Jumanne, 4 Februari 2025

ELIMU YA SHERIA YAWAFIKIA WANANCHI TAKRIBANI 5000 JIJINI MBEYA

Na Daniel Sichula-Mahakama, Mbeya

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda Mbeya Mhe. Joachim Tiganga jana tarehe 03 Februari, 2025 aliwaongoza wananchi na wadau wa tasnia ya sheria katika kilele cha maadhimisho ya siku ya sheria nchini katika sherehe zilizofanyika viwanja vya Mahakama Kuu Mbeya.

“Tunashukuru katika maadhimisho haya ya wiki sheria tumeweza wafikia takribani ya wananchi 5000 kwa kuwasaidia na kutoa elimu ya sheria ana kwa ana, na wengine wengi wamefikiwa kutoka kupitia vipindi vya radio mbalimbali jijini Mbeya”, alisema Mhe. Tiganga.

Mhe. Tiganga aliongeza kuwa, shughuli zote hizo zimefanikiwa kutokana na ushirikiano mkubwa uliooneshwa kutoka kwa watumishi wa Mahakama wakiongozwa na Waheshimiwa Majaji, Mahakimu, wadau mbalimbali wa sheria kutoka Taasisi tofauti za kiserikali na zisizo za kiserikali kama vile Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea, Ofisi ya mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jeshi la Polisi, Magereza na Ofisi ya Mwendesha Mashtaka wa Serikali.

“Niwashukuru wadau wote wa sheria kwa namna walivyojitokeza kwa wiki nzima na kutoa elimu ya sheria na msaada wa kisheria kwa wananchi waliojitokeza katika mabanda ya maonesho na vitu mbalimbali vilivyowekwa ili kufikisha huduma za kisheria karibu na wananchi na wengine walifikiwa na elimu  hiyo ya sheria kwa kupitia vipindi vya radio mbalimbali zinazopatikana jijini Mbeya,” alisema Jaji Mfawidhi.

 Aidha, Mhe. Tiganga alielezea kauli mbiu ya maadhimisho ya siku ya sheria inayoenda sambamba na malengo ya Dira ya Taifa ya maendeleo ya 2050 kuwa utoaji haki kwa wakati na kwa wote utasaidia kutatua changamoto za migogoro ya haki madai na kusaidia kukuza maendeleo ya kiuchumi na kuvutia wawekezaji.

Naye, Mkuu wa Wilaya ya Mbeya Mhe. Beno Malisa aliushukuru Uongozi wa Mahakama Kuu Mbeya kwa jitihada wanazofanya katika kusimamia na kutoa haki kwa wakazi wa Mbeya.

“Mhe Jaji Mfawidhi na jopo lako la Majaji na Mahakimu napenda kutoa shukrani zangu kwa niaba ya Mkuu wa Mkoa Mbeya kwa kazi nzuri ambayo mnaifanya kwa kusimamia sheria na kutenda haki, napenda kutoa wito kwa wanasiasa pale kunapokua na migogoro kwa wananchi wenu mnaowaongoza muwape ushauri wa kwenda mahakamani kwani wao ndiyo wanaweza kutatua migogoro hiyo kwa wakati,” alisema Mhe. Malisa.

Wakati huo huo, Mhe. Tiganga alipokea taarifa toka kwa wadau wa sheria Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) taarifa yao iliwasirishwa na Wakili Baraka Mbwilo na ilijikita zaidi katika dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kugusia mambo ya haki madai kwa ujumla na kuihamasisha Serikali na Mahakama kutilia mkazo suala hilo kwani linagusa watu wengi.

Wakili Mbwilo alisema kuwa, suala la ardhi katika dira ya 2050 ni la kulipa kipaumbele ili mwananchi wa kawaida aweze kumiliki ardhi. Serikali inawajibika   kuweka mipango madhubuti katika upimaji wa ardhi na kuweka gharama ambazo mwananchi wa kawaida anaweza kulipia na kuongeza idadi ya walipa kodi kwa ajili ya maendeleo ya Taifa.

















 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni