Jumanne, 18 Machi 2025

MAHAKIMU WAPYA MTWARA WAKABIDHIWA KOMPYUTA MPAKATO

Na HUBERT MAANGA-Mahakama, Mtwara

Katika juhudi za kuimarisha ufanisi wa Mahakama na kuboresha utendaji wa Mahakimu, Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, imekabidhi kompyuta mpakato kwa Mahakimu wapya wa Mahakama za Mwanzo walioteuliwa hivi karibuni katika Mkoa huo.

Hafla ya makabidhiano ilifanyika hivi karibuni katika jengo la Mahakama Kuu, ikiendeshwa na Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki, huku ikiwa na lengo la kuwawezesha Mahakimu kuendesha mashauri kisasa na kidigitali zaidi katika shughuli zao kimahakama.

Akizungumza wakati wa hafla hiyo, Mhe. Kakolaki alisisitiza kutimiza waraka wa Jaji Mkuu wa Tanzania wa kujikita kwenye TEHAMA kwani katika shughuli za sasa za Mahakama, matumizi ya mifumo ya kidijitali kama eCM, na Primary Court App ndio mwenendo wa sasa wa utoaji wa haki wa haraka na uwazi.

"Nyie mmekuja muda mzuri ambapo Mahakama inaondokana na mfumo wa makaratasi, majalada yote yanapatikana kwenye mifumo. Hii ni fursa kwenu kuendesha mashauri ndani ya muda mfupi kwani mabadiliko haya yamerahisisha namna ambavyo Mahakama zetu zinahudumia Wananchi,’ alisema.

Mahakimu walionufaika na kompyuta hizo waliishukuru Mahakama kwa kuwapatia nyenzo ambazo zitarahisisha usimamizi wa mashauri, maandalizi ya hukumu na utoaji wa huduma kwa wananchi.

Waliahidi kujituma katika kutimiza majukumu yao kwa uadilifu na weledi ili kuimarisha huduma za Mahakama katika Mkoa wa Mtwara.

Jumla ya Mahakimu wanne walikabidhiwa vitendea kazi hivyo ambao ni Mhe. Mainda Sengeda wa Mahakama ya Mwanzo Dihimba, Mhe. Caroline Butambala wa Mahakama ya Mwanzo Lulindi, Mhe. Delphina Charles wa Mahakama ya Mwanzo Nakopi na Mhe. Magori Nyamwoyo wa Mahakama ya Mwanzo Mnyambe.

Katika makabidhiano hayo, waliohuduria ni pamoja na Naibu Msajili wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara, Mhe. Seraphine Nsana, Mtendaji wa Mahakama Kuu, Kanda ya Mtwara, Bw. Yussuph Msawanga na Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama ya Hakimu Mkazi Mtwara, Mhe. Charles Mnzava.

 

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki (kulia) akizungumza kabla ya kukabidhi vitendea kazi kwa Mahakimu wapya wa Mahakama za Mwanzo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akimkabidhi Kompyuta mpakato Hakimu Mkazi, Mahakama ya Mwanzo Mnyambe Mhe. Magori Nyamwoyo.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akimkabidhi Kompyuta mpakato Hakimu Mkazi, Mahakama ya Mwanzo Lulindi Mhe. Caroline Butambala.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akimkabidhi Kompyuta mpakato Hakimu Mkazi, Mahakama ya Mwanzo Nakopi Mhe. Delphina Charles.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki akimkabidhi Kompyuta mpakato Hakimu Mkazi, Mahakama ya Mwanzo Dihimba Mhe. Mainda Sengeda.

Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania (wa nne kushoto), Kanda ya Mtwara, Mhe. Edwin Kakolaki katika picha ya pamoja na viongozi wa Mahakama na Mahakimu wapya baada ya zoezi la kukabidhi vitendea kazi vipya Mahakimu hao.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mwanza.

 

.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni