Jumanne, 18 Machi 2025

JAJI MKUU NA MSISITIZO WA MAMBO 12 KWA MAJAJI WAFAWIDHI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mwanza

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma jana tarehe 17 Machi, 2025 alifungua Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni, na kusisitiza mambo 12 wanayotakiwa kuzingatia wanapotekeleza majukumu yao katika muktadha mzima wa utoaji haki nchini.

Mhe. Prof. Juma aliwapongeza Majaji Wafawidhi kwa sababu wao, katika nafasi zao kama Viongozi ni wasimamizi wakubwa, sio tu katika muhimu utoaji wa haki, lakini pia katika maboresho ya maendeleo.

“Matunda makubwa tunayapata chini ya Uongozi wenu, maboresho yanafanyika makubwa, mmesimamia vyema hili gurudumu ambalo linasukuma mbele maboresho. Mradi wa maboresho wa Benki ya Dunia wasimamizi wake wakubwa wamekuwa ni nyinyi Majaji Wafawidhi…

“Nyingi ndio mmekuwa mkisimamia matumizi ya teknolojia katika utoaji haki na kazi hii mmefanya kwa mafanikio makubwa kiasi kwamba imekuwa ni kawaida mara kwa mara kupokea maombi ya Mahakama kutoka Nchi nyingine kutaka kuja kujifunza kazi kubwa ambayo tunafanya,” Mhe. Prof. Juma alisema.

Jaji Mkuu alitaja ugeni uliokuja kujifunza ni kutoka Uganda kwa mara kadhaa, kutoka Malawi, kutoka Zimbabwe, kutoka Angola, Korea Kusini, Uturuki, Jamhuri ya Watu wa China, pamoja na Vietnam na kwamba wanatarajia ugeni kutoka Kazkazistan, Nchi ambayo imepiga hatua katika teknolojia.

Kadhalika, Mhe. Prof. Juma aliwashukuru Majaji kwa kusaidia kuweka msingi imara wa utekelezaji wa Dira ya Taifa ya Maendeleo 2025 na namna ya kutekeleza Dira ya Maendeleo ya 2050.

Kuendeleza mabadiliko ya kifikra na mitazamo

Jaji Mkuu aliwaeleza Majaji Wafawidhi kuwa maboresho hayawezekani bila mabadiliko makubwa ya kifikra na mitazamo na kwamba msukumo wa maboresho ambao unaendelea ni lazima uendelezwe.

“Tayari uwekezaji mkubwa umefanywa katika Mfumo wa Tafsiri na Unukuzi, katika Mfumo wa Usimamizi wa Mashauri na usikilizaji wa mashauri kwa njia ya mtandao. Haya yote hayatadumu kama hatutayaendeleza na wenye uwezo wa kuyaendelea ni sisi wenyewe,” alisema.

Jaji Mfawidhi kioo katika Kanda au Divisheni

Jaji Mkuu aliwakumbusha Majaji Wafawidhi kuwa Watumishi waliopo chini yao mara nyingi hufuata anachokifanya Kiongozi wao. “Ukiwa una kawaida ya kuchelewa kufika ofisini, nao watachelewa. Ukiwa ni mjanja mjanja, na wao watakuwa wajanja wajanja,” alisema.

Hivyo, aliwaeleza kuwa wao kama kioo katika Kanda na Divisheni ni lazima waonyeshe uongozi katika hii zama ya matumizi ya akili bandia na teknolojia.

“Ukionekana wewe Kiongozi unatumia teknolojia unakuwa na uwezo wa kushawishi wale ambao unawaongoza kuweza vile vile kutumia teknolojia. Ukiwa wewe ni Kiongozi kazi yako ni kulalamika au kulaumu utawaambukiza wote unaowaongoza wao wawe ni watu wa kulalamika na kulaumu,” Jaji Mkuu alisema.

Majaji Wafawidhi watatuzi wa changamoto

Jaji Mkuu amewashukuru Majaji Wafawidhi kwa kufanya kazi hiyo kwa umakini mkubwa, jambo ambalo limesababisha changamoto chache kufika kwa Jaji Kiongozi na yeye hajapata changamoto kwa muda mrefu.

“Kwa hiyo, mnauwezo mkubwa wa kupima na kutatua changamoto mbalimbali ambazo tunakumbana nazo ambazo zimewawezesha kufanya maamuzi ambayo yana msaada mkubwa sana kwetu sote,” alisema.

