Alhamisi, 10 Aprili 2025

JAJI MKUU ATAKA UIMARISHAJI HUDUMA MAHAKAMA ZA MWANZO

Na FAUSTINE KAPAMA-Mahakama, Dodoma

Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma amewahimiza Viongozi wa Mahakama kuchukua hatua stahiki ili kuimarisha huduma ya utoaji haki katika Mahakama za Mwanzo nchini.

Mhe. Prof. Juma ametoa wito huo leo tarehe 10 Aprili, 2025 alipokuwa anafungua Kikao cha siku mbili cha Baraza la Wafanyakazi Taifa kinachofanyika katika Ukumbi wa PSSSF jijini Dodoma.

‘Ni ukweli usiopingika kuwa Mahakama za Mwanzo zinaongoza kuwa na mashauri mengi kwa asilimia zaidi ya 70 ya mashauri yote yanayofunguliwa katika Mahakama zetu. Kwa maana nyingine, Mahakama za Mwanzo ndizo zinazohudumia Wananchi wengi zaidi ya Mahakama nyingine hapa nchini,’ amesema.

Jaji Mkuu amebainisha kuwa katika Mpango Mkakati wa Miaka Mitano ijayo, ni lazima Viongozi na Watumishi waelekeze nguvu zao katika kuimarisha ubora wa huduma za haki katika ngazi ya Mahakama za Mwanzo.

Mhe. Prof. Juma amenukuu hotuba ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliyoitoa katika hafla ya uzinduzi wa jengo la Makao Makuu ya Mahakama hivi karibuni.

Katika hotuba yake, Rais Samia, pamoja na kupongeza jitihada za Mahakama katika kutekeleza jukumu lake la utoaji haki, alisisitiza uongozi wa Mahakama kutupia jicho zaidi katika Mahakama za Mwanzo ambazo bado zinalalamikiwa na Wananchi.

‘Tunafahamu kuwa Mahakama za Mwanzo bado zina changamoto nyingi za miundombinu, rasilimali watu na fedha. Ninawasihi Viongozi wa Mahakama katika Kanda, Mikoa na Wilaya, zingatieni idadi ya watu katika maeneo mnayopendekeza ujenzi wa Mahakama za Mwanzo,’ amesema.

Jaji Mkuu amewapongeza Watumishi wote wa Mahakama kwa kuendelea kufanya kazi kwa uadilifu, ueledi, uwajibikaji na kwa kulenga matokeo makubwa.

Amebainisha kuwa kwa mujibu wa Ibara ya 107A ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhimili wa Mahakama ni Mamlaka yenye Kauli ya Mwisho katika utoaji haki katika Jamhuri ya Muungano.

Mhe. Prof. Juma amesema kuwa Ibara ya 107B ya Katiba inatamka kuwa katika kutekeleza mamlaka ya utoaji haki, Mahakama zote zitakuwa huru na zitalazimika kuzingatia tu masharti ya Katiba na yale ya Sheria.

‘Ibara hizi zinatarajia Watumishi kujipanga kimkakati na kuzingatia uadilifu, ueledi, uwajibikaji na kwa kulenga matokeo makubwa,’ Jaji Mkuu amesema.

Akizungumzia maslahi ya Watumishi, Mhe. Prof. Juma alibainisha kuwa anafahamu kuwa bado suala hilo linahitaji kufanyiwa kazi kwa karibu na Viongozi wa Mahakama.

Amekumbushia kuwa wakati akizindua Jengo la Makao Makuu ya Mahakama, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan aliwakumbusha kuwa bado michakato na majadiliano ya maboresho ya maslahi kwa Watumishi wa Mahakama inaendelea.

‘Sisi kama Viongozi wa Mahakama tumekuwa tukijadiliana na Serikali kuhusu maslahi ya Watumishi wa Mahakama na ndiyo maana baadhi yenu mtakuwa mashuhuda kuwa juhudi hizo zimezaa matunda,’ amesema.

Meza Kuu ikiongozwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma-katikati-baada ya ufunguzi wa Kikao cha Baraza la Wafanyakazi Taifa leo tarehe 10 Aprili, 2025. Wengine katika picha kutoka kulia ni Jaji wa Mahakama ya Rufani, Mhe. Augustine Mwarija, Katibu wa Baraza, Bw. Ezra Kyando, Katibu Msaidizi wa Baraza, Mhe. Christina Mlwilo na Jaji Kiongozi wa Mahakama Kuu ya Tanzania, Mhe. Dkt. Mustapher Mohamed Siyani.

Meza Kuu na Makamishana na Viongozi wa Tume ya Utumishi ya Mahakama.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Mororogo. Picha chini ni wajumbe kutoka Kanda ya Dar es Salaam.



Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Arusha. Picha chini ni wajumbe wa Kanda ya Tabora.



Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Divisheni ya Ardhi. Picha chini ni wajumbe wa Divisheni ya Kazi.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Bukoba. Picha chini ni wajumbe wa Kanda ya Manyara. 



Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Musoma. Picha chini ni wajumbe wa Divisheni ya Biashara.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Iringa. Picha chini ni wajumbe wa Kanda ya  Mwanza.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Dodoma. Picha chini ni wajumbe wa Kanda ya Moshi.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Mbeya. Picha chini ni wajumbe wa Kanda ya Kigoma.



Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Mtwara. Picha chini ni wajumbe wa Divisheni ya Rushwa na Uhujumu Uchumi.



Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Tanga. Picha chini ni wajumbe wa Kituo cha Usuluhishi.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kanda ya Shinyanga. Picha chini ni wajumbe wa Kanda ya Songea.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Kituo Jumuishi Masuala ya Familia Temeke. Picha chini ni wajumbe wa Kanda ya Geita.


Meza Kuu na wajumbe wa Baraza kutoka Mahakama ya Rufani. Picha chini ni wajumbe wa Mahakama Kuu, Masjala Kuu.



Meza Kuu na wajumbe wa Menejimenti ya Mahakama ya Tanzania-juu na chini. Picha ya pili chini ni Kamati ya Maandalizi ya Kikao cha Baraza.





Hakuna maoni:

Chapisha Maoni