Ijumaa, 21 Machi 2025

KITUO CHA HUDUMA KWA MTEJA DARAJA MUHIMU KATI YA MAHAKAMA, WANANCHI

  • Chaadhimisha miaka mitatu tangu kianzishwe

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania, leo tarehe 21 Machi, 2025 kimeadhimisha miaka mitatu tangu kuanzishwa kwake, huku kikibainisha mafanikio makubwa yaliyofikiwa, ikiwemo kupokea na kushughulikia mrejesho kwa asilimia 100.

Maadhimisho hayo yamehudhuriwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisate Ole Gabriel, ambaye alikuwa Mgeni Rasmi, Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya, Wakurugenzi na Wakuu wa Vitengo na Watumishi wa Kituo hicho.

Akizungumza kwenye maadhimisho hayo, Mtendaji Mkuu amewapongeza Watumishi wa Kituo hicho kwa kazi nzuri wanayofanya ya kuwahudumia wateja kwa ubora na weledi wa hali ya juu na kukifanya Kituo kuwa Daraja kati ya Mahakam ana Wananchi.

‘Wapo Viongozi, Mabalozi wengi sana ambao wameshapata huduma kutoka kwa Wataalam wetu wa Kituo cha Huduma kwa Mteja. Yupo Balozi mmoja, alikuwa na suala lake fulani, tukamwelekeza Call Centre. Yule Balozi alinipigia simu akaniuliza hao vijana waliomhudumia kama ni Watanzania, au tuliwapata wapi. Hii inatufariji kwamba mnafanya kazi nzuri sana,’ amesema.

Mtendaji Mkuu amesema kuwa huduma bora zinazotolewa katika Kituo hicho zinaongeza imani ya Wananchi kwa Mahakama ya Tanzania, hasa baada ya kupokea simu 7,143, ikimanisha kuwa ndani ya siku moja wapo Watanzania wastani wa 150 ambao wangekuwa wanakosa kuhudumiwa na wasingeweza kufanya shughuli zingine za kiuchumi.

‘Hawa ni watu ambao pengine familia zao zingeweza kuwa katika matatizo, lakini pale ambapo mmeweza kuwasikiliza na kuwapa majibu wanakuwa wamebadilisha ule msimamo wao. Kituo hiki vile vile kimekuwa kikisaidia sana mawasiliano na Wananchi,’ amesema.

Akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, Msajili Mkuu ameeleza kuwa kuwepo kwa Kituo cha Huduma kwa Mteja ni dhamira ya Mahakama ya kuimarisha na kuboresha huduma zinazotolewa kupitia mrejesho, maoni, malalamiko na masuala mbalimbali yanayohusu huduma za Mahakama.

‘Kwetu Watumishi wa Mahakama, Kituo hiki kinatukumbusha juu ya kusimamia misingi ya utumishi na kutekekeleza Mkataba wa Huduma kwa Mteja,’ ameeleza.

Mhe. Nkya amebainisha kwamba kwa muda wa miaka mitatu, Kituo hicho kimepokea mrejesho takribani 7000 kutoka kwa Wananchi kuhusiana na mambo mbalimbali.

‘Ni jambo la kujivunia sana kuwa juhudi hizi zimeleta matokeo chanya katika kuimarisha imani ya Wananchi kwa Mahakama. Taarifa ya Mkurugenzi wa Usimamizi na Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Mrejesho kwa Umma na Maadili inaonesha malalamiko mahakamani yamepungua sana,’ amesema.

Naye Naibu Msajili na Mkurugenzi wa Usimamizi na Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Mrejesho kwa Umma na Maadili, Mhe. Maira Kasonde, akizungumza wakati wa maadhimisho hayo, aliwapongeza Watumishi wa Kituo kwa kuwa wabunifu na shirikishi.

‘Kituo cha Huduma kwa Mteja ndani ya kipindi husika kimekuwa siyo tu jicho, bali pia sikio la Mahakama. Kupitia Kituo hiki, Mahakama imesikia sauti ya Wananchi, tumejua nini Wananchi wanasema kuhusu huduma tunazozitoa na tumejua wapi ambapo tumefanya vizuri na wapi tunahitaji kuboresha,’ alisema.

Alibainisha kuwa ndani ya miaka mitatu, Kituo hicho kimetumiwa na Mahakama kama kioo ambapo kila mtumishi, idara na kitengo kimeweza kupata nafasi ya kujiona, kujiangalia na kuona dosari iliyopo na kuwa tayari kuirekebisha.

‘Kwa namna ya kipekee, Kituo hiki kimekuwa Daraja kati ya Mahakama na Wananchi. Tumewashirikisha Wananchi katika utoaji wa huduma zetu kupitia kupokea maoni na mapendekezo yao na hivyo kutufanya tujue wapi tunahitaji kuboresha ili tuweze kusonga mbele,’ alisema.

Akiwasilisha taarifa ya utendaji wa Kituo hicho. Hakimu Mkazi Mkuu na Mtalaam wa Kuchakata Taarifa katika Kituo hicho, Mhe. Domician Mlashani alieleza kuwa Kituo kimefanikiwa kushughulikia mirejesho yote iliyosajiliwa tangu kianzishwe.

Alieleza kuwa hadi tarehe 28 Februari ,2025, jumla ya mirejesho 6,948 ilikuwa imeshughulikiwa na kufungwa, hii ni sawa na asilimia 100.

Mhe. Mlashani alieleza mafanikio mengine kama wateja wa Mahakama kupunguziwa gharama, muda pamoja na kuongezeka kwa uwazi katika kuwasilisha na kufuatilia malalamiko yao, kufuatia uwepo wa namba ya bure (0800 750247) inayopatikana muda wote.

‘Kituo kimefanikiwa kutembelewa na wageni mbalimbali wa kitaifa na kimataifa waliokuja kujifunza namna tunavyofanya kazi. Tumepokea ugeni kutoka Mahakama ya Msumbiji, Mahakama ya Uganda, Mahakama ya Zanzibar, Maktaba Kuu ya Taifa ya Tanzania, Wizara ya Katiba na Sheria na Jeshi la Polisi, wote wakija kujifunza namna tunavyofanya kazi,’ alisema.

Mhe. Mlashani alieleza pia kuwa Kituo kimefanikiwa kutembelea Magereza mbalimbali, kuwasikiliza na kupokea mirejesho kutoka kwa wafungwa na mahabusu ambao ni wadau wa haki jinai.

Katika kipindi cha miaka mitatu, kituo kilitembelea Magereza kumi ambayo ni; Ukonga, Keko, Segerea (Dar es Salaam), Luanda (Mbeya), Karanga (Moshi), Uyui (Tabora) Butimba (Mwanza), Kisongo (Arusha), Maweni (Tanga) na Isanga (Dodoma).

Mhe. Mlashani alieleza pia kuwa kutokana na maboresho mbalimbali yaliyofanyika na yanayoendelea kufanyika mahakamani, mirejesho ya Wananchi kwa kipindi cha miaka mitatu inaonyesha baadhi ya maeneo malalamiko yamekuwa yakipungua kwa kiasi kikubwa.

Maeneo hayo ni yale yanayohusu kama ifuatavyo upatikanaji wa nakala za hukumu na mwenendo wa mashauri, utoaji wa hati za kimahakama kwa kutumia teknolojia,  utoaji wa vitabu vya rufaa za Mahakama ya Rufani, dhamana, muda wa kuanza shughuli za kimahakama na maadili juu ya Maafisa wa Mahakama.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel-juu na chini-akizungumza kwenye maadhimisho ya miaka mitatu ya Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania.



Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Mhe. Eva Nkya akizungumza kwenye maadhimisho hayo. Picha chini ni Mkurugenzi wa Usimamizi na Ukaguzi wa Huduma za Kimahakama, Mrejesho kwa Umma na Maadili, Mhe. Maira Kasonde.


Hakimu Mkazi Mkuu na Mtalaam wa Kuchakata Taarifa katika Kituo cha Huduma kwa Mteja, Mhe. Domician Mlashani akiwasilisha taarifa ya Kituo hicho.

Kiongozi Mkuu wa Kituo cha Huduma kwa Mteja, Bi. Evetha Mboya-wa kwanza kushoto-akitambulisha Viongozi mbalimbali waliohudhuria maadhimisho hayo. Wengine katika picha ni Watumishi wa Kituo hicho ambao ni Mahakimu Wakazi.


Watumishi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja cha Mahakama ya Tanzania wakitambulishwa.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel-katikati-akikata keki kwenye maadhimisho hayo. Picha chini ni muda wa shampaign.



Watumishi wa Kituo cha Huduma kwa Mteja wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu. Picha chini ni Wajumbe wa Menejimenti wa Mahakama ya Tanzania.



Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu. Picha chini ni Watumishi wa zamani wa Kituo cha Huduma kwa Mteja.



Sehemu ya Maofisa Utumishi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni