Jumatatu, 17 Machi 2025

UZINDUZI JENGO LA MAKAO MAKUU YA MAHAKAMA TANZANIA KUFANYIKA APRILI

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Mwanza

Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan atazindua rasmi jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania lililopo katika eneo la Tambuka Reli jijini Dodoma tarehe 8 Aprili, 2025.

Hayo yamebainishwa leo tarehe 17 Machi, 2025 na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma alipokuwa anafungua Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu, Kanda na Divisheni, kinachofanyika kwa siku tatu katika Hoteli ya Malaika jijini hapa.

‘Tarehe 8 Aprili, 2025 ni siku muhimu sana kwa Mahakama. Hilo ni jengo la kisasa. Tunawaomba wale watakaolitumia jengo hili wahakikishe kwamba linakuwa kweli la kisasa hata kwa huduma, siyo kwa muonekano tu,’ amesema.

Mhe. Prof. Juma ameeleza kuwa jengo hilo limejengwa kwa asilimia 100 na kodi za Wananchi na halikutokana na mradi wa Benki ya Dunia na kwamba jumla ya kiasi cha Shilingi za Kitanzania bilioni 129.7 zimetumika kwenye mradi huo.

‘Kwa hiyo, jengo hili ni mali ya Wananchi wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tuhakikishe kwamba jengo hili linakuwa la kisasa kweli, vyumba vyake vinakuwa na teknolojia. Lazima iwe tofauti na Mahakama zingine unapoingia kwenye Mahakama ya karne ya 21,’ Jaji Mkuu amesema.

Mhe. Prof. Ibrahim Juma amesisitiza matumizi ya mkutano mtandao wakati wa kusikiliza mashauri kwenye jengo hilo, hatua itakayochochea kupunguza mlundikano mahakamani.

Hivyo amewahimiza Majaji Wafawidhi kuwasaidia Magereza ili wawe na vyumba vizuri wezeshi vitakavyotumia teknolojia hiyo kutokana na changamoto inayowakabili ya kuwasafirisha Wafungwa wanaokata rufaa kutoka Magereza ya mbali na kuwaleta mahakamani.

‘Kuwasafirisha Wafungwa pengine kuwaleta Arusha, kutoka Songea kwenda Moshi ni gharama kubwa na kiusalama siyo salama. Magereza wametuomba tuongeze matumizi ya teknolojia katika kusikiliza mashauri,’ amesema.

Kazi za ujenzi katika mradi huo zilianza Julai 2020 na Jaji Mkuu wa Tanzania aliweka jiwe la msingi wa jengo hilo tarehe 26 Januari, 2022. Jengo hilo lipo kwenye eneo la ukubwa wa hekta 18.9, takribani hekali 45.

Akiwasilisha taarifa ya ujenzi katika hafla ya kuweka jiwe la msingi, Mtedaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel aliishukuru Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kutoa fedha za utekelezaji wa mradi huo kwa wakati.

Kwa mujibu wa Mtendaji Mkuu, kwa miaka mingi Mhimili wa Mahakama haukuwa na jengo la Makao Makuu, hivyo jitihada zilizanza mwaka 2013. Jengo hilo ilikuwa lijengwe katika eneo la Chimala jijni Dar es Salaam, karibu na jengo refu lile linalochungulia Ikulu ya Magogoni.

Alisema kuwa baada ya mipango ya Serikali kuwa Makao Makuu ya Nchi yanahamia Dodoma, mchakato huo uligeuza mwelekeo na ikaonekana jengo hilo lijengwe jijini Dodoma.

Prof. Ole Gabriel alisema kuwa mwaka 2017 mchakato huo ulipata msukumo pale ambapo Jaji Mkuu mwenyewe ulipoongea na Rais wa Awamu ya Tano, Hayati Dkt John Pombe Magufuli ili kuweza kupata eneo jijini Dodoma.

“Baada ya hapo kasi iliongezeka ambapo majadiliano yaliendelea na iliyokuwa Mamlaka ya Ustawishaji Makao Makuu (CDA) na baadaye Mamlaka ya Jiji la Dodoma na eneo hili likapatikana,’ alisema.

Mtendaji Mkuu aliwataja wanaosimamia ujenzi ni CRJE, Kampuni ya Kichina ambao wamefanya kazi kubwa na kazi yao ni ya viwango vya hali ya juu, huku akibainisha Wasanifu wa jengo hilo wakiwa ni Acquise Achtectural Design ambao ni wazalendo.

Alibainisha pia kuwa jengo hilo lina matawi matatu ambayo ni Mahakama ya Upeo (Supreme Court), Mahakama ya Rufani na Mahakama Kuu. Prof. Ole Gabriel alieleza kuwa matawi hayo yanatengeneza jengo katikati litakalokuwa linatumika kama ofisi za utawala.


Mwonekano wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania litakalozinduliwa rasmi na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma akizungumza wakati anafungua Kikao cha Mwaka cha Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni ambapo ametumia fursa hiyo kutangaza tarehe ya ufunzi rasmi wa Jengo la Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania.


Sehemu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni-juu na chini-wakimsikiliza Jaji Mkuu kwenye Kikao hicho.

Sehemu nyingine ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni-juu na chini-wakimsikiliza Jaji Mkuu kwenye Kikao hicho.



Sehemu nyingine ya tatu ya Majaji Wafawidhi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda na Divisheni-juu na picha mbili chini-ikiwa kwenye Kikao hicho.



Sehemu ya Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania-juu na chini-wakimsikiliza Jaji Mkuu kwenye Kikao hicho.


Sehemu nyingine ya Viongozi Waandamizi wa Mahakama ya Tanzania-juu na chini-wakimsikiliza Jaji Mkuu kwenye Kikao hicho.

 

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni