mkalama; Nyasa na
Rufiji, ujenzi wa Mahakama za Mwanzo Mkuyuni na Mkomazi na ukarabati wa nyumba
za Majaji katika Mikoa ya: Iringa; Mbeya; Tanga na Tabora.
Prof. Ole Gabriel
amewaeleza Waandishi wa Habari kuwa Mahakama ya Tanzania itaendelea kuboresha
mazingira ya kazi kwa Watumishi, kuendelea kuboresha taratibu za utaoji huduma
ili kuongeza ufanisi, kuendelea kuboresha Majengo ya Mahakama yaliyopo na
kujenga mapya na kuendelea kutekeleza Mpango wa Ujenzi na Ukarabati wa
Miundombinu ya Mahakama kwa kuzingatia vigezo vilivyoainishwa.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni