Ijumaa, 21 Machi 2025

MAHAKAMA YA TANZANIA YAWEKA HISTORIA NYINGINE

  • Yakabidhi Magereza makasha 10 ya Mahakama Mtandao

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania leo tarehe 21 Machi, 2025 imekabidhi makasha maalumu ya kisasa yatakayotumika kwenye Magereza mbalimbali nchini kuendesha mashauri kwa njia ya mtandao bila washitakiwa na wafungwa kufikishwa mahakamani.

Makasha hayo 10 yamekabidhiwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Profesa Elisante Ole Gabriel kwa Kamishna Jenerali wa Magereza, Jeremiah Katundu kwenye tukio la kihistoria lililohudhuriwa na Waziri wa Mambo ya Ndani, Innocent Bashungwa, ambaye ndiye alikuwa Mgeni Rasmi, pamoja na Viongozi wengine Waandamizi wa Mahakama, akiwemo Msajili Mkuu, Mhe. Eva Nkya na Jeshi la Magereza.

Akizungumza katika tukio hilo, Waziri Bashungwa amempongeza Jaji Mkuu wa Tanzania, Viongozi na Mahakama kwa ujumla kwa juhudi za kuleta mabadiliko chanya kupitia Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA.

Amewapongeza pia Jeshi la Magereza kwa kupatiwa makasha hayo na Mahakama ya Tanzania, huku akibainisha kuwa kutumika kwa makasha hayo itakuwa Daraja linalounganisha Mahabusu na haki na kusaidia kupunguza gharana za usafiri na maahirisho ya mashauri ambayo yangeweza kutokea kutokana na kutokufikishwa kwa Mahabusu mahakamani.

Amesema vile vile kuwa Mahakama Mtandao inarahisisha upatikanaji wa huduma za kimahakama, kuokoa gharama za uendeshaji, kupunguza msongamano wa Wananchi mahakamani na kuwezesha Mawakili kupata rejea za hukumu na nyaraka mbalimbali kwa urahisi.

Waziri Bashungwa amesema pia kuwa Mahakama Mtandao inasaidia kuwabaini Mawakili vishoka ambao wamekuwa wakiharibu mwenendo wa kesi mbalimbali, ulinzi wa  taarifa na nyaraka na kuokoa muda wa Wananchi katika utafutaji wa haki na badala yake muda mwingi wanautumia katika shughuli za uzalishaji, hivyo kuchangia ukuaji wa Uchumi wa Nchi.

‘Ni matumaini yangu makasha haya yatatumika kwa lengo lililokusudiwa na kusaidia ufanisi katika Nyanja za utendaji haki nchini. Serikali itaendelea kushirikiana na Mahakama kuhakikisha haki inapatikana kwa wakati na kwa usawa kwa kila Mtanzania,’ amesema.

Akizungumza katika tukio hilo, Mtendaji Mkuu wa Mahakama amesema kuwa kasha hilo ni moja kati ya makasha 10 yaliyotolewa kwa Jeshi la Magereza lengo likiwa kuimarisha mnyororo wa utoaji haki nchini.

Amesema kuwa makasha kama hayo yamepokelewa katika Magereza ya Ukonga, Segerea na Keko katika jijini la Dar es Salaam, Gereza la Uyui Tabora, Isaranga  Moshi, Ruanda Mbeya, Maweni Tanga, Butimba Mwanza  Ruanda, Kisongo Arusha na Isanga Dodoma.

Prof. Ole Gabriel ameeleza kuwa makasha hayo yatasaidia kuboresha kazi za Mahakama na magereza, kwani Hakimu hatakuwa na haja ya kuwapokea wafungwa au mahabusu, Jaji akiwa Mwanza au Bukoba anaweza kumsikiliza mfungwa bila kusafiri au mshtakiwa kupelekwa mahakamani.

‘Hili litasaidia kuokoa muda na kusaidia sana katika masuala ya kiusalama kwa baadhi ya wafungwa, hasa wale hatarishi,’ alisema.

Aliwaomba Wadau wengine washiriki kuchangia na kuwezesha jambo hilo kwani nia ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Luluhu Hassan ni kuona haki inatendeka kwa haraka na mwenye haki apate haki.

Kwa upande wake, Kamishna Jenerali wa Jeshi la Magereza, Jeremiah Katungu ameupongeza Uongozi wa Mahakama kwa maboresho makubwa ambayo yemefanyika, hali ambayo imesaidia usikilizaji wa mashauri kwa wakati na Kuharakisha upatikanaji wa haki.

Amesema kuwa hatua hiyo imesaidia kupunguza msongamano wa Mahabusu na Wafungwa katika Magereza. ‘Tunayo jumla ya Magereza 129 Tanzania Bara yenye uwezo wa kuhifadhi jumla ya Wahalifu 29,902 kwa siku. ‘Kwa tarehe ya leo, jumla ya wahalifu waliopo magerezani ni 26,917, kati yao 19,528 ni wafungwa na mahabusu 7,389…

‘Idadi ya wahalifu iliyopo magerezani ndogo ikilinganishwa na uwezo wa Magereza kuhifadhi wahalifu. Haya ni matokeo ya uboreshaji wa huduma wa haki jinai unaofanywa na Serikali ya Awamu ya Sita na ushirikiano mzuri wa vyombo vyote vilivyopo katika mnyororo wa haki jinai, ikiwemo Mahakama,’ amesema.

Kamishna Jenerali ameishukuru Mahakama ya Tanzania kwa kuwezesha Mahakama Mtandao katika Magereza ambapo takribani Magereza 69 nchini yana huduma ya Mahakama Mtandao.


Moja ya Makasha ya Mahakama Mtandao yaliyokabidhiwa na Mahakama ya Tanzania kwa Jeshi la Magereza leo tarehe 21 Machi, 2025.


Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe, Innocent Bashungwa akikata utepe kuashiria upokezi wa Makasha hayo, huku Viongozi wengine wakishuhudia.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel-kushoto-akimkabidhi funguo wa Makasha hayo Kamishna Jenerali wa Magereza Jeremia Katungu.

Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Innocent Bashungwa akisaini kitabu cha wageni baada ya kuingia kwenye moja ya Makasha hayo.


Waziri wa Mambo ya Ndani, Mhe. Innocent Bashungwa akizungumza kwenye hafla ya makabidhiano ya Makasha hayo.


Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akizungumza katika hafla hiyo. Picha chini ni Kamishna Jenerali wa Magereza, Afande Jeremia Katungu.




Makamishna na Viongozi Waandamizi wa Magereza-juu na chini- wakiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu.




Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania wakiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu.


Wakuu wa Vyombo vya Ulinzi na Usalama Mkoa na Wilaya ya Dodoma wakiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu.


Hakuna maoni:

Chapisha Maoni