Jumatano, 30 Aprili 2025

WAZIRI KATIBA NA SHERIA AELEZA BUNGE KASI UONDOSHAJI MASHAURI, MABORESHO MIUNDOMBINU MAHAKAMANI

  • Wabunge wakoshwa na Mtendaji Mkuu kwa uchapakazi

Na ARAPHA RUSHEKE na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Mahakama ya Tanzania imeendelea kuchukua hatua mbalimbali, ikiwemo kuboresha miundombinu ya majengo ili kusogeza huduma karibu na Wananchi na kuongeza kasi ya usikilizaji wa mashauri, hivyo kuwezesha upatikanaji wa haki kwa haraka na gharama nafuu.

Akiwasilisha bungeni hotuba ya Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara kwa mwaka wa fedha 2025/2026 jijini Dodoma leo tarehe 30 Aprili, 2025, Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro amesema kuwa kwa kipindi cha Julai, 2024 hadi Aprili, 2025 kulikuwa na jumla ya mashauri 238,154 mahakamani.

Mhe. Dkt. Ndumbaro amebainisha kuwa kati ya mashauri 238,154 yaliyokuwepo, mashauri 174,581 yalisikilizwa na kuhitimishwa na mashauri 63,573 yanaendelea katika hatua mbalimbali.

‘Mashauri yenye umri mrefu mahakamani ni 2,780, sawa na asilimia 4 ya mashauri yote yaliyobaki. Mashauri 1,325 yapo Mahakama ya Rufani; 189 yapo Mahakama Kuu; 553 yapo Mahakama za Hakimu Mkazi na Wilaya na 713 yapo Mahakama za Mwanzo…

‘Pia, katika Mahakama Kuu Divisheni ya Makosa ya Rushwa na Uhujumu Uchumi, jumla ya mashauri 59 yalibakia mwishoni mwa Juni 2024, 118 yalisajiliwa, 108 yalisikilizwa na 69 yalibakia,’ amesema.  

Waziri wa Katiba na Sheria ameliambia Bunge pia kuwa Mahakama ya Tanzania imeendelea kushirikiana na Wadau wake katika mnyororo wa haki jinai ili kuhakikisha mashauri yanamalizika kwa wakati.

Amebainisha kuwa tarehe 06 Aprili, 2025 Mahakama iliitisha kikao kazi cha pamoja kilichohusisha Wadau kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa, Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali na Ofisi ya Taifa ya Mashtaka.

Wadau wengine waliohudhuria kikao hicho ni Chama cha Mawakili Tanganyika, Idara ya Ustawi wa Jamii, Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza pamoja na Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya.

‘Kupitia kikao hicho, wajumbe walijadili taarifa ya hali ya mashauri ya mlundikano mpaka kufikia Desemba -2024, hali ya mahabusu magerezani na mkakati wa kupunguza mlundikano na matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano-TEHAMA-kwenye usikilizaji wa rufaa na maombi.

Akizungumzia uteuzi wa Majaji, Waziri Ndumbaro ameliambia Bunge kuwa katika mwaka wa fedha 2024/2025, jumla ya Majaji 10 wameteuliwa (Mahakama Kuu – 5 na Mahakama ya Rufani – 5) na hivyo kufanya idadi ya Majaji waliopo kufikia 146 (Mahakama Kuu – 107 na Mahakama ya Rufani - 39).

Vilevile, Waziri wa Katiba na Sheria ameeleza kuwa Mahakimu 91 wameajiriwa na hivyo kufanya idadi ya Mahakimu kufikia 1,426 (Mahakama za Mwanzo - 195 na Mahakama za Hakimu Mkazi - 1,231).

Kuhusu miundombinu ya majengo, Bunge limefahamishwa kuwa Mahakama ya Tanzania imeendelea na utekelezaji wa Mpango wa Ujenzi na Ukarabati wa Miundombinu ya Mahakama wa Miaka Mitano (2021/2022 – 2025/2026).

‘Lengo la Mpango huo ni kuboresha na kusogeza huduma za Mahakama karibu na Wananchi ili kuwapunguzia gharama na muda wanaoutumia kupata huduma za Mahakama,’ Mhe. Ndumbaro amesema.

Amebainisna kuwa katika mwaka wa fedha 2024/2025 hadi kufikia Aprili, 2025 hali ya ujenzi na ukarabati wa majengo mbalimbali ya Mahakama inaonesha kuwa ujenzi wa Vituo Jumuishi vya Utoaji Haki tisa (9) ktika Mikoa ya Katavi, Songea, Songwe, Njombe, Simiyu, Lindi, Singida, Pemba na Geita unaendelea kwa viwango tofauti.

‘Ujenzi wa majengo ya Mahakama za Wilaya 11 na Mahakama za Mwanzo 72 unaendelea vizuri katika maeneo mbalimbali nchini, huku ukarabati wa jengo la zamani la Mahakama Kuu Dodoma umefikia asilimia 57,’ amesema.

Waziri Ndumbaro ameeleza pia kuwa ujenzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama umekamilika na kuzinduliwa tarehe 05 Aprili, 2025; ujenzi wa nyumba za Majaji eneo la Iyumbu Dodoma umekamilika na kuzinduliwa tarehe 05 Aprili, 2025, huku ujenzi wa nyumba ya Jaji Mkuu, jijini Dodoma ukiwa unaendelea. 

Uwasilishaji wa hotuba hiyo ulihudhuriwa na Viongozi mbalimbali wakiwemo kutoka Mahakama ya Tanzania, Majaji wa Mahakama ya Rufani, Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania na Msajili Mkuu wa Mahakama ya Tanzania.

Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania walishindwa kujizuia na kuibuka kwa shangwe baada ya Naibu Spika wa Bunge, Mhe. Mussa Azzan Zungu kumtambulisha Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel. Kitendo hicho kiliibua shangwe na fifijo bungeni, huku Wabunge wakimpongeza kwa makofi ya kutosha na kumfanya Naibu Spika kutulia kwa muda kabla ya kuendelea na shughuli za Bunge.


Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro-juu na chini-akionesha mkoba uliobeba Hotuba ya Bajeti ya Mwaka wa Fedha 2025/2025 mara baada ya kuwasili kwenye viunga vya Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kusoma hotuba ya Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yake leo tarehe 30 Aprili, 2025.


Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro akiingia bungeni. Picha chini akiwa tayari bungeni tayari kwa kusoma hotuba yake.


Waziri wa Katiba na Sheria, Mhe. Dkt. Damas Ndumbaro-juu na chini- akiwasilisha bungeni Mpango na Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara yake leo tarehe 30 Aprili, 2025.


Jaji wa Mahakama ya Rufani Tanzania, Mhe. Dkt. Mary Levira akitambulishwa bungeni kama miongoni mwa Viongozi wa Mahakama waliohudhuria uwasilishaji wa hotuba hiyo. picha chini ni Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania , Prof. Elisante Ole Gabriel akipokea kwa heshima pongezi za Wabunge baada ya kupigiwa makofi ya kutosha yaliyomfanya Naibu Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Mussa Azzan Zungu kutulia kwa muda kuendelea na shughuli za Bunge.


Viongozi wa Mahakama ya Tanzania na wengine kutoka Wizara ya Katiba na Sheria-juu na chini-wakifuatilia shughuli za Bunge wakati wa uwasilishaji wa bajeti ya Wizara hiyo.


Picha na ARAPHA RUSHEKE-Mahakama, Dodoma





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni