Jumanne, 18 Machi 2025

MAHAKAMA YATOA ELIMU KUWAANDAA WATUMISHI KUSTAAFU

Na ASHA JUMA-Mahakama, Morogoro

Watumishi wa Mahakama wanaotarajia kustaafu kutoka katika Mikoa na Kada mbalimbali wamepata semina maalum kuhusu namna ya kuweza kukabili maisha baada ya kustaafu.

Mafunzo hayo yanafanyika kwa mujibu wa sera ya mafunzo ya Mahakama ya 2019. Sera hiyo inaelekeza Watumishi wa Mahakama wajengewe uwezo wa kujiandaa kustaafu ili waweze kukabili maisha baada ya kustaafu.

Mafunzo hayo ya siku sita yanayofanyika katika Ukumbi wa Mikutano kwenye Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki-IJC- Morogoro yalifunguliwa jana tarehe 17 Machi, 2025 na Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga.

Washiriki wa mafunzo hayo ni Watumishi wa Mahakama kutoka Makao Makuu, Mahakama ya RufanI, Kanda na Divisheni za Mahakama Kuu.

Mafunzo hayo yanaratibiwa na Mahakama na yanatolewa kwa kushirikiana na Wataalam kutoka Taasisi mbalimbali kama PSSSF, NSSSF, UTT-AMIS, Viongozi wa Dini na Wataalam wa Afya kutoka  Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.

Miongoni mwa mada zitakazowasilishwa ni pamoja na masuala muhimu ya kiafya, taratibu za kisheria za maandalizi ya kustaafu, stahiki na haki za mtumishi kabla na baada ya kustaafu, bima ya afya, ujasiliamali, mafao ya kustaafu, mirathi ya Watumishi, mifuko ya uwekezaji na masuala ya kiroho.

Akizungumza wakati wa ufunguzi wa mafunzo hayo, Mhe. Magoiga aliwaeleza wastaafu kuwa mafunzo hayo yatawapa mbinu za kukabiliana na changamoto mbalimbali, kuwapa maisha yenye tija, furaha na ustawi hata baada ya kustaafu.

“Mafunzo haya ni kwa ajili ya kuwatoa hofu kwani hofu inaua, kustaafu ni kuanza upya na kutafakari juu ya utumishi wenu,” alisema.

Mhe Magoiga aliwashukuru Watumishi hao kwa utendaji wao wa kazi akisema, “Nyinyi mna mchango mkubwa sana na tunautambua, katika mchakato mzima wa utafutaji haki, nyinyi pia mlikua na mchango mkubwa bila kujali kada zenu.”

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga akizungumza wakati akifungua mafunzo kwa Watumishi wa Mahakama wanaokaribia kustaafu.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga na Naibu Msajili, Mhe. Susan Kihawa-kushoto na kulia ni Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo, Bi. Patricia Ngungulu wakifuatilia yaliyokuwa yanajiri wakatinwa ufunguzi wa mafunzo hayo.

Watumishi kutoka sehemu mbalimbali wakifuatilia mafunzo.

Kaimu Jaji Mfawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Morogoro, Mhe. Stephen Magoiga akiwa na Watumishi mbalimbali na Wawezeshaji wa mafunzo.

Habari hii imehaririwa na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mwanza.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni