Jumanne, 4 Februari 2025

MAADHIMISHO YA WIKI YA SHERIA YAHITIMISHWA MKOANI SONGWE

Na IMAN PATSON MZUMBWE – RM, Songwe

Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Mhe. Francis Kishenyi, amewashukuru wadau na watumishi wote wa Mahakama Mkoa wa Songwe kwa kushiriki katika zoezi la utoaji elimu katika maadhimisho ya wiki na siku ya sheria nchini.

Mhe. Kishenyi ameyasema hayo wakati wa Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini kwa mwaka wa waka 2025 jana tarehe 03 Machi, 2025 katika sherehe zilizofanyika katika viwanja vya Mahakama ya Mkoa Songwe.

“Nimefurahishwa na zoezi hili pamoja na muitikio wa wananchi waliojitokeza kupokea elimu, nawashukuru kwa moyo wa dhati kwani elimu hiyo itasaidia kutatua baadhi ya migogoro bila kufikishana Mahakamani, nawashauri wadau na wananchi kumaliza mashauri kwa njia ya usuluhishi kwani kumaliza shauri kwa njia ya usuluhishi hutumia muda mfupi na kuokoa rasilimali fedha na hii itawafanya wananchi kufanya shughuli zao za kimaendeleo ili kufanikisha dira ya 2050...

Nawasihi Mawakili wa Serikali na wa Kujitegemea na wadau wote wa Mnyororo wa haki kuhakikisha wanajitahidi kuwashauri wadau wetu wakimbilie kwenye usuluhishi kwani ni njia nzuri inayojenga amani kati ya mtu na mtu, usuluhishi pia ufanywe na viongozi wa dini na amewaomba viongozi hao katika nafasi zao pale wanapowapokea wadaawa katika maeneo yao kabla ya kufika mahakamani washauriwe wamalize kwa njia ya usuluhishi ili kujenga Amani”, alisema Mhe. Kishenyi.

Kwa upande wake, Mkuu wa Wilaya Mbozi Mhe. Hamadi Mbega ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa Songwe Mhe. Daniel chongolo ameipongeza Mahakama ya Mkoa wa Songwe kwa kazi nzuri wanayoifanya  na ameeleza kuwa wataendelea kushirikiana nayo na kuhakikisha inafanya kazi  zake bila kuingiliwa, pia amewasihi Mawakili wa Serikali na Kujitegemea kuwa na jukumu la kuisaidia Mahakama katika zoezi zima la kufanikisha  utoaji haki kwa wananchi.

Aidha, Mwenyekiti wa kamati ya Elimu Mkoani Songwe Mhe, Vitalis Change amesema kuwa zoezi la utoaji elimu limefanikiwa kwa kiwango kikubwa kwa kuwafikia takribani watu 3,032 huku tukifanikiwa kuzifikia shule za sekondari kumi (10) na shule za msingi tisa (9) jumla ya shule zote ni kumi na tisa (19) hicho ni kiwango kikubwa ukilinganisha na maadhmisho ya wiki na siku ya sheria kwa mwaka wa 2024.

Naye, mwakilishi wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Mhe, Moses Mwampashi, ameeleza kuwa, chama kimejipanga kimkakati ili kuhakikisha kwamba kinatoa mchango wa kitaaluma kadiri iwezekanavyo na kama inavyohitajika ili kutekeleza tija na ufanisi katika malengo ya dira ya Taifa ya maendeleo 2050, aliendelea kwa kusema baadhi ya mambo ambayo yamekusudiwa kuyafanywa ni pamoja na kuboresha mahusinao na wadau mbalimbali wa haki hususani mahakama na wadau wengine, pia amesema kua chama kimejipanga kuendelea kutoa elimu kwa umma kuhusu maswala ya haki kwa ujumla.

Naye, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe Bw. Sosteness Mayoka amewashukuru, wadau, wageni waalikwa na watumishi kwa ujumla kwa ushirikiano wao tangu zoezi lilipofunguliwa na hadi mwisho kilele cha siku ya sheria nchini ambapo imehitimishwa tarehe 3, Feburuari 2025.

Sherehe hizo za siku ya kilele zimehitimishwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Songwe huku wadau mbali mbali wa Mahakama wakiwa wamehudhuria tatika maadhimisho hayo ya kilele cha siku ya sheria nchini.






















Hakuna maoni:

Chapisha Maoni