Kadhalika, Mhe. Prof. Juma aliwashukuru Majaji hao kwa kuwa madaraja ya mahusiano mema baina au miongoni mwa mihimili kwani kaatika kazi zao wanakutana na Viongozi wa Mikoa, Wilaya na Kata ambao wana tabia na mitazamo tofauti kuhusu Mahakama.

“Kwa hiyo, tuhakikishe tunakuwa hatuna migongano ambayo haisaidii Wananchi, migongano ambayo haisaidii Taasisi zetu, siku zote tujaribu kutatua kama jambo ni zito unalipandisha juu, huku juu kuna njia za kuweza kupata utatuzi,” alisema.

Kuwalinda Majaji, Wasajili, Mahakimu wasishambuliwe kwa hila, kuonewa.

Jaji Mkuu wa Tanzania amewaambia Majaji Wafawidhi hao kuwa wasikae kimya pale wanapoona Hakimu anashambuliwa kwa hila au kwa kuonewa kwani wana mamlaka makubwa ya kusimamia nidhamu.

Alifafanua kuwa Sheria inawataka wasimamie nidhamu na kutokukaa kimya wakati Hakimu kesi inaendelea huku wahusika wanatoka nje na kuanza kuzungumzia kilichoongelewa ndani.

“Unachotakiwa kufanya ni kumuita mhusika na kushow cause, tuna mamlaka ya contempt, usipoweza kutumia hayo mamlaka utakuwa umeshindwa kufanya kazi yako kama Jaji au Jaji Mfawidhi,” alisema.

Jaji Mfawidhi kuwa wabunifu

Jaji Mkuu amewahimiza Majaji Wafawidhi kuwa wabunifu katika maeneo mbalimbali, ikiwemo kuwasaidia Watumishi wanaokuja na mawazo Chanya katika eneo hilo.

Alitoa mfano wa Mtumishi mmoja anasoma PhD Chuo cha Mandela, ambaye ameongea anaweza kuleta software ambayo ikapunguza kazi za Mahakama ya Rufan na kuwafanya Majaji wa Mahakama ya Rufani kuwa hawana kazi tena.

‘Hiyo ni provocation nzuri sana. Mtu ambaye atasaidia kupunguza kazi, huyu lazima tumsaidie kwa kile tunachoweza ili huo ubunifu utusaidie,” alisema.

Kutafuta maarifa kwa kujisomea

Jaji Mkuu aliwakumbusha Majaji Wafawidhi kujilinda na matumizi mabaya ya akili bandia na kujitafutia maarifa kwa kusoma taarifa mbalimbali. Aliwaeleza kuwa kama Kiongozi ni muhimu kuhamasisha wengine kufanya.

“Kwa hiyo, tuwe na kawaida ya kusoma kila kitu kinachokuja kwetu kinachohusu maboresho. Tusiingie katika mtego, unapata nyaraka ambayo ni muhimu sana unampa msaidizi wako asome ili akushauri, hapo unakuwa umekosa maudhui kamili ya kilichomo mle ndani,’ alisema.

Kutoa elimu, kusahihisha upotoshaji.

Jaji Mkuu aliwahimiza Majaji Wafawidhi kuwavuta karibu Wadau wote na kuwaelimisha pale panapokuwa na malalamiko na kusahihisha kama kuna upotoshaji wa aina yoyote.

‘Jukumu ni lenu kuhakikisha kwamba mnasahihisha ule upotoshwaji. Muwe karibu na Wananchi na kuwasikiliza wanapolalamika, unapomsikiliza anakusaidia kufahamu changamoto ambayo ipo katika Taasisi yako,’ amesema.

Kushughulikia malalamiko yanayojitokeza katika Vyombo vya Habari

Jaji Mkuu amewaeleza Majaji Wafawidhi hao kuwa yeye binafsi huwa najifunza mambo mengi kutokana na malalamiko katika Vyombo vya Habari na wakati mwingine katika mitandao ya kijamii.

“Wakati mwingine unaweza kufahamu kinachoendelea katika ofisi yako kwa kusomwa kinachoandikwa nje, na wakati mwingine tunafahamiana vizuri kutokana na ufafanuzi unaoandikwa kuhusu wewe,” alisema.

Mhe. Prof. Juma aliwasisitiza kutofunga milango ya kuwaruhusu Wananchi kulalamika na kuleta dukuduku zao, hivyo wanapaswa kuwapa utaratibu wa kushughulikia malalamiko na majibu.

‘Kwa hiyo tusizibe hizi nafasi za wale wanaokuwa na dukuduku zetu kwa sababu uelewa wa Sheria na taratibu za kimahakama bado ni mdogo sana katika jamii yetu,” alisema.

Umuhimu wa teknolojia miaka 25 ijayo

Jaji Mkuu amewaeleza Majaji Wafawidhi kuwa zamani walikuwa awnapambana kutokujua kusoma na kuandika, lakini katika karne ya 21 kwenye zama za Dira ya 2050, mtu ambaye hataweza kutumia mifumo ya teknolojia atakuwa ni illiterate.

‘Tunaenda katika Dunia miaka 25 ijayo ambayo huwezi kuishi bila teknolojia. Kwa hiyo, tujitayarishe kuachana na illitrace inayotokana na matumizi ya teknolojia,’ amesema.

Kadhalika, Jaji Mkuu amewahimiza Majaji Wafawidhi kusoma tena Sera, hususan Dira ya Taifa ya Maenedeleo 2025 na kufanya tathmini katika maboresho yaliyofanyika kwa msaada mkubwa wa Benki ya Dunia.

‘Tunaweza kujiuliza kama tumeweza  kutekeleza yote yaliyoainishwa katika Dira ya 2025. Kama kuna mambo ambayo hatujaweza kuyatekeleza tunaweza kuyaleta tena chini ya Dira 2050. Kwa sababu tunajinazifu kwamba sisi Mahakama tumekuwa ni mfano wa utekelezaji wa Dira ya 2025,’ alisema.

Kujitayarisha kuwa mfano wa utekelezaji Dira 2050.

Jaji Mkuu pia amewahimiza Majaji Wafawidhi kusoma kwa makini Dira ya Taifa ya Maendeleao 2050 na kuilinganisha na shughuli wanazofanya kila siku.

Alitoa mfano wa Dira hiyo inaposema ifikapo 2050, Jamhuri ya Muungano wa Tanzania itakuwa na watu million mia moja arobaini, hivyo unaweza kujenga picha majengo ya Mahakama yaliyopo kama yatatosha kutoa huduma kama inavyotolewa sasa na kama kasi ambayo tunaenda nayo sasa itaweza kumudu.

‘Kwa hiyo, huu wakati ni wa kujitayarisha na nyinyi Viongozi katika kikao hiki tuanze kutafakari kwa sababu mpango mkakati wetu wa miaka mitano nadhani unaisha Januari, mwakani,’ alisema.

Kufikiria mpango mkakati wa Mahakama wa miaka mitano ijayo.

Jaji Mkuu ameeleza kuwa kwa kuwa mipango iliyopo inaisha na Mradi wa Benki ya Dunia nao unafikia mwisho, ni vema kwa Viongozi hao kufikiria mpango mwingine wa miaka mitano ijaypo.

“Isije kuonekana kwamba uhai wetu na maboresho yetu umesukumwa zaidi na uwekaji mkubwa ambao tumepata kutoka Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ambayo imetuwezesha kufanya maboresho makubwa. Tutafute namna gani ya kuendeleza hicho ambacho tumekianza,” alisema.

Utayarishaji kwa wakati vitabu vya rufaa

Jambo lingine ambalo aliwaambia Majaji Wafawidhi hao ni kutafuta namna ya kuondoa changamoto ya ucheleweshaji wa vitabu vya rufaa baada ya wadaawa kuwasilisha taarifa ya kukata rufaa Mahakama ya Rufani.

Alibainisha kuwa taarifa za kukata rufaa nyingine ni za muda mrefu lakini Mahakama ya Rufani hawapokei vitabu kwa muda muafaka.

“Kwa hiyo vitengo vya Mahakama ya Rufani ambavyo vipo kwenu ni sehemu ya majukumu yenu kusimamia, mhakikishe vile vile inatengewa bajeti ya kutosha ili viweze kutayarisha vitabu vya Mahakama ya Rufani, kwa sababu visipoweza kufanya hivyo kutakuwa na changamoto kubwa katika usikilizaji wa rufaa,” alisema.


Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati anafungua Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni, kinachofanyika jijini Mwanza.


Sehemu ya Majaji Wafawidhi-juu na chini- wakimsiliza Jaji Mkuu-hayupo kwenye picha.



Sehemu nyingine ya Majaji Wafawidhi-juu na chini-wakiwa kwenye Kikao hicho.

 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni