Na Mwandishi Wetu - Mahakama, Momba
Jaji
Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda
ya Mbeya, Mhe. Joachim Charles
Tiganga, tarehe 14 Februari 2025 amefungua mafunzo
maalum ya wadau wa haki jinai katika Wilaya ya Momba yaliyolenga kuboresha
utoaji wa haki kwa kuepusha kutonesha majeraha ya kisaikolojia kwa wahanga wa
ukatili wa kingono pamoja na matumizi ya adhabu mbadala katika mfumo wa haki
jinai ili kupunguza mlundikano
wa wafungwa katika magereza.
Mhe.
Tiganga amesisitiza umuhimu wa mafunzo hayo
kwa wadau wa sekta ya sheria na kuelekeza kuwa ni muhimu yakawafikia wadau wote
wa mkoa wa Songwe ili kuongeza ufanisi katika utoaji haki.
Aidha,
aliwapongeza wadau wa Mahakama Momba kwa kushiriki kwa pamoja katika mafunzo
hayo na kwa kujadiliana
kuhusu changamoto na mbinu bora za kuboresha utendaji kazi katika eneo hilo muhimu. Alisisitiza kuwa
ujuzi walioupata hauna budi kusambazwa
kwa wengine ambao hawakupata fursa ya kushiriki, ili kuhakikisha maarifa haya
yanawanufaisha wadau wote wa haki.
Pia, Mhe. Tiganga aliwahimiza
washiriki kuyatumia ipasavyo mafunzo hayo katika kutekeleza majukumu yao kwa
weledi katika kutenda haki.
Mafunzo
hayo yamefanyika katika ukumbi wa Mahakama ya Wilaya
Momba na kuhudhuriwa
na mahakimu wa
ngazi mbalimbali pamoja na wadau wa haki jinai ndani ya wilaya hiyo, Mkuu wa
Mashtaka wa Wilaya, waendesha
mashitaka, Kaimu Mganga Mkuu wa Mji, Afisa Ustawi
wa Jamii na wasaidizi wa kumbukumbu wa Mahakama.
Mafunzo
hayo yaliyopewa jina la “Enhancing
Justice Delivery: Integrating Trauma-Informed Approaches and Community-Based
Rehabilitation’’ yalifanyika
kwa lengo la kuwajengea uwezo washiriki katika kushughulikia wahanga wa ukatili
wa kingono na kuhakikisha kuwa mfumo wa haki jinai unatoa suluhisho mbadala kwa
wahalifu wa makosa madogo kupitia huduma kwa jamii badala ya vifungo vya
kawaida.
Aidha, Mafunzo hayo ni mwendelezo wa mafunzo ya kuzuia
kutonesha majeraha kwa wahanga wa ukatili wa kingono yaliyoendeshwa na Chuo cha
Uongozi wa Mahakama Lushoto kwa ushirikiano na Taasisi ya Irish Rule of Law
International (IRLI) jijini Dodoma kuanzia tarehe 4 hadi 6 Februari, 2025.
Katika
mafunzo hayo,
mada mbalimbali ziliwasilishwa na kujadiliwa kwa kina, ikiwa ni pamoja na Mikakati ya Kuzuia
Kutonesha Majeraha ya Kisaikolojia kwa Wahanga wa Ukatili wa Kingono iliyowezeshwa na Hakimu Mkazi
Mfawidhi Mahakama ya Wilaya Momba Mhe. Raymond V. Kaswaga, ambapo washiriki
walijifunza namna ya kutambua na kuwalinda mashahidi na wahanga wa ukatili wa
kijinsia na kingono.
Aidha, ilielezwa umuhimu wa mbinu
za kuzingatiwa na wadau wa haki jinai katika kuhakikisha mashahidi na wahanga
wa ukatili hawapati madhara zaidi wanapotoa ushahidi mahakamani.
Naye, Afisa Huduma za Uangalizi
kwa Jamii Bw. Nelson Duba, aliwaongoza
washiriki kubadilishana uzoefu wa namna ya kutoa adhabu
ya huduma kwa jamii kwa makosa yanayostahili adhabu mbadala ambayo ni ya kifungo cha chini
ya miaka mitatu. Washiriki walijifunza jinsi huduma kwa jamii inavyosaidia
katika urekebishaji wa wahalifu na kupunguza gharama kwa Serikali za uendeshaji wa
magereza.
Washiriki hao, walipata nafasi ya
kujifunza tofauti kati ya wafungwa wa huduma kwa jamii na wale wa uangalizi maalum
(probation) ambapo pamoja na mambo mengine ilielezwa kuwa wafungwa
hufuatiliwa na maafisa maalum wa uangalizi badala ya kutumikia vifungo
gerezani.
Kwa upande wake, Hakimu
Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu
Mkazi Songwe, Mhe. Francis Kishenyi, alisisitiza kuwa mafunzo hayo yana umuhimu mkubwa
katika kuleta mabadiliko chanya katika utoaji wa haki kwa njia mbadala na kwa
kuzingatia athari za kihisia na
kisaikolojia kwa wahanga wa matukio ya ukatili wa kingono na kueleza kuwa Mafunzo
hayo yataacha msingi imara wa
maboresho katika sekta ya haki wilayani humo.
Washiriki wa mafunzo hayo yaliyofanyika Mahakama ya Wilaya Momba wakifuatilia mafunzo hayo.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni