Ijumaa, 14 Februari 2025

RAIS CHAMA CHA MAWAKILI WA SERIKALI AMTEMBELEA JAJI MKUU

  • Jaji Mkuu atoa ushauri mzito kwa Chama

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dar es Salaam

Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali, Bw. Amedeus Shayo leo tarehe 14 Februari, 2025 amemtembelea Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma kwa lengo la kujitambulisha na kufanya naye mazungumzo mafupi.

Bw. Shayo, ambaye ni Wakili wa Serikali Mwandamizi kutoka Benki Kuu ya Tanzania, aliwasili ofisini kwa Jaji Mkuu katika jengo la Mahakama ya Rufani jijini Dar es Salaam saa 3.00 asubuhi, akiwa ameambatana na Wakili wa Serikali Mwandamizi, akiwakilisha Mkoa wa Dar es Salaam, Bi. Debora Mcharo.

Katika mazungumzo yake, Kiongozi huyo amemweleza Jaji Mkuu kuwa Mawakili wa Serikali wote ni wanachama wa Chama anachokiongoza ambacho ni cha kitaaluma na wala hakihusiani na kujihusisha na harakati za Wafanyakazi.

“Mteja wetu sisi kama Mawakili wa Serikali ni mmoja, tunasimamia maslahi ya Serikali nchi nzima. Ili uwe mwanachama lazima uwe Mwanasheria wa Serikali na lazima usajiliwe kwenye daftari la Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali. Kwa hiyo, hili ni jukwaa la kitaaluma, ni vema Mahakama pia ikatutambua,” amesema.

Bw. Shayo amemjulisha Mhe. Prof. Juma kuwa mwezi wa Aprili 2025 watakuwa na Mkutano Mkuu wa Chama na wanatarajia, pamoja na wageni wengine, kumwalika Jaji Mkuu ili aweze kushiriki.

Ameahidi ushirikiano na Mahakama ili Chama hicho kiweze kutoa mchango wake katika shughuli za kimahakama, ikiwemo Wiki na Siku ya Sheria kwani wanataka kushiriki kikamilifu kwa upande wao.

Kwa upande wake, Jaji Mkuu amewapongeza kwa imani kubwa ambayo wamepewa na Mawakili wa Serikali kukiongoza Chama hicho. Amemweleza Kiongozi huyo kwamba yeye binafsi anakifahamu Chama hicho kwani amekuwa akihudhuria mara kwa mara kwenye mikutano yao.

Mhe. Prof. Juma amemweleza Bw. Shayo pia kwamba Chama kina uwezo na wanaweza kutoa mchango mkubwa kwa Serikali na Mahakama kwa sababu wapo katika kila sehemu ya sheria.

“Ukianza kuangalia wasifu wa kila mmoja wenu utakuta mpo katika maeneo ya kimaboresho na maendeleo. Lakini bahati mbaya unaweza kukuta hayo maeneo ambayo mmesomea wengi hamuyatumii,” Jaji Mkuu amesema.

Ameeleza kuwa Chama hicho kinaweza kuwa mwamvuli na kuwa na vitengo vya kufanya tafiti katika maeneo mbalimbali kwenye Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 na kushauri namna ya kufikia malengo yanayokusudiwa.

“Rasimu ya Dira ya 2050 imetoa maeneo mengi sana ambayo yanahitaji mabadiliko na maboresho makubwa. Wakati mwingine ndani yenu mnahitaji kuwa na vitengo vya kufanya utafiti na kutoa mawazo yenu kwa faragha,” Mhe. Prof. Juma amesema.

Amekishauri Chama hicho kuanza kuwafahamu wanachama wake na kutambua ujuzi wa kila mmoja ili weweze kutumia elimu waliyonayo iliyojificha, ambayo hawaitumii, katika maeneo mbalimbali kama biashara, uwekezaji na masuala ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano.

Viongozi wa Mahakama waliohudhuria ugeni huo ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi na Katibu wa Msajili Mkuu, Mhe. Dkt. Jovin Bishanga.


Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali, Bw. Amedeus Shayo akizungumza alipokutana na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma  ofisini kwake jijini Dar es Salaam leo tarehe 14 Februari, 2025.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza na mgeni wake (juu na chini).


Viongozi wa Mahakama waliohudhuria ugeni huo. Kutoka kulia ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya, Katibu wa Jaji Mkuu, Mhe. Venance Mlingi na Katibu wa Msajili Mkuu, Mhe. Dkt. Jovin Bishanga.

Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali, Bw. Amedeus Shayo (kushoto) akichukua kumbukumbu muhimu. Kulia ni Wakili wa Serikali Mwandamizi, akiwakilisha Mkoa wa Dar es Salaam, Bi. Debora Mcharo.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Rais wa Chama cha Mawakili wa Serikali, Bw. Amedeus Shayo (wa pili kulia). Wengine ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Kiaki Nkya (wa pili kushoto), Wakili wa Serikali Mwandamizi, akiwakilisha Mkoa wa Dar es Salaam, Bi. Debora Mcharo (wa kwanza kulia) na Katibu wa Msajili Mkuu, Dkt. Jovin Bishanga










Hakuna maoni:

Chapisha Maoni