Jumatano, 19 Machi 2025

JAJI KIONGOZI AWASHA TAA NYEKUNDU MATUMIZI YA KARATASI MAHAKAMANI

  • Ahimiza matumizi ya mifumo kwenye utoaji haki

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mwanza

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani amewahimiza Majaji Wafawidhi kuzidisha matumizi ya mifumo ili kufikia azma ya Mahakama ya Tanzania ya kuachana na karatasi katika shughuli zote za kimahama.

Mhe. Dkt. Siyani ametoa wito huo leo tarehe 19 Machi, 2025 alipokuwa anafunga Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni, kilichokuwa kinafanyika jijini hapa.

‘Uzoefu tulioupta kutoka Kanda ya Geita ni uthibitisho tosha kwamba matumizi ya e-judiciary yanawezekana na changamoto chache za kimfumo hazitoshi kuwa sababu za kuturudisha nyuma kwenye karatasi,’ Jaji Kiongozi amesema.

Amewakumbusha Majaji Wafawidhi hao kuwa kwenye kikao chao walijadiliana pia kuhusu matumizi ya mifumo ya e-judiciary katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.

Kadhalika, aliwakumbusha kuwa kwa muda mrefu, Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na viongozi wengine wa Mahakama, wamekuwa wakisisitiza kuachana na matumizi ya karatasi na badala yake kuhakikisha huduma za haki zinatolewa kisasa kwa njia ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHEMA.

‘Katika hotuba yake ya ufunguzi, Jaji Mkuu alisisitiza matumizi ya TEHEMA na taarifa zilizomo katika mifumo yetu, hasa takwimu za mashauri mbalimbali kufanya maamuzi…

‘Bila shaka, kupitia mifumo yake, Mahakama ina chakata taarifa nyingi ambazo zikitumika ipasavyo zitasaidia sana kuboresha huduma za haki, ikiwemo kujulisha maeneo yanayohitaji mitizamo mipya ya sheria, tabia za jamii zinazotuzunguka katika vituo vyetu vya kazi na nini kifanyike ili kudumisha haki na amani kwenye maeneo husika,’ Mhe. Dkt. Siyani amesema.

Jaji Kiongozi amebainisha kuwa Jaji Mkuu ameelekeza na Watumishi wa TEHAMA wametekeleza kwa kutengeneza daftari maalumu(ledger) kwa ajili ya kusajili changamoto zozote za kimfumo ili kuwajulisha wajenzi kuzitafutia ufumbuzi na hivyo kujenga uwajibikaji.

Kwa mujibu wa Mhe. Dkt. Siyani, hali ilivyo kwa sasa bado kuna baadhi ya Kanda zinapokea nyaraka za mashauri kupitia mfumo na kisha kuitisha nakala ngumu ili kufungua majalada ya mashauri.

‘Hii si sahihi. Mbali na kuchelewesha kufikia azma ya kuwa mahakama isiyotumia karatasi, matumizi ya karatasi yanaiongezea Mahakama gharama ambazo TEHAMA imeshaleta unafuu wake…

‘Fedha zinazotumika kununulia karatasi na majalada zingeliweza kutatua changamoto zingine kwenye Kanda zenu ikiwemo kuweka mazingira bora ya kazi na kuongeza ari kwa Watumishi,’ amesema.

Jaji Kiongozi amebainisha pia kuwa baada ya kuwa wameweza kutumia mifumo kusajili na kusikiliza mashauri kwa mwaka mzima uliopita, haitarajiwi tena sasa kushuhudia utaratibu wa zamani wa kutumia karatasi katika utaoaji huduma au kuchanganya baina ya mifumo sambamba na karatasi.

‘Tumeona mifano ya kanda zinazotumia mifumo kwa asilimia100 na hivyo hakuna sababu kwa nini sote tusifanye hivyo. Ninajua baadhi yenu mnahofia kwamba kuna siku mifumo itashindwa kufanya kazi,’ amesema.

Mhe. Dkt. Siyani amewatoa hofu Majaji Wafawidhi hao kuwa mifumo ya Mahakama imejengwa na kuhakikiwa na wataalamu wa ndani, ina ulinzi wa kutosha na kuna hifadhi kubwa, hivyo hakuna kumbukumbu itakayopotea.

Baadhi ya Viongozi wa Mahakama waliohudhuria Kikao hicho ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mtendaji wa Mahakama Kuu-Kanda, Mtendaji wa Mahakama Kuu-Divisheni, Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu, Wakurugenzi mbalimbali, Naibu Wasajili na wengine.

Mbali na kujadili masuala mbalimbali yanayohusu utendaji wa Mahakama, Kikao hicho pia kilitoa fursa ya kujipima na kujitathmini kuhusu utendaji kazi, sambamba na utekelezaji wa Mpango Mkakati, Dira na Dhima ya Mahakama.

Aidha, Majaji walipata fursa muhimu ya kubadilishana uzoefu kwenye utendaji wa kazi za Mahakama, pamoja na kutambua na kujadili changamoto mbalimbali zinazojitokeza katika Mahakama Kuu na Mahakama za chini yake na hivyo kutafuta majibu kwa changamoto hizo.


Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akizungumza wakati anafunga Kikao cha siku tatu cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni, kilichokuwa kinafanyika jijini Mwanza.


Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Chiganga Tengwa akitoa maelezo ya utangulizi kabla ya kumkaribisha Jaji Kiongozi kufunga Kikao hicho.


Majaji Wafawidhi-juu na chini- wakimsikiliza Jaji Kiongozi katika siku ya tatu ya Kikao hicho.



Sehemu nyingine ya Majaji Wafawidhi-juu na picha mbili chini- wakimsikiliza Jaji Kiongozi katika siku ya tatu ya Kikao hicho.




 

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni