Jumanne, 4 Februari 2025

TANZANIA BORA YA MWAKA 2050 ITAJENGWA NA JAMII YENYE MAADILI; JAJI KAHYOZA

Na CHRISTOPHER MSAGATI-Mahakama, Manyara

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Rugalema Kahyoza amewasisitiza wananchi na wadau wa Mahakama kuelimishana na kuwa na jamii yenye maadili na tabia njema ikiwa wanataka kuwa na Nchi yenye maendeleo kiuchumi, kisisasa na hata kijamii ifikapo Mwaka 2050.

Mhe Jaji Kahyoza ameyaeleza hayo wakati wa Kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2025 jana tarehe 03 Februari, 2025 katika sherehe zilizofanyika katika viwanja vya Mahakama Kuu Manyara.

‘‘Ni kweli Serikali na Taifa kwa ujumla wetu tunatamani sana kuona kuwa tuna nchi yenye Uchumi unaokuwa na wenye tija na faida kwa kila mtu. Haya yote hayatawezekana endapo tutakuwa tuna taifa lenye watu wasiokuwa na maadili katika jamii.  Mkoa wa Manyara umekuwa na changamoto ya makosa mengi ya ukatili wa kijinsia kama vile Ubakaji na Ulawiti, sasa taifa haliwezi kufika mbali kimaendeleo kama hatutaacha tabia hizi’’ amesema Mhe. Kahyoza.

Akizungumzia Dira ya Maendeleo ya Mwaka 2050, Mhe. Kahyoza alisema kuwa Mahakama ya Tanzania imeunga mkono juhudi za Serikali kwa kuhakikisha matumizi makubwa ya TEHAMA katika shughuli zake na kuwezesha upatikanaji wa Haki kwa Wakati.

“TEHAMA imetuwezesha sana kusikiliza mashauri yetu kwa wakati na hata kuyatolea maamuzi kwa wakati, taarifa mbalimbali zinazohusu Mahakama pia zinapatikana kwa njia ya mtandao. Kimsingi jitihada hizi zote zinalenga kuwezesha Taifa letu kuwa na mazingira wezeshi ya Utoaji Haki ulio thabiti ambao pia unawahamasisha wawekezaji wa ndani na Nje ya Nchi kufanya mambo yao kwa utulivu pasipo kuwa na usumbufu wowote na jambo hili litafanya taifa letu kuwa na maendeleo tuyatakayo”. alisema Mhe Kahyoza

Naye, Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga, ameishukuru Mahakama kwa utaratibu wa Wiki ya Sheria na kutoa mfano wa namna walivyoweza kutoa elimu katika maeneo mbalimbali ya Mkoa wa Manyara katika wiki nzima. Pia alitoa wito kwa Mahakama na wadau wake kuendelea kutoa elimu zaidi ya masuala mbalimbali ya kisheria kwa jamii, jambo litakalo saidia kupunguza malalamiko mengi ambayo yanatokana na uelewa mdogo wa sheria.

“Mahakama imejitahidi sana kutoa elimu kwa wananchi katika kipindi hiki. Nimeweza kufanya ziara katika Wilaya za Mbulu, Kiteto na Simanjiro na katika meneo yote nimefurahi kuona jinsi mlivyojipanga kuwaelimisha wananchi wa Mkoa wa Manyara. Niwaombe suala hili liwe endelevu kwani kwa kiasi kikubwa litapunguza malalamiko na moigogoro katika jamii”. alisema Mhe. Sendiga.

Mahakama Kuu Kanda ya Manyara, kama zilivyo Mahakama katika Kanda nyingine nchini imehitimisha Maadhimisho ya Wiki ya Sheria Nchini kwa Mwaka 2025 ambayo yalianza rasmi mnamo tarehe 25 Januari, 2025 na kuhitimishwa jana tarehe 03 Februari, 2025 kukiwa na mafanikio makubwa ya kumaliza asilimia 97% ya mashauri yaliyofunguliwa mnamo mwaka 2024 kwa upande wa Mahakama Kuu na pia kutokuwa na mashauri yaliyozidi miezi mitatu kwa upande wa Mahakama za Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Rugalema Kahyoza akihutubia wananchi na wadau mbalimbali wa Mahakama siku kilele cha maadhimisho ya siku ya sheria nchini Mahakama Kuu Manyara.

Mkuu wa Mkoa wa Manyara, Mhe. Queen Cuthbert Sendiga akiwahutubia wananchi na wadau mbalimbali wa Mahakama katika sherehe za maadhimisho hayo.

Sehemu ya wananchi na wadau mbalimbali wa Mahakama katika sherehe za maadhimisho hayo.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Manyara Mhe. John Rugalema Kahyoza (katika) wakiwa kwenye picha ya pamoja na watumishi wa Mahakama katika sherehe za maadhimisho hayo.


Sehemu ya Viongozi mbalimbali kiserikali, Mawakili na watumishi wa Mahakama walishiriki katika sherehe za maadhimisho hayo.


Sehemu ya Viongozi mbalimbali  na watumishi wa Mahakama walishiriki katika sherehe za maadhimisho hayo.
















Hakuna maoni:

Chapisha Maoni