Na HUBERT MAANGA-Mahakama, Mtwara
Jaji Mfawidhi mpya wa
Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki amekabidhiwa
ofisi na mtangulizi wake, Jaji Rose Ally Ebrahim, ambaye amehamishiwa Mahakama
Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro kuendelea na wadhifa kama huo.
Makabidhiano hayo yaliyofanyika
hivi karibuni yalishuhudiwa na Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya
Mtwara, Mhe. Said Ramadhani Ding’ohi na Mhe. Martha Mpaze, Naibu Msajili, Mhe.
Seraphine Nsana, Mtendaji wa Mahakama Mtwara, Bw. Yusuph Issa Msawanga na Hakimu
Mkazi Mkuu Mfawidhi, Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mzava.
Akizungumza katika hafla
hiyo, Mhe. Ebrahim aliwashukuru Viongozi na watumishi kwa ushirikiano
waliompatia katika kipindi chote alichokaa Mtwara na kuwaomba kuendeleza
ushirikiano huo kwa Jaji Mfawidhi mpya katika utekelezaji wa majukumu ya
kimahakama.
Alisisitiza kuwa msingi
wa mafanikio ni ushirikiano, upendo, utendaji kazi kwa weledi, uwazi na
masikilizano.
Kwa upande wake, Mhe. Kakolaki alishukuru kwa mapokezi mazuri aliyopata kutoka kwa wenyeji wake na kuahidi kuendeleza mazuri aliyoyakuta. Aliomba ushirikiano na kuwahimiza Viongozi na watumishi kufanya kazi kwa weledi na kutoa haki kwa wakati.
Jaji Rose Ebrahim (kulia) akimkabidhi vitendea kazi vya ofisi ya Jaji Mfawidhi mpya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kushoto).


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (katikati) akiwa kwenye picha ya pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu Kanda ya Mtwara na watumishi baada ya mapokezi mazuri. Wengine ni Mhe. Rose Ebrahim (wa pili kushoto) aliyehamishiwa Mahakama Kuu Kanda ya Morogoro, Mhe. Saidi Ding’ohi (wa pili kulia) na Mhe. Martha Mpaze (wa kwanza kushoto) pamoja na Naibu Msajili, Mhe. Seraphine Nsana (wa kwanza kulia).
(Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Saklaam)


Hakuna maoni:
Chapisha Maoni