Jumanne, 18 Machi 2025

UASHAURI BORA WA PROF. MAKUBI KWA MAJAJI WAFAWIDHI

  • Awaomba kulinda afya zao kwa gharama yoyote
  • Awashauri kula mbogamboga, matunda kiasi cha kutosha
  • Aeleza ‘glass’ ya wine siyo muhimu kwa afya

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mwanza

Kikao cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni, kinachofanyika jijini hapa, leo tarehe 18 Machi, 2025 kimeingia siku ya pili, huku Mkurugenzi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa. Prof. Abel Makubi akiwapitisha Majaji hao kwenye mada muhimu kuhusu afya.

Wakati akiwasilisha mada yake inayosema, ‘Mchango wa Uchunguzi wa Afya juu ya Utambuzi na Kinga dhidi ya Magonjwa’ Prof. Makubi aliwaomba wajumbe wa Kikao hicho kinachoongozwa na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Dkt. Mustapher Mohamed Siyani kulinda afya zao kwa gharama yoyote.

‘Mungu ametupa uhai, ulinde kwa gharama yoyote na kuwa na kiasi kwa mambo yote,’ Mkurugenzi huyo amekiambia Kikao hicho kinachohudhuriwa pia na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma na Viongozi wengine Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania.

Prof. Makubi aliongeza, “Uwezo wa kutunza afya yako ni mhimili mkubwa wa maisha yako marefu na ufanisi katika kazi na familia. Kufanya uchunguzi wa afya yako kila mara ni muhimu kwa ajili ya kutambua magonjwa mapema na kupewa elimu ya kinga.”

Akiwasilisha mada hiyo, Mkurugenzi huyo aliwaambia Majaji hao kuwa kuna makundi makuu mawili ya magonjwa, yaani yale ya kuambukizwa ikiwemo Ukimwi, Maleria, Ajali, Kifua Kikuu na mengine ya maambukizi na yale yasiyokuwa ya kuambukizwa kama magonjwa ya moyo, kansa, kisukari na maengine.

Amesema kuwa idadi ya watu wanaofariki dunia kutokana na magonjwa yasiyoambukizwa ni mara mbili zaidi ya wale wanaotokana na magonjwa ya kuambukiza.

‘Tatizo la magonjwa yasiyo ya kuambukiza linakua kwa kasi katika Nchi zinazoendelea, kama Tanzania na moja ya mambo yanayochangia kuongezeka kwa magonjwa haya, ni mabadiliko ya taratibu za kimaisha zinazohusisha matendo yanayoweza kusababisha ugonjwa,” amesema.

Prof. Makubi ametaja baadhi ya taratibu hizo kama kutofanya mazoezi, mfano: kukaa darasani, ofisini, kuangalia runinga, kutumia lifti, kupanda magari na kutoshiriki michezo na ngoma za utamaduni.

Nyingine ni ulaji usiofaa kama kula chakula kuzidi ya mahitaji ya mwili na hivyo kunenepa, kula mafuta na chumvi zaidi ya mahitaji ya mwili, kutokula mbogamboga na matunda kiasi cha kutosha na kula nafaka zilizokobolewa.

Mkurugenzi huyo pia aliwaambia Majaji kuwa matumizi ya pombe, tumbaku na madawa ya kulevya pamoja na msongo wa mawazo husababisha magonjwa hayo.

‘Magonjwa mengi yasiyoambukiza hayana dalili za mapema. Magonjwa mengi yasiyoambukiza yanaweza kuzuilika kwa kubadili tabia na mtindo wa maisha. Magonjwa mengi yasiyoambukiza yana gharama kubwa ya tiba. Tuendelea kupata elimu ya magonjwa ili kufahamu dalili na njia za kujikinga’ amesema.

Katika siku ya pili ya Kikao, Washiriki pia wamepitishwa kwenye mada inayohusu taarifa ya utekelezaji wa maboresho ya huduma za Mahakama iliyowasilishwa na Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho, Mhe. Dkt. Angelo Rumisha.

Wajumbe pia walipokea uzoefu kuhusu usimamizi madhubuti na umalizaji wa mashauri ndani ya muda uliotolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda na kuhusu ushirikishwaji wa Wadau kwenye utekelezaji wa majukumu ya masingi ya Mahakama uliotolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina.

Kadhalika, wajumbe walipokea uzoefu kutoka kwa Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga kuhusu ufanisi wa Mfumo wa Tafsiri na Unukuzi na ule unaohusu mbinu za kumaliza mashauri ya mlundikano uliotolewa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi.

Baadhi ya Viongozi wa Mahakama wanaohudhuria Kikao hicho ni Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Msajili wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mtendaji wa Mahakama Kuu-Kanda, Mtendaji wa Mahakama Kuu-Divisheni, Msajili Mwandamizi wa Mahakama Kuu, Wakurugenzi mbalimbali, Naibu Wasajili na wengine.

Mkurugenzi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa, Prof. Abel Makubi (juu na chini) akifafanua jambo alipokuwa ana wasilisha mada kwenye Kikao cha Majaji Wafawidhi kinachofanyika jijini Mwanza.




Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akiwasilisha maoni na pongezi baada ya uwasilishaji wa mada mbalimbali kwenye Kikao hicho.

Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani akiongoza kikao hicho.

Jaji wa Mahakama Kuu ya Tanzania na Mkuu wa Kitengo cha Maboresho, Mhe. Dkt, Angelo Rumisha akiwasilisha mada kwenye kikao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Divisheni ya Ardhi, Mhe. Elinaza Luvanda akiwasilisha mada kwenye kikao hicho.


Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Geita, Mhe. Kevin Mhina akiwasilisha mada kwenye Kikao hicho.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, Mhe. Dkt. Ntemi Kilekamajenga akiwasilisha mada kwenye Kikao.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Dar es Salaam, Mhe. Salma Maghimbi akiwasilisha mada kwenye Kikao hicho.

Majaji Wafawidhi (juu na chini) wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa uwasilishaji wa mada mbalimbali.


Sehemu nyingine ya Majaji Wafawidhi (juu na chini) wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa uwasilishaji wa mada mbalimbali.


Sehemu nyingine ya Majaji Wafawidhi (juu na chini) wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa uwasilishaji wa mada mbalimbali.



Sehemu ya Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania (juu na chini) wakifuatilia kilichokuwa kinajiri wakati wa uwasilishaji wa mada mbalimbali.


Makatibu wa Viongozi Wakuu wa Mahakama ya Tanzania wakiwa kazini.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni