Ijumaa, 21 Machi 2025

WIZARA YA KATIBA NCHINI JAPAN YAAHIDI KUTOA USHIRIKIANO KWA MAHAKAMA YA TANZANIA

  •  Washangazwa na maendeleo pamoja na matumizi makubwa ya TEHAMA katika uendeshwaji wa Mashauri
  • Wadhamiria kuanzisha na kuimarisha mahusiano na Mahakama ya Tanzania

Na NAOMI KITONKA, Mahakama- Dar es Salaam

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof.  Elisante Ole Gabriel amepokea wageni kutoka nchini Japan waliokuwa katika ziara yao ya kikazi katika Ubalozi wa Japan hapa nchini jana tarehe 20 Machi 2025 katika jengo la Mahakama ya Rufani.

Ziara hiyo ilifanyika ikiwa na lengo la kuanzisha mahusiano na kuangalia fursa mpya nchini kwa kukutana na wataalamu wa masuala ya sheria wa Tanzania na kuelezea mchango wa Japan katika kuendeleza rasilimali watu na sheria katika nchi nyingine.

Akizungumza katika ziara hiyo Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel alifungua kwa kusema, “Tunayo furaha kubwa kuwakaribisha nchini Tanzania kipekee katika Mahakama yetu ya Tanzania ambayo ni Mhimili muhimu katika kuwapatia haki wananchi na ujio wenu utakuwa fursa kubwa ya kuimarisha mahusiano kati yetu.”

Prof. Ole Gabriel alisema Mahakama ya Tanzania kwa sasa imepiga hatua kubwa katika shughuli zake kwa kushirikiana na Chama cha Mawakili Tanganyika (TLS) na Chuo cha Uongozi  wa Mahakama Lushoto (IJA) pamoja na Idara ya Mafunzo kuhakikisha Maafisa wote wa Mahakama pamoja na watumishi wengine wanajengewa uwezo binafsi katika utafiti na mafunzo yatakayowasaidia katika kukamilisha majukumu ya Kimahakama kwa haraka na ubora.

Aidha, katika mazungumzo hayo, wageni hao walipata ufafanuzi juu ya shughuli mbalimbali zinazofanywa na Mahakama ya Tanzania hasa katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) katika usikilizwaji wa mashauri kwa njia ya mtandao, Mfumo wa Usimamizi wa Mashauri (eCMS) na Mfumo wa Unukuzi na Tafsiri (TTS) ambayo kwa kiasi kikubwa imechangia zoezi la upatikanaji haki kwa haraka.

“Mahakama ya Tanzania tumedhamiria kuhakikisha wananchi wanapata haki kwa ubora, haraka na kwa wakati, wakati mwingine bila hata kuwa na ulazima wa kufika mahakamani kutokana na maendeleo ya Sayansi na Teknolojia huku ikikumbana na changamoto mbalimbali ikiwa ni pamoja na suala la rushwa,” alisema.

Mtendaji Mkuu aliongeza kuwa, mabadiliko ya TEHAMA na kupitia ujio wa wageni hao anatumaini utawezesha kupunguza tofauti ya TEHAMA kati ya Mahakama na wadau wake wakubwa mfano Jeshi la Polisi na Jeshi la Magereza kwa sababu Japani wapo mbele zaidi katika maendeleo ya Sayansi na Teknolojia na wanatambua mchango mkubwa wa matumizi yake katika zoezi la utoaji haki pamoja na usuluhishi.

“Pia hii itasaidia utamaduni wa Mahakama kujulikana kwa wananchi katika kipindi hiki na kuwatoa wasiwasi hasa katika matumizi ya mtandao na mifumo katika ufunguaji wa mashauri na matumizi ya akili mnemba yaani (AI) na kuwa katika daraja la kwanza kwenye matumizi ya Teknolojia” alisisitiza Prof. Ole Gabriel.

Wageni hao waliongozwa na Mkuu wa Msafara huo, Bw. Ryota Tatemoto ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Taasisi ya Utafiti na Mafunzo wa Wizara ya Katiba ya nchini Japan.

“Ofisi yetu inahudumia nchi zaidi ya 10 za Kiasia na tumeona ni muhimu kuanza kutoa huduma zetu kwa kushirikiana na nchi nyingine katika nchi za Afrika na kuanzisha ushirikiano wa Kimahakama na fursa hiyo tukaiona nchini Tanzania na huu ni wakati mzuri wa sisi kujifunza kutoka kwenu nanyi kujifunza kutoka kwetu hasa katika ushirikiano wa Mafunzo na Utafiti pamoja na kubadilishana uwezo katika utendaji kazi wetu,” alisema Bw. Tatemoto.

Wageni hao kutoka Japan waliambatana na Mwakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Regina Ulomi aliipongeza Mahakama ya Tanzania kwa jitihada kubwa inayofanya katika zoezi la utoaji haki.

Kadhalika Bi. Regina alizungumzia kuhusu majukumu ya Wizara hiyo ambapo alisema, “Kazi yetu sisi kama Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki ni kuhakikisha  fursa zote za kimaendeleo zinapelekwa katika sehemu husika na wageni hawa wamelenga Mahakama ya Tanzania ili kujifunza na kubadilishana uzoefu kwenye masuala ya Kimahakama, matumizi ya Teknolojia, kujengeana uwezo, utafiti, mafunzo pamoja na kujifunza njia mbalimbali za usuluhishi.

Ziara hiyo ilihudhuriwa pia na Bw. Kazuaki Takahashi, Jaji na Mwendesha Mashtaka kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Taasisi ya utafiti na Mafunzo wa Wizara ya Katiba ya Japan, Bw. Rui Higuchi, Katibu wa Tatu kutoka Ubalozi wa Japan, Bi. Yoshino Shibata, Msajili wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Herbert George na Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo upande wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (kushoto) akisalimiana na Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Taasisi ya Utafiti na Mafunzo wa Wizara ya Katiba ya Japan, Bw. Ryota Tatemoto  wakati wa ziara yao walipomtembelea Mtendaji Mkuu ofisini Mahakama ya Rufani Dar es Salaam jana tarehe 20 Machi 2025.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akisisitiza jambo wakati wa ziara ya wageni kutoka Ubalozi wa Japan na Wizara ya Katiba ya Japan walipomtembelea Ofisini kwake jana tarehe 20 Machi, 2025.


Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Taasisi ya utafiti na Mafunzo wa Wizara ya Katiba ya Japan, Bw. Ryota Tatemoto akizungumza mbele ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) walipomtembelea ofisini kwake jana tarehe 20 Machi 2025.


Mwendesha Mashtaka kutoka Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Taasisi ya utafiti na Mafunzo wa Wizara ya Katiba ya Japan, Bw. Kazuaki Takahashi akisisitiza jambo wakati wa mazungumzo na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) walipomtembelea ofisini kwake jana tarehe 20 Machi, 2025.

Mkurugenzi Msaidizi wa Mafunzo wa Mahakama ya Tanzania, Bi. Patricia Ngungulu akitoa ufafanuzi wa shughuli zinazofanywa na Idara ya Mafunzo kwa wageni kutoka Japan waliofanya ziara ya kumtembelea Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel.

Mwakilishi kutoka Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Bi. Regina Ulomi (kulia) akitoa ufafanuzi wa  jambo fulani mbele ya Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) walipomtembelea ofisini kwake tarehe 20 Machi 2025.

Wageni  kutoka Wizara ya Katiba ya Japan wakimsikiliza kwa makini Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (hayupo katika picha) wakati wa ziara yao walipomtembelea katika ofisi yake ndogo Mahakama ya Rufani Dar es Salaam jana tarehe 20 Machi, 2025.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akipokea zawadi kutoka kwa Bw. Ryota Tatemoto ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Taasisi ya utafiti na Mafunzo wa Wizara ya Katiba ya Japan wakati wa ziara yao kwa Mahakama ya Tanzania.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Bw. Ryota Tatemoto (wa pili kushoto) ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Idara ya Ushirikiano wa Kimataifa na Taasisi ya utafiti na Mafunzo wa Wizara ya Katiba ya Japan (wa pili kushoto), wengine ni Maafisa kutoka Wizara ya Katiba ya Japan.

Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akiwa katika picha ya pamoja na ujumbe kutoka Wizara ya Katiba ya Japan pamoja na sehemu ya Viongozi wa Mahakama walioshiriki katika mazungumzo na ugeni huo.

(Habari hii imehaririwa na MARY GWERA, Mahakama-Arusha)

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni