Jumatatu, 3 Februari 2025

RAIS WA TLS AIMWAGIA SIFA ‘KEM KEM’ MAHAKAMA YA TANZANIA

Na INNOCENT KANSHA- Mahakama, Dodoma

Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Wakili Msomi Boniface Anyesile Kajujumele Mwabukusi leo tarehe 03 Februari, 2025 amesema, Chama hicho kinatambua na kupongeza jitihada kubwa zilizokwisha fanyika na zinazoendelea kufanywa na Mahakama ya Tanzania za ujenzi wa miundombinu ya kisasa pamoja na uwekezaji mkubwa katika Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) ili kurahisisha uratibu, usimamizi, uendeshaji na usikilizwaji wa mashauri na Uwekezaji huo Chama kimeuona kwa macho na kimetembelea maeneo hayo.

Akizungumza wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini zikiashiria kuanza kwa mwaka wa kimahakama, zilizofanyika kitaifa katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma, Wakili Mwabukusi amesema, “Uwekezaji huo ni wa kipekee na wa kujivunia, ambao hautii shaka hata kidogo ukiwa na nia thabiti ya kuimarisha mfumo wa utoaji haki nchini. Miundombinu hii inaifanya Mahakama ifikiwe na watu wote bila kujali umbali au mahali popote alipo mtu,” amesema Rais wa TLS.

“Chama kinatoa rai kwamba, wakati Mahakama ikiendelea na maboresho haya tusiwasahau wanaohusika kule ndani hususani Mahakimu, Mahakimu wanafanya kazi chini kabisa kule kwa wananchi. Kwa kweli majengo yanavutia sana na teknolojia ni nzuri na ya kisasa lakini ni vema tuhakikishe tunaboresha maslahi na mazingira yao ya utendaji kazi. Kwa sababu ni hatari sana mwananchi mwenye shida kukutana na wakili mwenye msongo wa kipato na Hakimu mwenye msongo wa kipato hapo anayeshughulikiwa ni mwananchi. Kwa hiyo kuboresha mazingira yao itakuwa zaidi ni kuwasaidia wananchi,” amesisitiza Wakili Mwabukusi.

Aidha, akizungumzia Kauli mbiu ya wiki ya sheria na siku ya sheria nchini 2025 inayosema, ‘Tanzania 2050: Nafasi ya Taasisi Zinazosimamia Haki Madai katika Kufikia Malengo Makuu ya Dira ya Taifa ya Maendeleo’.

Rais huyo amesema, nampongeza Jaji Mkuu na Mahakama kwa kauli mbiu hiyo imeletwa muda muafaka, kama ilivyo mwelekeo wa Dira ya Taifa ya Maendeleo ya mwaka 2025 ni kuwa na Taifa Jumuishi lenye ustawi, haki na linalo jitegemea pamoja na mambo mengine dira hiyo inajenga kukuza mfumo wa utawala wa haki na uliyojumuishi.

Msingi wa dira ni utawala, amani, usalama na utulivu ambapo lengo ni kuwa na mfumo imara wa kisheria na kitaasisi katika utelekelezaji endelevu wa maendeleo ya watu na wenye ufanisi.

“Mhe. Mgeni Rasmi nijaribu kuangalia Dira ya Taifa ya Maendeleo na hali ilivyo ya kisheria, ni matarajio ya Chama kuwa, wakati tukiendelea kuboresha na kujipanga tuhakikishe kwamba, tunaweka utaratibu wa kisheria wa kuhakikisha kuwa, sheria na sera zinazotungwa ziwe katika namna ya ushirikishaji wa kutosha wa wananchi katika ngazi zote,” amesema Rais Mwabukusi.

Aidha, Wakili Mwabukusi amesema pia dira ilenge katika kuongeza uwezo wa Taasisi katika utoaji wa huduma za kisheria kwa wananchi hasa kwa makundi yaliyo pembezoni na kuondoa mambo yote ya kiufundi na kuweka mkazo katika kutatua migogoro inayofikishwa mbele ya vyombo vya maamuzi. Kwani mambo ya kiufundi yanawagharimu sana wananchi na kuchelewesha haki. Hivyo tulenge kuelekea kwenye utaratibu huo unalenga nafuu ya kisheria kwa wananchi.

Vilevile, kujenga na kuimarisha ushirikiano wa Serikali na Sekta binafsi kama ambavyo TLS na Serikali wanavyofanya kazi kwa pamoja kwenye kampeni ya Mama Samia ya msaada wa kisheria. Kwa hiyo Chama kinaposhirikiana na Serikali siyo kweli kwamba Chama kinalamba asali. Chama kinapata changamoto wananchi wanapoona kinashirikiana na Serikali. TLS si kikundi cha magaidi ni chama kilichoanzishwa kisheria na moja ya kazi yake ni kuwahudumia wananchi kwa kushauri masuala ya kisheria na kuwawakilisha kwenye vyombo vya kutoa haki.

“Hivyo TLS itaendelea kutimiza wajibu wake wa kisheria kama kuna sehemu ya kuonya itaonya kwa haki, kama kuna sehemu ya kupongeza itafanya hivyo kwa haki pia, na sehemu ya kushiriki kufanya kazi tutashiriki pamoja kulijenga Taifa letu na kumuhudumia mtanzania,” amefafanua Rais huyo.

Wakati huo huo Wakili Mwabukusi ameongeza kuwa, dira itilie mkazo katika sheria za nchi zinazolinda rasilimali, kila taifa lina rasilimali za kulinda kwa Tanzania kuna ardhi, Mbunga za wanyama, Bahari, mito, maziwa na madini. Sheria, kanuni, sera na taratibu zinazotungwa zihakikishe zinalinda maeneo hayo kwa wivu mkubwa kwa sababu ndiyo urithi utako achwa kwa kizazi kijacho kitakacho weza kushindana na mataifa mengine kiuchumi.

Vilevile, akifafanua kazi mahususi ya Chama hicho Rais huyo amesema, “Sisi Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) tunaongozwa na kifungu cha nne cha sheria ya Mawakili na mambo yetu ya msingi tunayofanya ni kuimarisha ustawi wa tasnia ya sheria, kuhamasisha utawala bora na utawala wa sheria, kulinda na kusaidia umma wa watanzania katika masuala yote yanayohusiana na sheria,” amefafanua.

Wakili Mwabukusi amempongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kwa kubuni na kuanzisha kampeni ya msaada wa kisheria yenye lengo la kuwasaidia wananchi na Chama hicho kimekuwa kikishiriki katika kampeni hiyo mikoa yote kuwafikia wananchi. Hivyo kupitia programu kama hizo Serikali inakuwa inakisaidia Chama moja kwa moja, kwani wengi wanaokuwa na matatizo ya kisheria ni wananchi ambao hawana namna yoyote ile ya kupata huduma ya mawakili kulingana na uwezo wao wa kiuchumi na maeneo waliko, wengi wao wamekuwa wakisaidiwa na kufikiwa.

“Kwa hiyo huduma hii ya Mama Samia ya msaada wa kisheria iwe endelevu na tuone namna ya kuiboresha zaidi iwe endelevu na ya kudumu,” ameongeza Wakili Mwabukusi.


Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Wakili Msomi Boniface Anyesile Kajujumele Mwabukusi leo tarehe 03 Februari, 2025 akitoa hotuba kwa niaba ya chama hicho wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini zikiashiria kuanza kwa mwaka wa kimahakama, zilizofanyika kitaifa katika viwanja vya Chinangali jijini Dodoma.

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akifuatilia kwa makini hotuba ya Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Wakili Msomi Boniface Anyesile Kajujumele Mwabukusi.
Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan akifurahi jambo wakati wa hotuba ya Rais wa Chama cha Wanasheria Tanganyika (TLS) Wakili Msomi Boniface Anyesile Kajujumele Mwabukusi (hayupo pichani) leo tarehe 03 Februari, 2025.


Kwaya ya Ng'aring'ari ya Mahakama ya Tanzania kitoa burudani mbele ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan wakati wa sherehe za maadhimisho ya kilele cha siku ya sheria nchini.
Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.

Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, Makamisha wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Viongozi wa Dini wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.
Sehemu ya Viongozi Wakuu waandamizi wa Mahakama ya Tanzania walioshiriki sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.

Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania pamoja na Majaji wa Mahakama Kuu wakiimba wimbo wa Taifa na Afrika Mahariki wakati wa kuanza kwa sherehe hizo.


Sehemu ya wanafunzi walioshiriki sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini
Sehemu ya wanafunzi walioshiriki sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.
Sehemu ya Mawakili wa serikali na wa kujitegemea walioshiriki sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.
Sehemu ya Viongozi waandamizi wa Mahakama ya Tanzania walioshiriki sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.

Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.
Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini
Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, wakifuatilia matukio mbalimbali wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini

Makamisha wa Tume ya Utumishi wa Mahakama na Viongozi wa Dini kiwa wamesimama wakati wa wimbo wa Taifa wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.

Majaji wa Mahakama ya Rufani ya Tanzania, na sehemu ya Majaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania wakipokea heshima wakati Jaji Mkuu wa Tanzania alipokuwa anakagua gwaride maalum wakati wa sherehe za kilele cha kuadhimisha siku ya sheria nchini.

(Picha na Innocent Kansha - Mahakama)
  

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni