Jumanne, 18 Machi 2025

KIKAO CHA WATUMISHI LINDI CHA HIMIZA NIDHAMU NA KUJALI AFYA

Na Hilari Herman – Mahakama, Lindi

Watumishi Mahakama ya Hakimu Mkazi na Wilaya ya Lindi wamefanya kikao cha kawaida cha ndani kikiongozwa Viongozi wa Mahakama hiyo ambao ni Hakimu Mkazi Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe. Consolata Peter Singano na Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela. Kikao hicho kilifanyika katika ukumbi wa wazi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi  hivi karibuni.

Akizungumza wakati wa kufungua kikao hicho Mhe. Singano amewataka watumishi wa Mahakama hizo kuzingatia zaidi suala la nidhamu mahala pa kazi huku akisisitiza watumishi wa Mahakama kuongeza uwajibikaji, uadilifu na ueledi katika kutekeleza majukumu yao.

“Hayati Mwl. Nyerere aliwahi kusema kuwa mtu yeyote asiye na maadili anaweza kufanya kazi nyingine lakini siyo uhakimu au ujaji na hii nikutokana na unyeti wa kazi hii. Natambua walizungumziwa Mahakimu na Majaji lakini watu hao hawafanyi kazi peke yao hivyo niwaombe Mahakimu na watumishi wenzangu tuwe waadilifu na wenye nidhamu,” alisema Mhe. Singano

 Mhe. Singano amesisitiza kwa watumishi hao kuwa na mawasiliano mazuri mahali pa kazi miongoni mwao wenyewe, watumishi kwa viongozi na watumshi kwa wateja, huku akiwataka watumishi hao kutambua kuwa mawasiliano mazuri huleta afya hasa ya maelewano mazuri, upendo, utatuzi wa masuala yanayoleta maswahibu, undugu, ushirikiano na zaidi kufikia mwafaka pasi na mgongano wa aina yoyote.

Kwa upande wake, Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi. Bi. Quip Godfrey Mbeyela amewahimiza watumishi kujali afya zao hasa kwa kufanya mazoezi kwa kutekeleza agizo aliloto Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara Mhe. Edwin Elias Kakolaki. Aidha amewataka watumishi kuchukua hatua madhubuti kwakufanya uchunguzi wa afya zao (body checkup) kwa lengo lakujua  afya zao.

“Nataka kila mmoja afanye uchunguzi wa afya yake ili ajue yupo imara kiasi gani jambo hii litaenda sambamba na ushauri wa kitabibu  kujua ni aina gani ya vyakula unatakiwa kula, mazoezi gani unatakiwa kufanya na mambo mengine kadha wa kadha kulingana na ushauri wa kitabibu,” alisema Mtendaji huyo

Viongozi hao vilevile waliwatambulisha watumshi wapya wa kada mbalimbali akiwemo Mtumishi aliyehamia ambaye ni Hakimu Mkazi Mwandamizi Mahakama ya Wilaya ya Lindi Mhe. Khalfan Khalfan, Watumishi ajira mpya akiwemo Afisa Tehama Bw. Furaha Khatibu, Afisa hesabu Bw. Othmani Chimko, Afisa Ugavi Msaidizi Bw Abeid Omar, Fundi sanifu wa Mifumo ya Maji Bi. Ansila Mziray na Mlinzi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bw. Jackson C. Clialence.

Zoezi hilo lilienda sambamba na utambulisho Msaidizi wa Kumbukumbu Mkuu Bw. Selemani Chikumba aliyekuwa masomoni kwa mwaka moja akisoma Shule ya Sheria kwa vitendo Zanzibar.

Kikao hicho kilihitimishwa kwa watumishi kumjua mtumishi hodari wa mwezi Februari ambae ni Bi. Mwanate Ally akihudumu kama Msaidizi wa Ofisi Mkuu. Huu ukiwa ni mwendelezo wa utoaji wa motisha kwa wafanyakazi wa Mahakama hizo ambao ni wabunifu, wenye bidii ya kazi, wanaofanya kazi  vizuri kwa mwezi husika.

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Godgrey Mbeyela  akimkabidhi zawadi ya ufanyakazi hodari Bi. Mwanate Ally (kushoto) anayehudumu kama Msaidizi wa Ofisi Mkuu. 

Hakimu Mkazi  Mfawidhi Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Mhe. Consolata Peter Singano (aliyekaa nyoosha mikono) akitoa neno wakati wa  ufunguzi wa kikao.

Hakimu Mahakama ya Wilaya ya Lindi Mhe.Khalfan Khalfan akichangia mada wakati wa kikao

Mtendaji wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Lindi Bi. Quip Godfrey Mbeyela  (aliyesimama ) akielezea moja ya ajenda ya kikao.


Sehemu ya Watumishi wakifuatilia kwa makini mada zinazowasilishwa. 


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni